Kapteni Traole afuata huduma za afya nchini

 - Aichagua JKCI kupata huduma za kibingwa 

- Burkina Faso yasaini makubaliano na JKCI 

Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Rais wa Burkina Faso,Kapteni Ibrahim Traore amefuata huduma bora za afya zinazotolewa nchini, hasa za magonjwa ya moyo.

Rais wa Burkina Faso, Kapteni Ibrahim Traore

Ndivyo unavyoweza kueleza, baada kiongozi huyo maarufu duniani,kutuma mwakilishi wake wa masuala ya afya Burkina Faso nchini kuzungumza na kutiliana saini hati ya makubaliano na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), katika kutoa huduma bobezi ya matibabu ya  magonjwa ya moyo.

Kwa mujibu wa JKCI, hati hizo zimesainiwa kati ya  Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dk. Peter Kisenge na Mshauri wa Rais wa Burkina Faso na Mratibu wa Kitaifa wa Mpango wa Afya wa Rais, Drissa Traore, jana jijini Dar es Salaam.

Akizungumza baada ya kusaini makubaliano hayo, Dk. Kisenge amesema makubaliano hayo yataimarisha utoaji wa  huduma za matibabu ya moyo nchini Burkina Faso na kuokoa maisha ya wananchi wenye matatizo ya moyo.

“Tumekubaliana kuwasaidia katika kufanya tatifi, kuwafundisha  wataalamu wa afya wakiwemo madaktari, wauguzi na wataalamu wa vifaa tiba jinsi ya kuwatibu wagonjwa wa moyo na namna ya kutumia vifaa tiba vya moyo, pia watatuma wagonjwa walioshindwa kuwafanyia upasuaji, waje kutibiwa kwenye taasisi yetu.”

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dk. Peter Kisenge (Wa pili kushoto) na Mshauri wa Rais wa Burkina Faso na Mratibu wa Kitaifa wa Mpango wa Afya wa Rais, Drissa Traore (Wa pili kulia), wakisaini hati ya makubaliano ya ushirikiano katika utoaji huduma za kibingwa na mafunzo kwa wataalam wa nchi hiyo.

“Katika kutoa mafunzo ya kutibu wagonjwa ya moyo kuna wataalamu wetu watakwenda Burkina Faso kufundisha na kuna wataalamu kutoka nchini humo watakaokuja  kujifunza katika taasisi yetu,” amesema Dk. Kisenge

Dk. Kisenge ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo, amesema kuhusu upatikanaji wa vifaa tiba, wamekubaliana wanunue katika  Bohari ya Dawa nchini(MSD), ambao ni wasambazaji wa vifaa hivyo JKCI.

“Kwa namna ya kipekee namshukuru sana Mhe. Rais Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuimarisha tiba ya magonjwa ya moyo katika taasisi yetu,  kitu ambacho kimesababisha nchi mbalimbali kuja kujifunza namna ya kutoa matibabu ya moyo katika nchi zao, pia kuwaleta wagonjwa wao kutibiwa JKCI;

“Pia ninamshukuru Rais wa Bukina Faso, Kapteni Ibrahim Traore kwa kuiamini nchi yetu na kuwatuma wataalamu wake, ambao tumesaini makubaliano nao ili nao kupitia sisi wawe taasisi bora ya matibabu ya moyo na kufika hatua tuliyoifikia sisi.Leo tumeingia katika historia na Burkina Faso ya kutangaza utalii tiba, ambao umekuja katika afya,” amesema Dk. Kisenge.

Kwa upande wake, Mshauri wa Rais wa Burkina Faso na Mratibu wa Kitaifa wa Mpango wa Afya wa Rais,  Drissa Traore ambaye kwa mara ya pili ameongoza timu hiyo ya wataalamu kuja hapa nchini, amesema siku ya kwanza walipotembelea JKCI walivutiwa kwa huduma wanazozitoa pamoja na uhusiano mzuri wa uongozi na manejimenti uliokuwepo, baada ya kurudi nchini kwao walivichukua hivyo vyote na kuvifanyia kazi.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dk. Peter Kisenge (Kulia) na Mshauri wa Rais wa Burkina Faso na Mratibu wa Kitaifa wa Mpango wa Afya wa Rais, Drissa Traore wakibadilishana hati ya makubaliano ya ushirikiano.

“Ninawashukuru maraisi wetu wa Burkina Faso, Kapteni Ibrahim Traore na wa Tanzania Mhe. Dk. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa tayari kuimarisha huduma za afya katika nchi zao, nimevutiwa na JKCI kwani haitoi huduma tu Tanzania, bali Afrika nzima na  ndiyo maana nasi tumekuja kujifunza. Tunawategemea sana katika mafunzo, tafiti na matibabu ya moyo kwa afya za watu wa Burkina Faso”, alisema Traore.

Mapema mwezi wa pili mwaka huu, Rais wa Burkina Faso, Kapteni Ibrahim Traore alituma timu ya wataalamu kwenda kujifunza katika taasisi hiyo na kuona  hatua walizopitia katika tiba ya moyo hadi kuwa moja ya Taasisi zinazoongoza Barani Afrika kutoa huduma za kibingwa bobezi ili nao waweze kujifunza na kuboresha huduma za matibabu ya moyo nchini humo.

Utiaji saini wa makubaliano hayo ni jitihada zilizofanywa na Ubalozi wa Tanzania nchini Burkina Faso, unaowakilisha nchi hiyo kutokea Abuja, Nigeria unaoongozwa na Balozi Selestine Kakele, ambao waliratibu mawasiliano ya JKCI na Burkina Faso hatimaye kufanikisha kusainiwa kwa hati ya makubaliano ya ushirikiano huo.

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Sanamu ya Bikira Maria yaonekana ndani ya Hifadhi ya Taifa Saadani

Wawekezaji wa Oman watua nchini, wateta na NHC kuchochea mapinduzi sekta ya makazi