Ni katika miradi 62 ya uendelezaji wa majengo inayotekelezwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), ikibadilisha nyumba za umma zilizochakaa kuwa vituo vya kisasa vya biashara na makazi, kuzalisha ajira, kuvutia uwekezaji na kuchochea ukuaji wa miji nchini.
Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com
Katika miji ya Tanzania inayoendelea kukua kwa kasi, wimbi
jipya la uwekezaji limeanza kubadili namna ardhi na mali za umma na binafsi zilizochakaa
na kuziwezesha kutumika kuchochea ukuaji wa Uchumi wa taifa.
Majengo yaliyokuwa ya Serikali, ambayo kwa muda mrefu
yalikuwa yamechakaa au kukosa ufanisi kwa kutotumika, sasa yanageuzwa kuwa
majengo ya kisasa ya biashara na makazi kupitia mpango kabambe wa Ushirikiano
kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), unaosimamiwa na Shirika la Nyumba
la Taifa (NHC).
Mpango huo hauishii katika kubomoa majengo ya zamani na
kujenga mapya, bali unalenga kufungua thamani ya mali za umma zilizokuwa
hazitumiki kikamilifu, kuvutia mitaji ya sekta binafsi na kuibua mazingira
mapya ya biashara yanayozalisha ajira, kuongeza shughuli za kiuchumi na
kuchangia maendeleo endelevu ya miji.
Mpango huo wa NHC wa uendelezaji wa mali na majengo umeifikia
miradi 62 katika maeneo mbalimbali nchini na kufikia thamani ya Sh535
bilioni, hivyo kuufanya kuwa miongoni mwa mipango mikubwa ya uhuishaji wa
maeneo ya mijini Tanzania.
Miradi hiyo inaashiria mabadiliko kutoka majengo
yaliyotumika chini ya uwezo wake kwenda kwenye miradi ya matumizi mchanganyiko,
inayojumuisha biashara na makazi.
Hatua hiyo inalenga kuzalisha thamani ya kiuchumi ya muda
mrefu huku ikikidhi mahitaji yanayoongezeka ya nafasi bora za biashara na
makazi ya kisasa.
Mpango huo pia unaonesha kuongezeka kwa imani ya wawekezaji
binafsi katika kushirikiana na taasisi za serikali kutekeleza miradi mikubwa
inayounganisha tija ya kibiashara na manufaa kwa umma.
Meneja Habari na Uhusiano wa Umma NHC, Yahya Charahani
anasema kuwa ajenda ya shirika hilo ya uendelezaji wa majengo hayo imevuka
hatua ya mipango na sasa iko katika utekelezaji, huku matokeo yakianza
kuonekana katika maeneo mbalimbali nchini.
“Mkakati wa uendelezaji umevuka hatua ya mipango na kuingia
katika utekelezaji, ambapo baadhi ya miradi tayari imekamilika, mingine iko
katika hatua za mwisho za kukamilika,” anasema Charahani.
Anabainisha kuwa awamu ya kwanza ya mpango huo ilihusisha miradi
21 ya ubia, ambayo mikataba yake ilisainiwa kati ya Aprili na Oktoba 2024,
ikiwa na thamani ya takribani Sh179 bilioni, huku muda wa utekelezaji
ukiwa kati ya miaka miwili na mitatu.
Kwa mujibu wa Charahani licha ya muda huo kuwa mfupi,
utekelezaji umeonesha mafanikio makubwa.
NHC inasema miradi mitatu imekamilika, wakati miradi
10 imefikia zaidi ya asilimia 80 ya utekelezaji. Miradi mingine minne iko
kati ya asilimia 50 na 79, huku minne iliyobaki ikiwa chini ya asilimia 50.
“Kwa ujumla, miradi 13 kati ya 21 ya awamu ya kwanza
imekamilika au imefikia zaidi ya asilimia 80, hali inayoonesha kasi nzuri
ya utekelezaji na kutoa msingi wa kupanua mpango huo. Mafanikio ya awamu ya
kwanza yameiwezesha NHC kuanzisha miradi mingine 41 ya uendelezaji, na
hivyo kuongeza jumla ya miradi hiyo kufikia 62 yenye thamani ya Sh535
bilioni,” anasema Charahani.
Anaeleza kwamba mpango huo una maana kubwa zaidi ya kujenga
miundombinu mipya na kwamba unaonesha namna ushirikiano kati ya sekta ya umma
na binafsi unavyoweza kuharakisha uwekezaji, huku ukiongeza tija ya ardhi na
mali zinazomilikiwa na Serikali.
Amesema badala ya kutegemea fedha za umma pekee, NHC
imetumia mfumo wa ubia unaounganisha mali za serikali na mitaji, utaalamu wa
uhandisi, ubunifu pamoja na uwezo wa sekta binafsi katika usimamizi wa miradi.
Charahani anasema mfumo huo unasaidia kuongeza thamani ya
mali za umma huku ukiwezesha kujengwa kwa miundombinu ya kisasa inayokidhi
mahitaji ya wafanyabiashara na wananchi.
“Kupitia ubia huu, tunabadilisha mali ambazo hazitumiki
kikamilifu kuwa rasilimali zenye tija zinazochangia ukuaji wa uchumi, wakati
huo huo tukitoa majengo ya kisasa kwa wafanyabiashara na wakazi,” anaeleza.
Charahani anasma matokeo ya mkakati huo yanaonekana wazi
katika maeneo ya Kariakoo, Dar es Salaam, mojawapo ya vituo vikubwa vya
biashara Afrika Mashariki.
