Saa wakurugenzi mashirika ya umma zahesabika

 -Serikali yaja na mageuzi ya sheria

-Wana takriban siku 200 kubaki madarakani

-Mageuzi kugusa mamlaka ya Rais kuwateua

-Mashirika kusajili hisa, kuongeza wajibikaji

Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Siku za wakurugenzi wa mashirika ya umma na wakala za Serikali nchini zinahesabika, wakibakiwa na takriban siku 217 kabla ya kujua hatma yao, iwapo watasalia au kuondoka kwenye nafasi hizo.

Kuanzia Desemba 2025, siku hizo 217 sawa na wastani wa miezi saba, zikizidishwa kwa saa 24 za kila siku moja, zinakuwa jumla ya saa 5,208, muda unaolingana na kipindi kilichosalia kabla ya kuanza kutumika kwa mfumo mpya wa ajira.

Profesa Kitila Mkumbo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji

Hatua hiyoi inakuja baada ya Serikali kutangaza mpango wa kufanya mageuzi makubwa katika uongozi wa mashirika ya umma, unaotarajiwa kuanza rasmi Julai 1, 2026

Kwa mujibu wa Serikali, mabadiliko hayo yatakwenda na mabadiliko ya sheria ambapo Wakurugenzi wa mashirika watalazimika kuomba nafasi hizo na kusailiwa badala ya kuteuliwa na Rais kama ilivyo sasa.

Mageuzi hayo ya Serikali yanakusudia kuondoa utaratibu wa uteuzi wa moja kwa moja hasa ule unaofanywa na Rais, badala yake kuanzisha mfumo wa upatikanaji wa viongozi kwa njia ya ushindani wa wazi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Mipango na Uwekezaji, Profesa Kitila Mkumbo, amebainisha hayo  Desemba 8,2025 Dar es Salaam, akisema; “Mfumo huo mpya utaanza kutumika Julai 1, 2026, baada ya kupitishwa kwa sheria mpya inayoandaliwa na Serikali.”

Prof. Mkumbo amesema hatua hiyo ni sehemu ya mpango mpana wa Serikali wa kuboresha utendaji wa mashirika ya umma, kujenga uaminifu wa umma, na kuondoa malalamiko yaliyokuwapo kuhusu uteuzi wa viongozi bila mchakato shindani.

“Kama ni Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO utaomba, uta-apply, na utashindanishwa.

Kama unataka kuwa mjumbe wa bodi ya TPA au TISEZA utapitia mchakato wa ushindani. Watanzania wote wenye sifa wataomba, na uchaguzi utafanywa kwa competitive recruitment,” amesema.

Mijadala ya wanaharakati yaguswa

Kwa muda mrefu, baadhi ya wananchi, wasomi na wanaharakati wa demokrasia nchini wamekuwa wakipendekeza kupunguzwa kwa baadhi ya mamlaka ya Rais, ikiwemo katika uteuzi wa wakurugenzi wa mashirika na bodi za umma.

Hoja yao kuu imekuwa kwamba mamlaka makubwa ya uteuzi huondoa ushindani wa wazi, huzuia uwajibikaji, na kuacha mianya ya upendeleo wa kisiasa au undugu.

Mageuzi haya mapya yanayohamisha uteuzi kwenda kwenye mfumo wa ushindani wa kitaalamu, yanaonekana kugusa moja kwa moja kilio hicho cha muda mrefu, na kwa wengi, ikiwa ni hatua muhimu kuelekea kuimarisha misingi ya utawala bora na uongozi bora nchini.

Wachambuzi wa masuala ya utawala wanasema hatua hii inaweza kupunguza minong’ono kuhusu ‘uteuzi wa kiupendeleo,’ hususan katika nyadhifa za wakurugenzi, wajumbe wa bodi, na watendaji wa ngazi za juu katika mashirika ya serikali.

Mabadiliko mengine yajayo

Katika maelezo yake kwa waandishi wa habari jijini Dar es Salaam, Prof. Mkumbo amesema Serikali inaunda mfumo mpya wa upimaji utendaji wa mashirika ya umma, utakaozingatia tija ya kiuchumi, ubora wa huduma na mchango wao kwenye uchumi wa taifa.

Amesema sheria mpya itayalazimisha baadhi ya mashirika ya kibiashara ya Serikali kujisajili kwenye Soko la Hisa ili kutoa fursa kwa wananchi kumiliki hisa, kuongeza uwazi katika uendeshaji na kuongeza uwajibikaji kwa menejimenti na bodi.

 

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Sanamu ya Bikira Maria yaonekana ndani ya Hifadhi ya Taifa Saadani

Kapteni Traole afuata huduma za afya nchini

Wawekezaji wa Oman watua nchini, wateta na NHC kuchochea mapinduzi sekta ya makazi