Tanzania,EU zakubaliana kuunga mkono maendeleo
Na Hussein
Ndubikile, daimatznews@gmail.com
Serikali ya Tanzania na Umoja wa Ulaya (EU) zimesaini Tamko la
Makubaliano ya Kuendelea Kuunga Mkono Jitihada za Maendeleo kwa faida za pande
zote mbili.
Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Cosato Chumi
Akizungumza kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mahmoud Thabit Kombo, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Cosato Chumi baada ya kusainiwa kwa tamko hilo Desemba 10, 2024 jijini Dar es Salaam amesema ushirikiano huo ni wa muhimu kwa pande zote.
“Majadiliano haya ya leo ni sehemu ya utekelezaji wa Mkataba wa Samoa,
uliosainiwa mwaka 2023, ambao unaelekeza umuhimu wa kuwa na majadiliano ya mara
kwa mara kati ya Umoja wa Ulaya na Nchi za Afrika, Karibiani, na Pasifiki
(ACP). “ amesema.
Amesema kuwa Tanzania ni moja ya nchi wanachama wa kundi la ACP, ambayo
inaendelea kutekeleza wajibu wake kwa kushiriki kikamilifu kwenye majadiliano
hayo muhimu kila mwaka kwa lengo la kuimarisha ushirikiano wa kimkakati na
Umoja wa Ulaya.
Chumi amebainisha kuwa majadiliano hayo yalijielekeza zaidi katika masuala
yanayogusa maslahi ya pande zote, ikiwa ni pamoja na utawala bora, demokrasia,
usalama wa baharini, biashara na uwekezaji, na ulinzi na usalama kikanda na
kimataifa.
Chumi ameyataja baadhi ya maazimio yaliyofikiwa kwenye mkutano huo ambapo
alisema kuwa Tanzania na Umoja wa Ulaya zimedhamiria kuimarisha zaidi
ushirikiano wa pande mbili chini ya Mkataba wa Samoa.
Ushirikiano huo unaendana
na Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2020- 2025 na Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya
Miaka Mitano ambapo pande zote mbili zimekubaliana kuongeza ushirikiano ili
kuhakikisha matokeo chanya na yenye manufaa kwa wananchi.Baadhi ya wajumbe wa Umoja wa Ulaya (EU) wakifuatilia hafla ya utiaji saini makubaliano baina ya umoja huo na Tanzania.
Aidha Chumi kwa niaba ya Tanzania aliushukuru Umoja wa Ulaya kwa msaada wake endelevu kupitia mfumo wa mpango wake
wa maendeleo wa majirani na ushirikiano wa kimataifa ambao umeweka Euro 726
Milioni kwa Tanzania.
Amefafanua kuwa fedha hizo zimewezesha kutekeleza miradi muhimu katika sekta ya
nishati, uchumi wa buluu, mabadiliko ya tabia nchi na mpango wa miji kuwa ya
kijani.
Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa Umoja wa Ulaya anayeshughulikia Kanda
ya Afrika katika Kurugenzi ya Huduma za Nje ya Umoja wa Ulaya (Europeana
External Action Service), Balozi Ritha Maria Laranjinha amehimiza kudumishwa kwa ushirikiano huo kwa ajili ya maslahi mapana ya wananchi.
Maoni
Chapisha Maoni