Dk. Yonazi awaasa watumishi Ofisi ya Waziri Mkuu kutekeleza majukumu yao
Mwandishi Weu,daimatznews@gmail.com
Katibu Mkuu Ofisi ya Waziri Mkuu Sera, Bunge na Uratibu Dk. Jim Yonazi amewaasa Watumishi wa Ofisi ya Waziri Mkuu kuendelea kufanya kazi kwa bidii na weledi mkubwa katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.
Dk. Jim Yonazi
Ameyasema hayo leo Julai 29, 2025 wakati akifungua Mkutano na Watumishi wa ofisi hiyo, ambapo alisema ni muhimu kuwa na nidhamu ya kazi, kushirikiana na kuendelea kuwa wabunifu katika majukumu ya kila siku na kuwakumbusha watumishi kuwa kazi wanazofanya zinagusa maisha ya mamilioni ya wananchi, hivyo ni wajibu wao kuhakikisha anatoa huduma bora na kwa viwango vya juu.
“Pia, nawasihi kuendelea kujenga mshikamano miongoni mwenu. Tunaposhirikiana, tunajenga nguvu ya pamoja ambayo hakuna changamoto inayoweza kutuzuia. Nawaomba tuendelee kufanya kazi kwa bidii na kwa moyo mmoja. Kumbukeni kuwa, kila mchango wenu una thamani kubwa katika kufanikisha malengo ya Ofisi yetu na Taifa kwa ujumla,” amesema Dk. Yonazi.
Katibu Mkuu Yonazi alieleza kuwa katika kuboresha ofisi hiyo kwa Mwaka wa Fedha 2025/2026, ofisi yake imeendelea kuboresha mazingira ya kazi kwa kushughulikia changamoto zinazohusu mazingira ya kazi na maslahi ya wafanyakazi, ikiwa ni pamoja na kukuza ubunifu katika utendaji kazi wa kila siku na kuimarisha mifumo bora zaidi ya kufuatilia maendeleo ya kazi na kuhakikisha kila mfanyakazi anawajibika ipasavyo kwa nafasi yake.
Katika mkutano huo watumishi wataweza kupata elimu kutoka kwa wataalam wa Mfuko wa Uwekezaji wa UTT kuhusu umuhimu wa kuwekeza.
Pamoja na mambo mengine pia watapewa elimu itakayowakumbusha masuala mbalimbali yanayohusu uzingatiaji wa maadili ya utumishi wa umma, masuala ya Afya hususan homa ya ini na magonjwa yasiyoambukizwa.
Maoni
Chapisha Maoni