Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) limeendelea kuchanua likiandika historia mbili mpya moja ikiwa kutoa gawio la Shilingi Bilioni 10 kwa Serikali kwa mara ya kwanza, pili ni kuingia kwa mara ya kwanza katika kundi la taasisi za umma zilizotoa gawio la zaidi ya Shilingi Bilioni 10 kwa Serikali.
Hatua hiyo ya NHC inatajwa ni kudhihirika kwa kuwa na
kiwango bora cha utendaji lakini pia sha kuimarika kwa utendaji wake na mchango
wake katika uchumi wa Taifa.
Akizungumza katika hafla ya utoaji wa gawio kwa Serikali na tuzo iliyoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu
Hassan, Juni 30,2026, Msajili wa Hazina, Nehemia Mchechu, amesema idadi ya
taasisi zilizofikisha kiwango hicho imeongezeka kutoka taasisi sita za mwaka
uliopita ambapo kwa mwaka huu zimefikia taasisi kumi kutokana na maboresho
makubwa ya utendaji katika taasisi za umma.
Kwa mujibu wa Mchechu, mwaka uliopita taasisi hizo sita
zilichangia jumla ya Shilingi Bilioni 267, ambapo kwa mwaka huu taasisi kumi zimechangia
Shilingi Bilioni 481.
“Ongezeko hilo linaakisi mafanikio ya mageuzi na usimamizi
madhubuti wa uwekezaji wa Serikali kwenye mashirika ya umma,” amesema Mchechu.
Akiizungumza kuhusu NHC, Mchechu amesema shirika hilo ni
miongoni mwa taasisi mpya zilizoingia kwenye orodha hiyo mwaka huu, baada ya
kutoa gawio la Shilingi Bilioni 10, tofauti na mwaka uliopita ambapo haikufikia
kiwango hicho.
“Mafanikio haya yanaonesha namna NHC inavyoendelea
kuimarisha utendaji wake wa kifedha, huku ikiendelea kutekeleza dhamira yake ya
kujenga makazi bora, kuendeleza miradi ya kimkakati na kuongeza thamani kwa
Serikali pamoja na wananchi,” amesema Mchechun a kuongeza;
“Hatua hii ni ushahidi kuwa uwekezaji wa Serikali kupitia
NHC unaendelea kuzaa matunda, huku Shirika likiendelea kuwa nguzo muhimu katika
maendeleo ya sekta ya makazi na uchumi wa Taifa.”

Chapisha Maoni