Hot Posts

6/recent/ticker-posts

Mkurugenzi Mkuu NHC alivyocheza nambari nane, tisa mikoani

 -Ni miezi minane tangu kuteuliwa
-Atembelea mikoa tisa ya NHC

Mwandishi Wetu, Bukoba

Kwa wafuatiliaji wa mchezo wa mpira wa miguu yaani soka, anaelewa umuhimu wa namba nane na tisa kwenye mchezo huo, kwani anayecheza namba nane ndiye kiungo anayesukuma mpira kwa washambuliaji, huku namba tisa akisukuma mashambulizi na kufunga magoli.

Hata hivyo, ingawa nafasi hizo za namba nane na tisa huchezwa na watu tofauti, lakini Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba Tanzania (NHC), Hamad Abdallah ameweza kucheza nafasi hizo mbili peke yake katika kuhakikisha anatimiza majukumu yake ya kuliongoza shirika hilo la taifa.

Mkurugenzi huyo amecheza nambari nane kwani Oktoba hii ametimiza miezi minane tangu alipoteuliwa na Rais Samia kuiongoza NHC  Februari 23, mwaka huu akichukua nafasi ya Nehemia Mchechu, ambaye ameteuliwa kuwa Msajili wa Hazina.

Si hivyo tu, bali Hamad pia amehitimisha ziara ya mikoani ambapo ametoa maagizo na maelekezo nane yenye lengo la kulisukuma mbele shirika hilo kiutendaji na kujiongezea kipato katika kuchangia maendeleo ya taifa.

Hamad pia amecheza namba tisa kwa kuwa amefanya ziara katika mikoa tisa ya NHC, aliyoikamilisha katika Mkoa wa Kagera mwishoni wa wiki iliyopita, hivyo kuitia chachu mpya katika utendaji mikoa hiyo na kuipa ushindi NHC katika kutekeleza majukumu yake kwa taifa kuhakikisha Watanzania wanakuwa na makazi bora.

 Mkurugenzi huyo amekamilisha ziara yake katika mikoa ya Shirika, huku akiacha tabasamu, matumaini na ari mpya kwa wafanyakazi  katika mikoa hiyo.

Ziara hiyo ilimuwezesha Hamad kukutana ana kwa ana na wafanyakazi katika mikoa hiyo pamoja na kukagua miradi na rasilimali mbalimbali za NHC.

 Ameihitimisha ziara yake mjini Bukoba, ambapo pamoja na kutembelea miradi iliyopo Chato mkoani Geita, nyumba za shirika Mjini Bukoba na jengo la kibiashara lilipo mpaka wa Tanzania na Uganda eneo la Mutukula, Mkurugenzi Mkuu Hamad ameonyesha kufurahishwa na ari na ubunifu wa hali ya juu, uliofanywa na Mkoa wa Kagera kuongeza mapato ya mkoa huo.

Meneja wa NHC Mkoa wa Kagera, Deogratius Batakanwa (aliyesimam), akitoa taarifa ya utendaji wa Mkoa wake kwa Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah aliyekuwepo mkoani humo kukagua nyumba na miradi ya NHC na kuhimiza utendaji wa kazi. (Picha kwa hisani ya NHC)

 

Akihitimisha ziara hiyo kwa kuzungumza na wafanyakazi wa Mkoa huo, Mkurugenzi Mkuu alirejea kusisitiza mambo makuu nane ili kuiletea NHC tija kubwa.

Mambo hayo ni pamoja na wafanyakazi wote kufanya kazi kwa upendo, mshikamano kama familia moja ili shirika liweze kufikia malengo yake na kupata faida kubwa. 

"Tuishi kwenye miiko ya shirika inayosisitiza uadilifu na ushirikiano. Tuishi kama familia moja, ukiona mwenzio anakosea, mwambie tu kwa nia njema, hakuna mtu ambaye ni malaika, vumilianeni," amesisistiza Mkurugenzi Mkuu.

Ameongeza: “Wafanyakazi wote wanapaswa kuwa na upendo, kutakiana mema na kuhakikisha  hakuna majungu, lakini pia muwe wepesi wa kusameheana kwa kuwa hakuna anayejua kesho yake. 

Muwe  ‘positive’(Mawazo mema) wakati wote na kumtegemea Mungu kwa kila jambo, mjue kuwa kazi mbaya ukiwa nayo, lakini ikikuponyoka utaitafuta na hutaipata kirahisi, tunzeni kazi zenu."

Amesisitiza kuwa kazi ni kipimo cha utu na kwamba kila mtu akijibidisha vizuri NHC itapata tija na kubadilisha maisha ya kila mfanyakazi.

Mkurugenzi Mkuu amerejea kuhimiza wafanyakazi wote kushirikiana katika kukusanya kodi na malimbikizo yaliyopo, pia kubuni mambo yatakayoliongezea shirika  mapato.

 "Ukusanyaji wa kodi ya nyumba za NHC ni kipaumbele kikubwa kwa kuwa hiki ni chanzo muhimu cha mapato ya shirika,"amesema.

