Namba saba inavyoing’arisha WFC
-Makusanyo yapaa zaidi ya sh. bilioni 700
-Inatoa mafao saba, ina faida 7
-Imelipa fidia miaka 7, imetaja mafanikio saba
Exuperius Kachenje,
daimatz@gmail.com
Ingelikuwa tunazungumzia namba ya bahati, basi tungeweza kuielezea namba saba kuwa ndiyo ya bahati kwa Mfuko wa Fidia kwa Wafanyakazi nchini (WCF), unaoakisi kukusanya mapato ya zaidi ya shilingi bilioni 700.
Makusanyo hayo ya mapato ni hadi Septemba mwaka huu, yakikua kutoka Sh. bilioni 146 miaka saba iliyopita, mwaka 2017.
Hayo yamebainika wakati Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dk.John Mduma
akiwasilisha taarifa ya mfuko huo mbele ya wahariri na waandishi wa habari wa
vyombo mbalimbali nchini Novemba 2,2023 jijini Dar es Salaam, ambapo pamoja na
mambo mengine alieleza kuhusu makusanyo ya michango na fidia zilizolipwa na
mfuko huo kwa wafanyakazi kwa miaka saba iliyopita.
![]() |
Mkurugenzi Mkuu wa WCF, Dk.John Mduma akiwasilisha maelezo kuhusu mfuko huo, mbele ya Wahariri wa Waandishi wa Habari wa vyombo mbalimbali vya habari nchini Novemba 2,2023 jijini Dar es Salaam. |
Katika taarifa hiyo, Mduma amebainisha mapato yaliyokusanywa
na WCF kwenye miaka saba ya utekelezaji wa shughuli za mfuko huo akieleza: “
Hadi Septemba mwaka 2023 tumekusanya shilingi bilioni 758.78, mwaka 2022
kipindi kama hicho tulikusanya sh. bilioni 671.87, 2021 tulikusanya sh. bilioni
585.22 na 2020 sh. bilioni 478.29.”
Mkurugenzi Mkuu huyo wa WCF akaitaja miaka mingine mitatu kati
ya saba na makusanyo yake kuwa ni mwaka 2019 ambapo zilikusanywa sh.bilioni 371.84,
mwaka 2018 sh. bilioni 262.88 na mwaka 2017 ambao WCF ilikusanya sh. bilioni 146.11.
Katika mkutano huo ulioratibiwa na Ofisi ya Msajili wa
Hazina, WCF ilibainisha pia imelipa mafao kwa wafanyakazi kwa kipinzi cha miaka
saba, ambayo pia yamekuwa yakiongezeka mwaka hadi mwaka kati ya mwaka 2017 hadi
mwaka huu 2023.
“Kwa upande wa fidia kwa wafanyakazi, kwa mwaka 2017 WCF
ililipa fidia ya shilingi bilioni 1.55, mwaka 2018 sh. bilioni 4.40, mwaka 2019
tulilipa sh.bilioni 9.09 na mwaka 2020 tulilipa fidia inayofikia sh.bilioni
18.18. Lakini mwaka 2021 sh.bilioni 31.38 zililipwa, mwaka 2022 fidia zililipwa
sh.bilioni 44.30 na sh.bilioni 62.22 zililipwa kwa mwaka 2023 hadi kufikia
Septemba,” alisema Mduma.
Katika wasilisho la Mkurugenzi huyo wa WCF, namba saba
iliakisi tena wakati akieleza idadi na aina ya mafao yanayotolewa kwa
wafanyakazi wanapoumia kazini na kupoteza uwezo wa kufanya kazi, au uwezo wao
kupungua ambapo Mduma amesema kuna aina saba za mafao yanayotolewa na mfuko
huo.
Mduma aliainisha mafao hayo saba kuwa ni; Fao la Matibabu, Fao la Ulemavu wa Muda, Fao
la Ulemavu wa Kudumu na Fao la Kumuuguza
Mgonjwa. Mengine ni Malipo Kwa
Wategemezi , Msaada wa Mazishi na Fao la Utengemao.
Akizungumzia usajili wa waajiri, Mkurugenzi Mkuu Mduma,
amesema hadi kufikia Septemba30 mwaka 2023 jumla ya waajiri waliosajiliwa ni
31,469 sawa na asilimia 93.33 ya waajiri 33,680 walio katika kanzidata ya WCF.
“Katika mwaka wa fedha 2022/2023, waajiri waliosajiliwa
walikuwa 30,866 sawa na asilimia 91.64, mwaka 2021/2022 walisajiliwa 27,786 ambao
ni asilimia 82.50, mwaka 2020/2021 walikuwa 25,085 na mwaka 2019/2020 ni waajiri
22,802,” amesema Mduma na kuendelea:
“Mwaka 2018/2019 walisajiliwa waajiri 20,102 sawa na silimia
59.69, mwaka 2017/2018 waajiri 14,836 ambao ni asilimia 44.05, mwaka 2016/2017 kulikuwa na asilimia 23.33 ya waajiri ambao ni 7,857 na mwaka 2015/2016 walisajiliwa
waajiri 5,178 sawa na asilimia 15.37.”
