Makamu wa Rais: Uhuru wa Mahakama ni dhamana ya haki, sio kinga ya uzembe
- Mahakama zageukia AI kuongeza ufanisi utoaji haki
Makamu wa Rais Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi amesema Serikali
imeendelea kuchukua hatua za makusudi katika kuimarisha uhuru wa Mahakama ili
kuiwezesha kutekeleza wajibu wake kikamilifu na kuchochea ustawi na maendeleo
ya Taifa ikitambua umuhimu wa Mahakama katika ujenzi wa Taifa.
Makamu wa Rais Balozi Dk. Emmanuel Nchimbi
Dk. Nchimbi pia ametoa rai kwa majaji na mahakimu akitaka uhuru wa Mahakama
usitumike kama sehemu ya kuficha uzembe, upendeleo au vitendo visivyo vya haki
na kwamba uhuru huo ni dhamana ya kutenda haki kwa uadilifu, uwazi na kwa
kuzingatia Katiba na Sheria za nchi.
Amesema hayo, alipomwakilisha Rais Dk. Samia Suluhu
Hassan katika Maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini, yaliyofanyika leo Februari
2,2026 Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania, Tambukareli, Jijini Dodoma.
“Serikali itaendelea kushirikiana na Mahakama katika
ujenzi wa miundombinu ya Mahakama, kuimarisha rasilimali watu, kuboresha
maslahi ya watumishi wa Mahakama na kusogeza huduma za utoaji haki karibu zaidi
na wananchi, hususan kupitia mpango wa ujenzi wa Mahakama za Mwanzo kwa kata
zote nchini zisizo na Mahakama za Mwanzo,”
amesema Dk.Nchimbi.
Amesema Mahakama ina wajibu muhimu wa kulinda utawala wa
sheria, kusimamia utekelezaji wa mikataba, kulinda rasilimali za Taifa na
kuhakikisha kuwa maendeleo yanayopatikana yanawanufaisha Watanzania wote kwa
usawa.
Kiongozi huyo amesema Mahakama ina mchango mkubwa katika
utekelezaji wa Dira ya Taifa ya 2050 kwa kuendelea kulinda haki na misingi ya
Katiba, kuhakikisha migogoro ya kiuchumi, kibiashara na kijamii inatatuliwa kwa
haraka na kwa haki, kujenga imani ya wananchi na wawekezaji katika mfumo wa
kisheria wa nchi, kukuza uwajibikaji na nidhamu katika utumishi wa umma na
sekta binafsi pamoja na kudumisha amani na mshikamano wa kitaifa, ambao amesema
ni msingi wa maendeleo endelevu.
“Ni muhimu
Mahakama, ikazuia migogoro inayoweza kuwa chanzo cha migawanyiko ya kijamii au
kisiasa na kuharakisha utekelezaji wa sera na mipango ya maendeleo kwa kutoa
tafsiri ya kisheria iliyo wazi na thabiti,” amsema Dk. Nchimbi na kuongeza;
“Mi muhimu kujenga na kuimarisha utamaduni wa kuheshimu
sheria, haki na taasisi za umma, pia kuchangia katika mapambano dhidi ya rushwa
na matumizi mabaya ya madaraka pamoja na kuwezesha wananchi kushiriki
kikamilifu katika maendeleo ya Taifa kwa kuwahakikishia ulinzi wa haki zao za
kisheria.”
Katika hatua nyingine, Makamu wa Rais amewaasa viongozi,
wanasiasa, wanaharakati na wananchi wote kuheshimu tume iliyoundwa na Rais ya
kuchunguza matukio ya uvunjifu wa amani baada ya Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29,
2025 kwa kuacha kuongelea masuala hayo nje ya mfumo wa kisheria.
Kwa upande wake, Jaji Mkuu wa Tanzania George Masaju
amesema Mahakama inaendeleza na kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika shughuli
zake ili kuimarisha ufanisi.
“Kwa sasa Mahakama inajenga mfumo unaotumia Akili Unde
(AI) kwa ajili ya kurekodi mwenendo wa kumbukumbu za mashauri na hukumu mahakama,”
amesema.
Amesema katika
mfumo huo, Jaji, Hakimu, Wakili na Shahidi wanapozungumza mahakamani mfumo huo
utatafsiri lugha iliyotumika na kuiandika kwa lugha iliyokuwa imechaguliwa
kuandika kwa wakati huo huo.
Jaji Mkuu Masaju amefafanua kwamba mfumo huo utakapoanza
kutumika utaimarisha ufanisi wa utendaji wa Mahakama kwani kuchukua kumbukumbu
za mwenendo wa mashauri Mahakamani kwa kuandika kwa mkono au kompyuta
kunachelewesha na wakati mwingine kupotosha.
Maoni
Chapisha Maoni