Kwa mujibu wa Hamad, mikoa ya NHC inapaswa kuwa na mikakati ya kukusanya kodi, ikiwemo kuhakikisha kila mpangaji ana amana ya pango, pamoja na kuhakikisha wapangaji wasiolipa kodi kwa wakati hawapewi mikataba mipya.

"Kusanyeni kodi kwa ushirikiano na  hakikisheni mnakusanya malimbikizo yote. Kila mpangaji awe na amana ya pango ifikapo Desemba 2023,” amesema.

Hamadi amerejea kauli yake kwamba  ili kufikia malengo ya shirika, kila mfanyakazi wa NHC atimize wajibu wake kwa mujibu wa ajira yake, akaagiza Mameneja, Wakuu wa Idara na Kurugenzi kuhakikisha kuwa upimaji wa utendaji kazi unafanyika kwa haki, kikamilifu na kuangalia majukumu ya kila mfanyakazi, ili kila mmoja ijulikane tija anayoliingizia shirika.

 "Pimeni utendaji kazi wa kila mfanyakazi kwa haki bila kuonea mtu ili kila anayestahili apewe  motisha inayomstahili, iwe hasi au chanya," Hamad ameasa.

 Kuhusu motisha kwa watumishi, Hamad amebainisha kuwa Menejimenti ya NHC imeanza kufuatilia uboreshaji  motisha kwa wafanyakazi,  ikiwemo malipo ya mshahara wa mwezi mmoja kwa kila likizo na kwamba nia ya menejimenti ni kuona kila mfanyakazi anafurahia kuwa sehemu ya familia ya NHC.

 "Wafanyakazi wanadanganya maeneo walikozaliwa ili wapate nauli kubwa ya kwenda likizo. Hili tunaenda kulimaliza kwa kulipa kila anayekwenda likizo mshahara wake wa mwezi mmoja; 

Mazungumzo na Msajili wa Hazina yanakamilishwa ili tuanze kutekeleza motisha ya likizo kwa wafanyakazi. Mimi ni mtu wa haki, nikiahidi jambo natekeleza, mkichapa kazi kwa bidii, tukapata tija, tutaongezana mishahara katika mwaka huu wa fedha," Hamad aliahidi.

Akizungumzia miradi ya ubia iliyosimama kwa muda mrefu bila kukamilika, Hamad amesema kuwa NHC imeanza kuchukua hatua za kurejesha miradi hiyo chini ya shirika ili ikamilishwe.

“Tayari tuna miradi miwili tumeshairudisha mikononi mwa NHC, iliyopo jijini Arusha na hata Mwanza tumenza kufanya mazungumzo na wabia, yenye lengo la kuwanyang'anya miradi minne ambayo haijaendelezwa kwa muda mrefu."

 Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah(Mwenye shati la mikono mirefu), akiingia katika moja ya majengo ya NHC mkoani Kagera alipofanya ziara kukagua nyumba na miradi ya NHC na kuhimiza utendaji wa kazi. (Picha na NHC)


 Akizungumzia  huduma bora kwa wateja, Mkurugenzi Mkuu huyo amewataka mameneja wa mikoa kuwa na utaratibu wa kukutana na wateja wa NHC ili kutatua changamoto zinazowakabili.

"Tumieni lugha nzuri kwa wateja wetu, andikeni barua za wateja  bila kuonyesha hasira wala jazba, maana maandishi yanadumu muda mrefu. 

Shirikianeni katika kuwahudumia wateja na muisemee NHC na Serikali vyema. Shirika lina sifa nzuri ni vyema tukailinda sifa hiyo."anasema Hamad.

Kuhusu ajira mpya ndani ya NHC, Mkurugenzi Mku, Hamad amerejea kueleza kuwa, ajira hizo zitatekelezwa hivi karibuni, lakini kwa kufuata ikama na mahitaji ya watumishi yaliyopo, kipaumbele kikiwa kwa wafanyakazi wa mikataba wanaolitumikia shirika hivi sasa kwa uaminifu na uzalendo mkubwa.

Hamad amewataka wafanyakazi hao kuendelea kuchapa kazi kwa weledi na uaminifu ili ajira hizo zikitoka wawe na sifa za kuajiriwa.

Akizungumzia uuzaji wa nyumba za  gharama nafuu zilizopo chini ya NHC, Hamad ameitaka mikoa yenye nyumba hizo ukiwemo Mkoa wa Kagera, eneo la Chato na Muleba kuanza kutafuta wanunuzi wa nyumba hizo ili kuliondolea shirika mzigo mkubwa wa kuzitunza nyumba hizo, ambazo nyingi zimeanza kuchakaa.

"Tulijenga nyumba hizi ili tuziuze, naona zimechakaa sana na zitatugharimu kila mara, menejimenti ya NHC inapitia bei ya kuuzia nyumba hizi na itatolewa hivi karibuni ili muanze kuziuza,” amesema Hamad.

