TAWA KANDA MAALUM DAR YAHIMIZA UHIFADHI WALIO HATARINI KUTOWEKA

-Yaadhimisha Siku ya Wanyamapori Duniani

-Yaita wananchi kujionea vivutio vya mjini

 Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Mamlaka ya Uhifadhi Wanyamapori nchini (TAWA), Kanda Maalum ya Dar es Salaam, leo Machi 3, 2026, imeungana na wadau wengine wa sekta hiyo katika kuadhimisha Siku ya Wanyamapori Duniani, inayoadhimishwa Machi 3 kila mwaka, ikihimiza jamii kushiriki katika kulinda wanyama walio katika hatari ya kutoweka  kwa faida ya taifa leo na vizazi vijavyo.

Kamishna Msaidizi Mwandamizi, Sylvester Mushy 

Kamanda wa Uhifadhi Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Kamishna Msaidizi Mwandamizi, Sylvester Mushy ametoa wito huo ofisini kwake jijini Dar es Salaam leo Machi 3, 2026  alipokuwa akizungumzia maadhimisho hayo yaliyobeba Kauli mbiu isemayo; ‘Mimea dawa, manukato, uhifadhi urithi na kuboresha maisha.’

Amesema kauli mbiu hiyo inahamasisha wananchi kutunza hifadhi wanyama pori na mimea, lakini pia TAWA imetumia siku hiyo kuwapa elimu na kuwahamasisha wananchi kujifunza kudhibiti wnyama wakali waharibifu wa mimea kama tembo kwa kutumia mimea ambayo huwafukuza badala ya kuwaua.

“Leo ni Siku Kuu, Dunia inapokumbuka umuhimu wa uhifadhi wanyamapori. Kwa mwaka huu kitaifa siku hii inaadhimishwa mkoani Arusha. Wananchi wanapaswa kupata uelewa wa manufaa ya wanyamapori na mimea na kushiriki kuifadhi,” amesema Mushy na kuongeza:

“Mfano katika kudhibiti Wanyama wakali waharibifu, TAWA inafundisha wananchi kutumia pilipili kichaa, kwa kupanda kando ya mashamba yao au kuzisaga na kumwaga maeneo hayo ili kuwafukuza tembo wasiharibu mazao.”

Kamishna Msaidizi Mwandamizi, Mushy amesema wananchi hasa vijana wana fursa kutembelea maeneo mbalimbali ya vivutio na hifadhi yaliyo chini ya mamlaka hiyo, ikiwamo hifadhi za mjini kama Msitu wa Pande Dar es Salaam wenye wanyama mbalimbali ikiwamo simba na duma.

Ametaja vivutio vingine ndani ya kanda hiyo maalum kuwa ni Magofu ya Kunduchi yaliyobeba historia ya waswahili na Hifadhi ya Wami Mbiki iliyopo Morogoro nili kujifunza, kuburudika na kujionea shughuli za uhifadhi wanyamapori na mimea zinavyofanyika.

Akizungumzia zaidi maadhimisho ya Siku ya Wanyamapori Duniani, Kamanda huyo wa Uhifadhi Kanda Maaluma ya Dar es Salaam amesema chimbuko lake ni Kikao cha 68 cha Baraza Umoja wa Mataifa wa mwaka 2013, ambapo Tanzania imesaini mkataba huo unaozuia uwindaji na usafirishaji wa Wanyama na mimea iliyo katika hatari ya kutoweka.

Naye Ofisa Mhifadhi Mwandamizi anayeshughulikia pia Ujirani Mwema TAWA Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Sanjo Mafuru (pichani chini), ametaja baadhi ya wnyama walio katika hatari ya kutoweka kuwa ni Pamoja na Mbwa mwitu, tembo, faru weusi na sokwe.

Amesisitiza kwamba wananchi wanapaswa kupata uelewa wa manufaa ya wanyamapori na mimea lakini pia kushiriki katika kuwalinda wanyama hao.

“TAWA inawakumbusha vijana, wanawake na wazee kwamba ni muhimu kufuatilia elimu ya uhifadhi na kushiriki kweny uhifadhi kwa kuwa uhifadhi wa Wanyama na mimea una faida kiuchumi, kiutamaduni, kimazingira. Bila wanyamapori hakuna utalii, tukumbuke asilimia 17 ya Uchumi unachangiwa na utalii,” amesema Sanjo na kuongeza;

“Tushikamane katika kuhifadhi misitu na wanyamapori, kuna faida katika kuhifadhi wanyamapori na misitu kwani pia katika mzunguko wa maisha, binadamu, mime ana Wanyama tunategemeana.”

 

 

 

 


Post a Comment

Mpya zaidi Nzee zaidi