Kasi ya mageuzi, matokeo chanya miradi ya NHC kwa Watanzania

 -NHC imeendelea kuutumia 2025 kuongeza kasi ya mageuzi

-Imeandika mafanikio lukuki, weledi waibeba

-Mkono wa Serikali waipa nguvu

-Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Katika ramani ya maendeleo ya Taifa, mwaka 2025 unajitokeza kama kipindi cha kipekee kwa Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) kwani ni mwaka ambao kasi yake ya mageuzi imeendelea kuthibitisha kuwa si tu mtekekelezaji wa miradi ya makazi, bali ni chachu na injini ya ukuaji wa miji, uchumi wa taifa na mhimili wa ajenda ya makazi bora kwa wote nchini.

Chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye ameendeleza mageuzi makubwa katika sekta ya ardhi, makazi na mipango miji, NHC limefufua miradi iliyokwama, limezindua mikakati mipya ya uwekezaji na limepanua kasi ya ujenzi maeneo yote ya Tanzania.

NHC iliuanza mwaka 2025 kama taasisi iliyo imara zaidi kifedha, kiutekelezaji na kiushindani, ikibeba dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita ya kutengeneza Taifa lenye miji ya kisasa, yenye heshima na inayotoa fursa kwa wananchi wote ikileta matokeo chanya.

Ushirikiano na Sekta Binafsi

Kupitia sera ya ubia iliyozinduliwa 2022, NHC limesaini mikataba mbalimbali 21 yenye thamani ya Sh 179 bilioni na kati ya miradi hiyo, 18 tayari imepewa vibali na utekelezaji unaendelea.

NHC pia linafanya upembuzi wa viwanja 80, ambavyo vitapangiwa uwekezaji mpya wa makazi na biashara.

Baadhi ya majengo yaliyokarabatiwa eneo la Kariakoo

Usimamizi wa miradi ya Serikali

NHC limeendelea kuwa mshauri elekezi na msimamizi wa miradi ya kimkakati ya Serikali na sekta ya umma ikitenda kwa weledi.

Baadhi ya miradi hiyo ni Soko Kuu la Kariakoo (asilimia 97), Ofisi za Wizara ya Fedha – Mtumba, Ofisi ya Makamu wa Rais – Muungano & Mazingira na Soko la Tanzanite – Mirerani.

Ujenzi wa majengo ya wizara nane katika Mji wa Serikali umeshakamilika kwa zaidi ya asilimia 90 huku pia NHC ikijenga Hospitali za Kanda – Mitengo na Musoma ambazo zimekamilika, lakini pia inajenga Jengo la TMDA Dodoma na majengo ya TFS 44 (miradi 17), Jengo la TCRA Dodoma.

Miradi hiyo inaonesha uwezo mkubwa wa wataalamu wa ndani wa NHC katika kusimamia majengo ya viwango vya kitaifa.

Kuboresha mifumo, uwazi na ufanisi

Katika mkutano wa Baraza la Wafanyakazi Februari 2025, viongozi wa ngazi mbalimbali wakiongozwa na Msajili wa Hazina, Nehemia Mchechu, Mwenyekiti wa Bodi – Dk. Sophia Kongela na Mkurugenzi Mkuu, Hamad Abdallah walisisitiza umuhimu wa kuongeza ufanisi, kuimarisha usimamizi wa rasilimali, kuepuka majungu kazini, kuongeza uwazi wa matumizi ya mali za umma, na kuzalisha matokeo yenye tija.

Baadhi ya Watendaji wa NHC wakifuatlia Mkutano mkuu wa Baraza la Wafanyakazi wa NHC mwanzoni mwa mwaka huu.

Dk. Kongela alieleza kuwa NHC linaendelea kuhakikisha uwekezaji unaongezeka, miradi inatekelezwa kwa viwango vya juu na shirika linaendelea kutoa gawio kwa Serikali, kiasi kinachotarajiwa kufikia Sh bilioni 6.5 mwaka huu.

Nguvu ya mageuzi

Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah, anasema wazi kwamba mageuzi yaliyofanyika ndani ya miaka mitano si ya kawaida.

