ABSA, NHC waandika historia mpya ya makazi Tanzania
- Benki ya ABSA yatembelea miradi ya kisasa ya NHC Dar es Salaam
- NHC yajengea wataalam ABSA uelewa, kuwezesha umiliki
nyumba bora
- Ushirikiano sekta ya fedha, ujenzi matumaini mapya ya makazi endelevu
Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com
Ni asubuhi tulivu ya Ijumaa Oktoba 10, mwaka 2025. Magari kadhaa yenye nembo ya Shirika la Nyumba Tanzania (NHC) na Benki ya ABSA Tanzania, yakipenya barabara za Jiji la Dar es Salaam, kuelekea kwenye miradi miwili mikubwa ya makazi inayotekelezwa na NHC, ambayo ni Samia Housing Scheme eneo la Kijichi na Kawe 711 Housing Project.
Lengo la safari
hiyo limewekwa wazi kuwa ni kujifunza, kushirikiana, na kujenga daraja kati ya
sekta ya fedha ikiongozwa na ABSA kwa upande mmoja na NHC upande wa sekta ya
ujenzi.
Timu ya
wataalamu wa ABSA imefanya ziara hiyo ili kujionea kwa macho ubora wa kazi ya
NHC, kubaini fursa za biashara, lakini zaidi ya yote, kufahamu jinsi mikopo ya nyumba
inavyoweza kumsaidia Mtanzania wa kawaida kutimiza ndoto ya kumiliki makazi
yake ya kisasa.
Walipowasili Kawe, upepo wa baharini ulipuliza taratibu, ukipenyeza kwenye majengo mapya yaliyosimama kwa Fahari yakiwa na urefu wa kipekee eneo hilo, Kawe 711 Housing Project ilionekana kama sura mpya ya makazi ya kisasa kutokana na majengo yaliyosimama kwa mpangilio, yakionesha ubunifu na usanifu wa kisasa unaokidhi viwango vya kimataifa.
Msafara huo kisha
ukaelekea Kijichi, kwenye Samia Housing Scheme, mradi unaolenga Watanzania wa
kipato cha kati na cha chini eneo
lililojaa matumaini, nyumba bora zenye gharama nafuu na mazingira tulivu ya
familia.
“Tumeshuhudia
kwa macho yetu ubora wa kazi unaofanywa na NHC,” anasema kwa msisitizo
Mkurugenzi Mtendaji wa ABSA Tanzania, Obedi Laiser na kuongeza;
“Nyumba hizi ni za kisasa kabisa, zinadhihirisha ubunifu na weledi wa hali ya
juu. Hii ni kazi inayochangia kupunguza uhaba wa makazi, kukuza ajira na kuinua
hadhi ya miji yetu.”
Kauli yake inapokelewa kwa tabasamu na nyuso za furaha kutoka kwa wenyeji wao NHC. Kwa NHC ziara ya ABSA imekuwa ni ishara ya kuthamini kazi yao, ambayo hasa imejikita katika dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, kuhakikisha Watanzania wanapata makazi bora, salama na nafuu.
“Miradi hii ni sehemu ya utekelezaji wa dira ya Serikali kuhusu makazi endelevu,” ameeleza Mhandisi Grace Musita, Meneja wa Miradi wa NHC Kijichi.
Anafafanua;“Tunatumia teknolojia za kisasa zinazopunguza gharama na kulinda
mazingira. Tunataka kila Mtanzania awe na nyumba bora bila kuathiri uwezo wake
wa kifedha.”
Akizungumzia zaidi mradi wa Kijichi Msita anasema unatarajiwa kuwa na majengo Matano yenye nyumba 260 zitakazokuwa za chumba kimoja cha kulala, vyumba viwili, vyumba vitatu na maegesho ya magari takriban 300, ambapo pia litajengwa jengo litakalokuwa na maeneo ya maduka na huduma mbalimbali za kijamii.
Mhandisi Msita
anabainisha; “Ujenzi wa mradi huu tayari umeanza kutekelezwa Agosti 22, mwaka
huu 2025 na utakamilika Agost 22 mwaka 2027 takriban miaka miwili kufikia
ukamilifu wake, ambapo thamani yake ni shilingi bilioni 41.5.”
Anabainisha
kuwa bei kwa nyumba ya chumba kimoja ni shilingi milioni 112, vyumba viwili vya
kulala ni shilingi milioni 220 na vyumba vitatu vya kulala ni shilingi milioni
335 ikijumuishwa na VAT.
“Malipo yapo ya namna tattu, kuna malipo kwa fedha taslimu, kuna malipo kwa awamu kuanzia walau asilimia 10 ya bei, lakini pia mnunuzi anaweza kununua kwa mkopo wa benki, (Mortgages),” anasema Msita.
Kwa macho ya
ABSA, falsafa yao ya “Hadithi yako ina thamani” imepata maana halisi
wakati wa ziara hiyo. Kwa benki, kila nyumba iliyoonekana kwenye miradi ya NHC
imekuwa ni hadithi ya mafanikio, hadithi ya familia itakayopata amani, heshima,
na mwanzo mpya kwa kupata nyumba za NHC.
Katika
mazungumzo yaliyofuata, Mkurugenzi wa Mauzo na Masoko wa NHC, Deogratious
Batakanwa anasisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya pande hizo akisema:
“ABSA imekuwa mshirika wetu muhimu sana. Wametuwezesha kifedha kwenye ujenzi wa miradi hii na wamekuwa daraja kwa wateja wetu kupata mikopo ya nyumba. Huu ni mfano bora wa sekta binafsi na umma kushirikiana kwa manufaa ya Watanzania.”
Ziara hiyo
haikuwa tu tukio la kiserikali, bali pia ilikuwa ni sura hai ya matumaini
mapya.
Kwa upande wa uchumi, miradi ya NHC inaongeza ajira, biashara ndogo ndogo hata za kati, na thamani ya ardhi katika maeneo yanayozunguka miradi hiyo.
Kijamii, miradi ya NHC inatoa makazi salama na yenye heshima, ikibadilisha maisha ya wananchi kutoka kukaa nyumba za kupanga hadi kuwa wamiliki kamili.
Kupitia ushirikiano
kama huu, ndoto ya umiliki wa nyumba inakuwa halisi zaidi, hasa Benki kama ABSA
zinapotoa mikopo nafuu, na taasisi kama NHC zikijenga nyumba bora hivyo,
mafanikio yanakuwa ya pamoja.
Hatimaye msafara
wa ABSA uliondoka Kijichi ukiwa umebeba zaidi ya kumbukumbu. Umehitimisha ziara
hiyo ikibeba imani mpya katika uwezo wa sekta binafsi na umma kuleta mabadiliko
chanya.
NHC na ABSA Tanzania wameonyesha kuwa maendeleo jumuishi hayaji kwa maneno pekee, bali kwa vitendo, kwa kuweka msingi imara wa jamii yenye makazi bora, salama na ya kisasa kwa kila Mtanzania.
![]() |










Maoni
Chapisha Maoni