Kesi ya Benki Yetu dhidi ya BoT, NMB leo tena
-Ni ya kudai warejeshewe benki yao
-Wadai mabilioni ya shilingi
Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com
Kesi ya madai namba 24650 ya mwaka 2025 inayowahusisha
wanahisa wa Benki ya Biashara ya Yetu, dhidi ya
Benki Kuu ya Tanzania, Benki ya NMB na Mwanasheria Mkuu wa Serikali
itaendelea kusikilizwa leo Makahama Kuu Masjala Ndogo ya Dar es Salaam.
Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania(BoT) Emmanuel Tutuba
Wanahisa wa Benki ya Biashara Yetu ni Taasisi ya Vijana ya
Yosefo, Cornelius Kasiya Kariwa na Altemius Ambros Milinga, ambao katika kesi
hiyo wanaongozwa na Wakili Ibrahim Bendera, aliyeieleza Mahakama kwamba wateja
wake ambao ni wanahisa zaidi ya 12,000 wanadai Benki Kuu imekiuka sheria kwa
kuichukua Benki ya Yetu na kuwapa Benki ya NMB, bila ya kuwalipa wanahisa hao
thamani ya hisa zao.
Wakili Bendera amesema katika kesi hiyo, wanahisa hao pia wanadai
warudishiwe benki hiyo pamoja na pesa zao zote ziizokuwa benki, kiasi cha
Sh6.18 bilioni.
Amesema Benki hiyo ilikuwa inahudumia Watanzania wa Bara na
visiwani zaidi ya 200,000 katika mikoa nane nchini.
Wanadai walipwe Sh 6.18 billioni pamoja na riba ya tangu
benki yao ilipochukuliwa; walipwe na Benki Kuu na NMB fidia kwa madhara ya
jumla Sh2 billioni, malipo ya Sh3 billioni kwa madhara waliopata wanahisa
namalipo mengine kama Mahakama itakavyoona inafaa
Mapema wiki iliyopita Wakili wa wadai katika kesi hiyo ya
madai aliiomba Mahakama Kuu Masjala ndogo ya Dar es Salaam, kusikiliza kesi
hiyo upande mmoja dhidi ya wadaiwa
wawili kati ya watatu.
Wakili Bendera alitoa ombi hilo baada ya wadaiwa kushindwa
kuwasilisha utetezi wao wa maandishi ndani ya muda unaotakiwa.
Mbele ya Jaji Mfawidhi Salma Maghimbi, Wakili Bendera
aliieleza mahakama kwamba wadaiwa wote watatu walipelekewa wito wa mahakamani
Oktoba 2, 2025, hivyo walikuwa na muda wa kutosha kuwasilisha utetezi wao,
lakini ni mdaiwa mmoja tu ambaye ni Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali
aliyewasilisha utetezi wake ndani ya muda.
Benki hiyo ilikuwa inahudumia Watanzania wa Bara na visiwani
zaidi ya 200,000 katika mikoa nane nchini.
Madhara maalum tzs 6.18 billioni pamoja na riba ya Toka
benki ichukuliwe;
Madhara ya jumla Tzs 2 billioni ilipwe na Banki Kuu na NMB
MALIPO ya 3 billioni
Kwa madhara waliopata wanahisa. Na MALIPO mengine kama Mahakama
itakavyoona inafaa
Mdaiwa wa kwanza ambaye ni Benki Kuu ya Tanzania, yeye
amewasilisha utetezi wake nje ya muda, wakati mdaiwa wa pili ambaye ni Benki ya
NMB yeye hakuwasilisha kabisa utetezi wake.
Mbele ya mahakama hiyo kwa niaba ya Benki Kuu, Wakili wa Serikali
Catherine Kiiza aliiomba Mahakama ikubali kupokea utetezi wa BoT ingawa umewasilishwa
nje ya muda uliotakiwa.
Hata hivyo, Wakili huyo hakuelezea hoja au sababu za msingi
za kuchelewa kwa utetezi wa BOT zaidi ya kumuomba Jaji aongeze muda.
Naye Wakili Mrano Mlekano
kwa niaba ya Benki ya NMB aliiomba Mahakama Kuu Masjala Ndogo ya Dar es
Salaam kuwaongezea siku moja, ili aweze kuwasilisha utetezi wake kwa madai
kwamba alishindwa kufanya hivyo kutokana na vurugu za Uchaguzi Mkuu wa Oktoba
29.
Alitaja sababu nyingine ni kuwepo kwa taarifa na nyaraka
muhimu ambazo zilikua na zuio la kuonekana na watu wengine, hadi kupata ruhusa
kutoka kwa Ofisa Fedha Mkuu wa NMB na Kitengo cha Uzingatiaji Kanuni (Compliance)
cha Benki kuu.
Hata hivyo, Wakili Bendera alipinga hoja hizo na kueleza kuwa
wadaiwa walikuwa na muda wa kutosha kuwasilisha utetezi wao na kumuomba Jaji
Maghimbi aanze kusikiliza upande mmoja ambao umewasilisha utetezi wake ndani ya
muda.
Kwa mujibu wa Sheria ya Mwenendo wa Kesi za Madai, mara
baada ya kupokea wito wa mahakama, mdaiwa anatakiwa kujibu utetezi wake ndani
ya siku 21.
Sheria hiyo pia inasema, iwapo muda huo utapita, basi mdaiwa
anaweza kuomba kuongezewa siku saba.
Maoni
Chapisha Maoni