Kwa mara ya kwanza tangu 2016, miradi mikubwa iliyokwama kama Morocco Square, Kawe 711 na Golden Premier Residence imefufuliwa na kuingia hatua za mwisho baada ya Serikali kuingilia kati na kuweka mazingira wezeshi ya ufadhili.

Matokeo ya mageuzi hayo yanaonekana kwenye hesabu ambapo kwa miaka mitano NHC imepata faida inayofikia Sh bilioni 235.4, huku faida kwa mwaka uliopita pekee ikifikia Sh bilioni 36.8

Katika kipindi hicho thamani ya mali za NHC hadi Juni 2024 imefikia Sh trilioni 5.5 huku kodi iliyolipwa kwa Serikali kwa miaka 5 ikiwa Sh bilioni 134.4.

Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah 

NHC katika miaka mitano imelipa gawio kwa Serikali la takriban Sh bilioni 9.85 huku gawio la mwaka 2024/25 pekee likiwa Sh bilioni 5.5 kiasi ambacho kimeandika rekodi mpya.

Hayo si mafanikio ya kawaida bali ni uthibitisho kwamba NHC sasa ni taasisi ya kimkakati, inayoweza kujiendesha kwa tija na kurudisha thamani kwa umma.

Ujenzi unaobadilisha taifa

Katika kipindi cha miaka mitano, NHC imejenga nyumba 5,399 zenye thamani ya Sh bilioni 659.5 na kati ya hizo 3,217 zimekamilika huku 2,182 zikiwa katika hatua mbalimbali za ujenzi.

Ni nyumba zinazoanzia Dar es Salaam hadi Tanga, kutoka Dodoma hadi Kagera – kila mahali NHC imeacha alama.

NHC ina miradi mikubwa ya kimkakati ambayo tayari imetekelezwa au inaendelea ambayo ni pamoja na Morocco Square – Dar es Salaam, Kawe 711 Housing Project – Dar es Salaam,Samia Housing Scheme – Kijichi & Kawe, Golden Premier Residence – Dar es Salaam, 2H Plaza – Morogoro na Mkwakwani Project – Tanga.

Mingine ni 2F Project – Singida, Soko la Madini la Tanzanite – Mirerani, Meru Shops – Arusha, Samia Iyumbu Apartments – Dodoma, Njendengwa Housing – Dodoma.

Zaidi ya hapo, Shirika la Nyumba la Taifa limetimiza mikataba 67 ya kazi za umma yenye thamani ya Sh bilioni 458.2, ikiwa ni pamoja na Jengo la Ofisi za Wizara Dodoma, Kitengo cha Moyo cha JKCI na Soko la Kimataifa la Tanzanite Mirerani.

NHC pia limeanzisha miradi ya ubia 21 na sekta binafsi yenye thamani ya Sh bilioni 351.

Tabora Commercial Complex

Katika mji wa kihistoria wa Tabora, NHC imeanzisha mradi wa Tabora Commercial Complex, jengo la kwanza la kisasa kuwahi kujengwa mkoani humo – thamani Sh bilioni 4, kukamilika Aprili 2026.

Ni mradi unaoonekana kama kuhuisha urithi wa Utemi wa Milambo–Tabora kuondoka katika unyonge na kujiweka kwenye ramani ya miji ya kisasa.

Zaidi ya maombi 200 ya nafasi za biashara, ofisi na makazi yamepokelewa kabla hata jengo kukamilika.

Ushirikiano na sekta binafsi

Katika ziara yake Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Deogratius Ndejembi, NHC iliwasilisha taarifa ya mwelekeo wa 2025, ikionyesha kuwa NHC inatekeleza miradi inayozingatia Dira ya Taifa, miradi inajaa ubunifu, thamani ya fedha na tija ya kijamii, ujenzi unaenda sambamba na mahitaji ya miji inayoendelea kukua.

Mkurugenzi wa Ujenzi wa NHC, Mhandisi Godwin Maro, alieleza kuwa NHC linafanya zaidi ya kujenga majengo, linaboresha maisha, uchumi, ajira na mazingira ya miji.

