Samia Housing Scheme Kawe: Ndoto makazi bora ya kisasa imetimia

-Kutoka wazo, ramani hadi uhalisia
-Wamiliki wapigwa msasa, waanza kukabidhiwa nyumba zao

Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com
Barabara zimekamilika, mifereji ya maji safi na maji taka iko tayari, taa za barabarani na kamera za usalama zimeshawekwa, huku bustani na miti michache ikipamba mitaa na kuleta utulivu. 

Ukiwa maeneo hayo asubuhi utashuhudia jua linapochomoza, lakini jioni jua linapozama juu ya majengo hayo mapya, likiongeza mvuto wa rangi za nyumba hizo mpya zilivyopangiliwa kwa umaridadi, zisizochosha kutazama.

Eneo hilo pia lina vizuia moto, mifumo ya kisasa ya utiririshaji maji na barabara za ndani  zilizokamilika, mitandao ya umeme imetengenezwa, na maeneo ya kijamii yameundwa kwa ustadi, pamoja na bustani.

Mradi huo  wenye nyumba 560 unaunganisha maisha ya kisasa, faraja, na mshikamano wa kijamii, lakini pia kutoa mwonekano unaochochea hisia za kifahari. 

NHC sio tu limekamilisha mradi huo, bali pia siku limeanza kukabidhi kwa wamiliki wake nyumba hizo, ambao walisubiri miaka mitatu kwa hamu  kutimia  ndoto hiyo, iliyofanikishwa kwa jitihada za Shirila la Nyumba la Taifa , chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah, nyumba hizo zina thamani ya Sh, bilioni 48, ukiwa ni mpango mkubwa zaidi unaolenga kujenga nyumba 5,000 kote nchini, ambao ukikamilika utakuwa na thamani ya Sh bilioni 466.

Mkurugenzi Mkuu wa NHC Hamad Abdallah

Kila nyumba imejengwa kwa ubora wa hali ya juu, kwa kuzingatia mazingira ya kijamii, usalama wa familia, na uhakika wa kuwa na thamani ya muda mrefu. 

Bila shaka huu ni mfano wazi wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita, ya Rais Samia ikilenga kuhakikisha Watanzania wanapata makazi bora ya heshima, yenye thamani na ustawi, yakiwa yamejengwa maghorofa 10 yenye ghorofa kumi kila moja, yaliyosanifiwa na timu ya NHC ya wasanifu majengo yaliozingatia mtiririko wa hewa kutoka Bahari ya Hindi. 

Hii ndiyo taswira ya ustaarabu, faraja na mshikamano wa kijamii walionao wamiliki wa nyumba eneo la Kawe kwenye Mradi wa nyumba bora za makazi wa Samia Housing Scheme, mkoani Dar es Salaam, uliofanikishwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).

Mkutano wa kwanza wa wamiliki wa nyumba

Kutokana na kukamilika mradi huo wa Kawe, hivi karibuni wamiliki watapatiwa taarifa kuhusu miundombinu, sheria, ada za matengenezo, bima na usajili wa huduma.
Si hivyo tu bali sasa kimeanzishwa Chama cha Wamiliki wa Nyumba (Homeowners Association – HOA) kitakachoratibu usimamizi na maendeleo ya eneo hilo.
Wateja wa nyumba za NHC Samia Scheme, Kawe wakiwa kwenye mkutano na watendaji wa Shirika la Nyumba la Taifa, kuhusu ukaazi katika nyumba hizo.

Kabla ya makabidhiano rasmi, NHC imeandaa Mkutano wa Kwanza wa Wamiliki wa Nyumba utakaofanyika Jumamosi, 16 Agosti 2025, eneo la mradi. Mkutano huu unaashiria mwanzo wa maisha mapya ya pamoja.

Sherehe ya kukabidhi funguo za mfano, kukata utepe na picha za pamoja zitahitimisha hafla, huku alama rejeleo #SamiaHousingScheme ikitamba kwenye mitandao ya kijamii kusambaza furaha hii kwa taifa zima.

