KARDINALI PENGO KUZIKWA PUGU FEBRUARI 28
Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhasham Yuda Thadei Ruwa'ichi, ametangaza kwamba mazishi ya Askofu Mkuu Mstaafu wa jimbo hilo, hayati Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, yatafanyika Jumamosi ya Februari 28, mwaka 2026 katika makaburi ya Kituo cha Hija Pugu.
Ikumbukwe kuwa, enzi za uhai wake, hayati Kardinali Pengo alisema kuwa kaburi lake lipo Pugu na atafurahi tamanio lake hilo likitimizwa.
Katika taarifa yake ya leo, Askofu Ruwa'ichi amesema siku ya Ijumaa Februari 27, saa 3 asbuhi, mwili wa hayati Kardinali Pengo utawasili viwanja vya Kanisa la Mtakatifu Joseph, Jimbo Kuu la Dar es Salaam, ambapo heshima za mwisho zitatolewa.
Ratiba hiyo inaonesha kuwa siku hiyo saa 10 jioni itafanyika misa maalum ya kumuombea marehemu.
Imeabinisha kwamba siku ya Jumamosi Februari 28 kianzia saa 1 kamili asubuhi hadi saa 3.45 heshima za mwisho zitatolewa kabla ya Ibada ya Mazishi kuanza saa 4 kamili asubuhi kwenye Kituo cha Hija Pugu.
Kwa mujibu wa Askofu Ruwai’chi, Kardinali Pengo ametwaliwa wakati akipatiwa matibabu katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), Dar es Salaam.
“Ninayo masikitiko makubwa kuwatangazieni kwamba, leo 19/02/2026, saa 04.00 usiku huu, mpendwa baba yetu Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu la Dar es Salaam, ameitwa nyumbani kwa Baba wa Milele, akiwa katika Taaisisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI), jijini Dar es Salaam,” amesema Askofu Ruwa’ichi katika taarifa yake jana usiku.

Maoni
Chapisha Maoni