Dodoma

Mradi wa Samia Iyumbu Apartments unategemewa kutoa nyumba zaidi ya 300, zenye miundombinu ya Barabara,maji na umeme, shule na huduma za afya

Eneo la Njendengwa, NHC inaendelea kujenga nyumba zaidi ya 120 kwa watumishi wa umma na sekta binafsi.

Dar es Salaam

Mtanda Commercial Complex (iliyofikia zaidi ya asimilia 75 kukamilika, wenye thamani ya Sh bilioni 4.2

Samia Kijichi Housing Scheme

Nyumba zaidi ya 300 za gharama nafuu, zenye huduma muhimu na mazingira tulivu zinajengwa.

Samia Housing Scheme – Kawe

Nyumba 560 zilizokamilika na nyingine 560 zinazofuata.
Ni mradi wa thamani ya Sh bilioni 48 ukiwa sehemu ya mpango wa nyumba 5,000 wenye thamani ya Sh bilioni 466.


Miradi hiyo kwa inabadilisha sura ya jiji na kutoa makazi ya hadhi kwa maelfu ya watu.

Miradi ya upembuzi, ukarabati

NHC pia linafanyia ukarabati majengo ya zamani, kuziwekea mifumo mipya ya maji, umeme wa kisasa, barabara za ndani, mandhari na bustani mpya

Hatua hiyo inalinda thamani, kupandisha ubora wa miji na kuongeza mapato ya Serikali.

Tuzo na utambuzi

Utekelezaji wa kiwango bora na usimamizi wa fedha za Serikali umeiweka NHC katika ramani ya kutambuliwa kitaifa na kupata tuzo.

Katika kikao kazi cha viongozi wa mashirika ya umma kilichofunguliwa na Makamu wa Rais,(Sasa mstaafu), Dk. Philip Mpango Agosti 2025, NHC lilipata Tuzo ya Shirika Bora la Umma kwa mwaka wa fedha 2023/24.

Vigezo vilivyozingatiwa katika kupewa tuzo hiyo ni pamoja na uzalishaji wa mapato, ukwasi, faida, ubora wa taarifa za fedha, ufanisi wa huduma kwa jamii na utekelezaji wa hoja za CAG.

Ushirikiano na sekta ya fedha

Ziara ya kitaalamu ya Benki ya ABSA katika miradi ya Kijichi na Kawe ni  uthibitisho wa ubora wa kazi za NHC.

Katika ziara hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa ABSA, Obedi Laiser, amesema; “Tumeshuhudia kwa macho yetu ubora wa kazi ya NHC. Hii ni kazi inayochangia kupunguza uhaba wa makazi, kukuza ajira na kuinua hadhi ya miji yetu.”

Baadhi ya Wafanyakazi wa Benki ya ABSA wakiwa na watendaji wa NHC hivi karibuni
.

Kwa NHC, huu ulikuwa mhuri wa ubora kutoka kwa sekta ya fedha.

Kwa mwaka huu 2025, NHC imekuwa mshirika madhubuti wa maendeleo ya Taifa kutoka ujenzi wa nyumba, masoko ya madini, majengo ya biashara, hadi kubuni miradi ya ubia na kujenga miundombinu endelevu, ikiendelea kutekeleza majukumu yake kwa umakini na weledi.

Kwa kufanya hivyo, NHC imepanua ajira, imeongeza makusanyo ya kodi na gawio kwa Serikali, imechochea ukuaji uchumi wa wananchi, imebadilisha sura ya miji na imejenga heshima na matumaini mapya kwa Watanzania.

Kwa kasi ya utekelezaji, uwajibikaji na ubunifu unaoendelea, NHC linaibuka kama nguzo ya Taifa katika sekta ya makazi, likielekea kutimiza ndoto ya Tanzania yenye makazi bora, salama na yenye hadhi kwa wote.

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Sanamu ya Bikira Maria yaonekana ndani ya Hifadhi ya Taifa Saadani

Kapteni Traole afuata huduma za afya nchini

Wawekezaji wa Oman watua nchini, wateta na NHC kuchochea mapinduzi sekta ya makazi