“Miongoni mwa miradi iliyokamilika ni ule wa Salala
Solution Ltd, uliopo Kiwanja Na. 1/19 katika makutano ya Mitaa ya Uhuru na
Congo. Jengo hilo la biashara lenye Basement + Ghorofa ya Chini + Ghorofa
Tisa (B+G+9) limekamilika kwa asilimia 100 na tayari linafanya kazi,”anasema.
Anasema mradi huo umeongeza upatikanaji wa maeneo bora ya
ofisi na biashara katika eneo hilo lenye thamani kubwa kibiashara, huku
ukiendelea kuchangia mabadiliko ya sura ya Kariakoo.
Anataja mradi mwingine wa Mwigomelo Co. Ltd, uliopo
Kiwanja Na. 13/44 katika makutano ya Mitaa ya Aggrey na Sikukuu, umefikia asilimia
99 na kwa sasa uko katika hatua ya kukabidhiwa.
Kariakoo pia inaendelea kunufaika na miradi mingine
inayokaribia kukamilika.
Kwa mujibu wa NHC Mradi wa Mambo Sasa Msimbazi Fabrics,
uliopo katika Mitaa ya Congo na Tandamti, umefikia asilimia 96. Jengo
hilo la kisasa lenye B+G+10 linatarajiwa kuongeza nafasi za biashara
katika mojawapo ya maeneo yenye shughuli nyingi za kibiashara jijini Dar es
Salaam.
Vilevile, Shananga Group Ltd inatekeleza jengo la
matumizi mchanganyiko lenye B+G+9 katika eneo la Msimbazi, ambalo
limefikia asilimia 90 ya utekelezaji. Likikamilika, jengo hilo
litaongeza upatikanaji wa maeneo bora ya biashara na kukidhi mahitaji
yanayoongezeka ya majengo ya kisasa.
Mradi mwingine muhimu ni wa Kings Executive Apartment Ltd,
uliopo katika makutano ya Mitaa ya Swahili, Narung'ombe na Tandamti. Mradi huo
umefikia asilimia 91 na utatoa huduma za makazi ya kisasa pamoja na
maeneo ya biashara, ukiimarisha zaidi matumizi mchanganyiko ya majengo katikati
ya jiji.
Akizungumzia miradi ya nje ya Dar es Salaam, Charahani
anasema mkakati wa NHC unaendelea kuleta mabadiliko katika miji mingine yenye
shughuli kubwa za kiuchumi.
Anasema mkoani Mwanza, mradi wa JOBECE Logistics
Ltd, uliopo Mtaa wa Rwagasore, umefikia asilimia 99 na sasa uko
katika hatua ya kukabidhiwa. Ukianza kufanya kazi, jengo hilo linatarajiwa
kuongeza uwezo wa utoaji wa huduma na kufungua fursa mpya kwa wafanyabiashara
katika moja ya miji inayokua kwa kasi nchini.
“Kwa pamoja, miradi hiyo inaonesha namna PPP zinavyoweza
kuwa kichocheo cha mabadiliko ya kiuchumi. Majengo mapya ya biashara huvutia
wafanyabiashara, huongeza mapato ya upangishaji, huimarisha tija na kuzalisha
ajira wakati wa ujenzi na baada ya miradi kuanza kufanya kazi,” anasema.
Wakati huo huo, miradi hiyo inaongeza thamani ya mali,
inaboresha mwonekano wa miji na kuimarisha imani ya wawekezaji katika soko la
mali isiyohamishika nchini.
Kwa NHC, mpango huu si suala la kubadilisha majengo ya
zamani pekee. Ni mkakati wa muda mrefu wa kugeuza mali za umma kuwa injini za
maendeleo ya uchumi, sambamba na ajenda ya Serikali ya kukuza viwanda, biashara
na miji yenye ushindani.
Charahani anasema baadhi ya miradi iliyokamilika tayari
imeanza kutoa manufaa ya kiuchumi.
“Kati ya miradi 21 ya awamu ya kwanza, mitano imekamilika na
tayari inafanya kazi. Wafanyabiashara wameanza kuhamia na baadhi ya majengo
tayari yanatumika,” anasema.
Kujaa kwa wapangaji katika majengo yaliyokamilika kunaonesha
kuwa mahitaji ya maeneo bora ya biashara na makazi bado ni makubwa, hususan
katika maeneo muhimu ya kibiashara mijini.
Kadiri miji ya Tanzania inavyoendelea kupanuka, mahitaji ya
miundombinu ya kisasa, maeneo bora ya biashara na majengo yenye matumizi
mchanganyiko yanatarajiwa kuongezeka zaidi.
Kwa kuwa na miradi 62 yenye thamani ya Sh535 bilioni,
pamoja na miradi mingine iliyo katika maandalizi, mpango wa PPP wa NHC unazidi
kuwa mfano muhimu wa namna Serikali na sekta binafsi zinavyoweza kushirikiana
kugeuza mali za umma kuwa rasilimali zenye tija na kuchochea maendeleo ya
mijini.
Hatua hii inaifanya NHC isiwe tu mjenzi wa majengo, bali pia
mshirika muhimu katika kujenga miji yenye ushindani zaidi—miji ambayo biashara
zinaweza kukua, wananchi kunufaika na mali za umma kutoa thamani ya kudumu kwa
uchumi wa Tanzania.
Chapisha Maoni