Akizungumzia uadilifu na uaminifu katika kusimamia miradi na mali za shirika, Mkurugenzi Mkuu wa NHC amesema jambo hilo ni kipaumbele cha kila mfanyakazi wa NHC, akawataka kuhakikisha kuwa usimamizi wa miradi na rasilimali za NHC vikiwemo vifaa vya ujenzi katika miradi vinalindwa na kila mfanyakazi ili shirika lipate faida iliyokusudiwa.

"Kila mfanyakazi ana wajibu wa kuhoji mwenendo wa usimamizi wa miradi, utunzanji wa mali za NHC na kuelezana ukweli pale tunapoona kuna ufujaji wa mali za shirika," amesema  Mkurugenzi Mkuu na kusisitiza: “Hili siyo suala la Makao Makuu pekee, bali kila mmoja awe mlinzi wa mali za shirika.”

 Katika ziara hiyo Mkurugenzi Mkuu Hamad ameupongeza Mkoa wa Kagera kwa kuwa kinara katika kujua kila kinachoendelea kwenye miradi ya shirika iliyopo Chato akieleza kwamba huo ni mfano wa kuigwa na kila mkoa wa NHC.

 Ameusifu pia kwa kuwa na ubunifu wa kuongeza mapato na kuwa na kiu kubwa ya kuendeleza maeneo muhimu yanayomilikiwa na shirika katika mkoa huo.

 "Mmenipa uchambuzi mzuri wa uanzishwaji wa miradi na namna miradi hiyo itakavyorudisha fedha za shirika zitakaxowekezwa hapa, nimependa sana ubunifu wenu wa kibiashara," amehitimisha Mkurugenzi Mkuu Hamad.

NAMBA NANE ALIYOCHEZA

1-Kwa kusisitiza upendo, umoja na kuzingatia maadili ya msingi ya shirika.

2-Kwa kuhimiza uadilifu na uaminifu ili kuongeza tija

3-Kuhimiza  kipaumbele makusanyo ya kodi, ubunifu kwa kuongeza mapato ya NHC

4- Usimamizi miradi ya ujenzi kikamilifu kwa uzalendo

5- Ataka kila mfanyakazi kuwa mlinzi wa mali za shirika

6- Ataka huduma bora kwa wateja izingatiwe

7- Atangaza miradi ya ubia isiyoendelezwa kutwaliwa

8- Aahidi bonasi, nyongeza ya mishahara kwa wafanyakazi

 

NAMBA TISA ALIYOCHEZA

Kutembelea mikoa tisa ya NHC ziara iliyotia chachu mpya ya utendaji katika kutimiza majukumu ya NHC

Awali, akiwasilisha taarifa ya Mkoa wa Kagera, Meneja wa NHC Mkoa huo,  Deogratius Batakanwa amemshukuru Mkurugenzi Mkuu  Hamad kwa ubunifu wake wa kupeleka rangi katika mikoa yote ambayo wameanza kuutumia kutengeneza nyumba na kupendezesha nyumba hizo.

Ameelezea kuwa siri ya mafanikio ya mkoa huo ni mshikamano na kuwa na mikakati ya kuwajengea umoja na uwajibikaji ikiwemo kuwa na timu ya michezo, kuwa na ‘breakfast meeting’, kuwa na ‘checkpoint’ katika tarehe za mwezi za kutathmini ukusanyaji wa mapato kwa asilimia na kuwa na ‘champion of the month’, ambaye huwa kama kiranja wa zamu wa mwezi husika, anayeratibu  utekelezaji wa kila jambo katika mkoa na kukumbusha kwa anayejisahau kutekeleza wajibu wake, kupitia "breakfast meeting".

Meneja wa NHC Mkoa wa Kagera, Deogratius Batakanwa(Wa kwanza kushoto), akitoa maelezo kuhusu miradi ya NHC inayotekelezwa katika mkoa wake, mbele ya Mkurugenzi Mkuu wa shirika hilo, Ahmad Abdallah(Aliyevaa shati  la mikono mirefu). (Picha kwa hisani ya NHC) 

Batakanwa amesema wilayani Ngara kuna fursa ya ujenzi wa nyumba kutokana na uwepo wa mradi wa ‘Nickel’ na kwamba mkoa wake utahakikisha kuwa kila fursa inayojitokeza wataitumia ili kuongeza mapato ya NHC.

Katika ziara hiyo Mkurugenzi Mkuu alifuatana na Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala Fatma Chillo, ambaye aliwaeleza wafanyakazi namna NHC inatakavyoondoa uhaba wa wafanyakazi katika ikama ya shirika kwa mfumo wa ‘job enrichment na job enlargement’, ambapo alizungumzia upandishwaji wa madaraja kwa mserereko akisema ni jambo litakalotekelezwa na NHC yenyewe bila kupitia utumishi.

Mkurugenzi Mkuu na ujumbe wake wamerejea jijini Dar es Salaam, akiwa ameacha furaha na matumaini mapya kwa wafanyakazi wa NHC, ambao walimpokea kwa bashasha na kuelezea kwa uwazi changamoto zinazoikabili mikoa hiyo na kuahidi kuzipatia ufumbuzi.

Chapisha Maoni

0 Maoni