Akizungumzia mafanikio ya WCF, namba saba pia imehusika
baada ya Mduma kunainisha mafanikio saba ambayo WCF imepata na kuyaainisha kuwa
ni pamoja na kukipata Hati Safi kila mwaka tangu kuanzishwa kwake mwaka 2015, kuongezeka
kwa malipo ya fidia kwa wafanyakazi (mpaka 30/09/2023, TZS bilioni 65.35) na uhai
na uendelevu wa kulipa fidia bila kutetereka kwa mujibu wa Tathmini ya Uhai na Uendelevu
wa Mfuko ya Mwaka 2022.
Kwa mujibu wa Mduma,
mafanikio mengine ya WCF ni kuimarika uwezo wa kifedha wa Mfuko kufikia shilingi bilioni 697.83 kwa mujibu wa
hesabu za hadi tarehe 30 Septemba 2023, kuboreshwa kwa huduma kupitia usimikaji
mifumo ya TEHAMA, kuboreshwa kwa kituo cha huduma kwa wateja (Call Centre) na
kuboreshwa kwa tathmini za ulemavu kupitia mafunzo kwa madaktari.
Mkurugenzi huyo wa WCF ametaja mafaniko mengine kuwa ni kuongezeka
kwa wigo wa utoaji huduma kwa kuingia
makubaliano na hospitali, watoa huduma mbalimbali za afya nchini na ufunguzi wa
ofisi mikoani pamoja na WCF kuwa kinara hata kuzifanya nchi za Zambia, Kenya,
Botswana, Afrika Kusini na Zimbabwe kujifunza kutoka mfuko huo.
Katika mkutano huo wa kawaida wa kampuni, mashirika na
taasisi zilizo chini ya Msajili wa Hazina,WCF pia imeeleza mambo iliyofanya kuboresha
mchango wake katika kuimarisha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini
Serikali ya awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, ambayo
ni pamoja na kupunguza kwa kiwango cha uchangiaji kwa waajiri wa sekta binafsi
kutoka asilimia moja ya awali hadi asilimia sifuri nukta tano.
![]() |
Baadhi ya Wahariri na Waandishi wa Habari, wakifuatilia mkutano wao na Mkurugenzi Mkuu wa WCF(hayupo pichani) uliofanyika jijini Dar es Salaam, Novemba 2, 2023 |
Mengine ni kupunguzwa kwa riba kwa waajiri waliochelewesha
michango kutoka asilimia 10 iliyokuwa ikitozwa kwa mwezi hadi asilimia mbili, kufitiwa
riba ya malimbikizo ya michango kwa waajiri waliochelewa kulipa na kuongezwa
kwa kima cha chini cha fidia kutoka utaratibu wa awali ambao haukuwa na kima
cha chini cha fidia kwa mfanyakazi ambaye hakupata ulemavu wa asilimia 100 hadi
kufikia sh. 275,702.83.
Kuhusu mwelekeo wa WCF ,
Mduma ametaja hatua mbalimbali yanayokusudiwa ili kutoa huduma bora
zaidi ambayo ni pamoja na kupanua wigo wa huduma za utengemao kwa kulipia
huduma za mafunzo ya ujuzi mbadala, kulipia huduma za utengemao wa uwezeshaji
wa kijamii na kuimarisha huduma za uhakiki wa bili za matibabu kupitia ujenzi
wa mifumo stahiki ya TEHAMA.
Mduma amesema, mengine ni kuimarisha ushirikiano wa
kimkakati na taasisi mbalimbali za Serikali zikiwamo Jeshi la Polisi, TRA,
BRELA na mifuko mingine ya Hifadhi ya Jamii katika kutatua changamoto za
kupokea taarifa zisizo sahihi za madai na michango, kujenga jengo la Fidia House
Dodoma ili kuimarisha juhudi za kuboresha makao makuu ya nchi na kuimarisha
upatikanaji wa huduma za WCF katika mikoa mbalimbali nchini, ikiwemo kupitia
ufunguzi na uboreshaji wa ofisi za mfuko huo mikoani.
Mduma alieleza kuwa mfuko huo ulioundwa kwa mujibu wa sheria
mwaka 2015, dira yake ni kuwa mfano wa kuigwa katika utoaji wa huduma za fidia
kwa wafanyakazi barani Afrika, ukibeba dhima ya kutoa huduma za fidia za kuaminika
na fanisi kwa wafanyakazi zitakazowawezesha kukabiliana na athari za kijamii na
kiuchumi zitokanazo na ajali mahali pa kazi kwa kuzingatia tunu za uadilifu, ushirikiano,
uwajibikaji, ubora na kujali.
Maoni
Chapisha Maoni