Kwa nini mradi umepewa jina la Rais Samia
Mradi huu umepewa jina la Rais Samia kuenzi mchango wake mkubwa katika mageuzi ya NHC, yaliyowezesha taasisi kupata mikopo, kukamilisha miradi iliyokwama kwa miaka nane, na kuongeza uwezo wake wa kifedha.
Wateja wa nyumba za Samia Housing Scheme-Kawe wakifuatilia mkutano wao na NHC

Mbali na Kawe, NHC linaendeleza miradi mingine mikubwa ikiwemo Soko la Madini Mirerani, 2H Plaza Morogoro, Tabora Commercial Complex, na Meru Shops Arusha

Miradi hii inaimarisha ajira, mapato na huduma kwa wananchi, ikiashiria kwamba uwekezaji wa makazi ni kichocheo cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Samia Housing Scheme inabaki kuwa zaidi ya mradi wa nyumba – ni hadithi ya matumaini, mabadiliko na ustawi wa taifa. Kila nyumba ni sehemu ya historia binafsi ya mmiliki, kila bustani ni alama ya familia, na kila awamu mpya ni ahadi ya mustakabali bora kwa vizazi vijavyo.mradi huu unawakilisha mafanikio ya mageuzi ya kiutendaji na kiushirikiano yaliyofanikisha makazi bora kwa Watanzania.

Mradi huu ni sehemu ya mpango wa uboreshaji wa miji, unaotekelezwa kwa njia kadhaa: kuvunja majengo ya zamani na kuyajenga upya, kuendeleza vitovu vya miji (satellite city), kuimarisha maendeleo ya miliki, na kuendeleza miradi ya ubia pamoja na nyumba za gharama kubwa. Ni mradi unaochangia si tu kwa makazi, bali pia kwa maendeleo ya miundombinu na mpangilio wa miji unaolenga kuongeza thamani ya maisha ya wakazi.

Mpango wa NHC unafanya faida inayopatikana kutokana na nyumba za gharama kubwa inarejeshwa kwa jamii, kwa kujenga nyumba za bei nafuu ambazo Watanzania wa kipato cha chini wanaweza kumudu. Hii ni ishara dhahiri ya dhamira ya Shirika ya kuunganisha ufanisi wa kifedha na ustawi wa jamii.

Mradi wa Samia Housing Scheme- Kawe unawakilisha mafanikio ya mageuzi ya kiutendaji na kiushirikiano yaliyofanikisha makazi bora kwa Watanzania.

Mbali na mradi huo, NHC pia inaeleza kuwa miradi mbalimbali inabuniwa na kujengwa katika miji na majiji, huku asilimia 75 ya biashara ya nyumba ikihusisha Dar es Salaam ikihusiana na mikoa mitano ya Shirika. Faida ya Shirika imeongezeka kutoka Sh. bilioni 198 miaka mitano iliyopita hadi Sh. bilioni 235 mwaka huu, jambo linalothibitisha ukuaji endelevu wa mpango wa makazi na ufanisi wa miradi.

Hadi sasa, nyumba 5,399 ziko kwenye mpango wa kuuza na kupangisha kwa gharama ya jumla ya Sh. bilioni 659.48, kati ya hizo nyumba 3,217 zimekamilika, na nyumba 2,182 ziko katika hatua mbalimbali za ujenzi ambazo zinatarajiwa kukamilika ifikapo Juni 2026. Hii inaonesha wazi kuwa mradi huu sio wa kawaida; bali ni matokeo ya sera bora, mageuzi makuu, na dhamira thabiti ya Shirika ya kuleta makazi bora kwa Watanzania wote.

Kwa msingi huu, mradi umepewa jina la heshima ili kuwakilisha dhahiri mageuzi, usimamizi bora, na mchango wa Shirika katika kuhakikisha kila Mtanzania ana makazi salama, ya kisasa, na yenye thamani ya muda mrefu.

Miradi minginne ya NHC

NHC siyo tu limejenga majengo ya kisasa, bali limeibua matumaini mapya kwa maelfu ya Watanzania, huku likichochea uchumi, kuzalisha ajira, na kuboresha taswira ya miji na mikoa mbalimbali, jambo ambalo ni ishara wazi ya jinsi taasisi za umma zinavyoweza kuleta mabadiliko chanya katika maisha ya watanzania.

Miradi ya NHC imeenea katika miji mikubwa na mikoa ya pembezoni, ikilenga kutoa makazi salama, ya kisasa, na yenye thamani. 

NHC pia linaendeleza miradi ya kibiashara na ukarabati wa majengo ya zamani, ikionyesha ushirikiano wa miradi ya makazi na biashara. Mradi wa Soko la Madini Mirerani, 2H Plaza Morogoro, Tabora Commercial Complex, na Meru Shops Arusha unaimarisha ajira, mapato na huduma kwa wananchi. 

Hali hii inathibitisha kuwa uwekezaji katika makazi hauishii kwenye nyumba pekee, bali unachochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa ujumla

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Sanamu ya Bikira Maria yaonekana ndani ya Hifadhi ya Taifa Saadani

Kapteni Traole afuata huduma za afya nchini

Wawekezaji wa Oman watua nchini, wateta na NHC kuchochea mapinduzi sekta ya makazi