- Washiriki 500 kukutana na fursa zenye tija katika sekta za kimkakati zinazolenga utekelezaji wa Dira ya Zanzibar 2050, wamo wawekezaji wa kimataifa, wajasiriamali, washirika wa maendeleo
Exuperius Kachenje, daimatznews@gmail.com
Siku zinakwenda kasi kuelekea Mkutano wa
Uwekezaji Zanzibar 2026 (Zanzibar Investment Summit – ZIS 2026), huku Mamlaka
ya Kukuza Uwekezaji Zanzibar (ZIPA) ikiongeza kasi ya kuvitangaza visiwa hivyo kimataifa,
kuwa ni kitovu kipya cha uwekezaji ikiweka mkazo kwenye sekta zenye zinazolenga
kuchochea ukuaji wa uchumi na maendeleo endelevu.
Saleh Saad Mohamed, Mkurugenzi Mtendaji wa ZIPA
Mkutano huo, unaoratibiwa na ZIPA, umepangwa
kufanyika Juni 3 hadi 5, 2026 ukitarajiwa kukutanisha washiriki kati ya 400
hadi 500 kutoka mataifa mbalimbali duniani, wakiwemo wawekezaji wa kimataifa,
watunga sera, taasisi za fedha, viongozi wa biashara, washirika wa maendeleo,
wajasiriamali pamoja na mashirika ya kimataifa kwa lengo la kujadili fursa za
uwekezaji zitakazochangia sura mpya ya maendeleo ya Zanzibar.
Akizungumza kuelekea mkutano huo, Mkurugenzi
Mtendaji wa ZIPA, Saleh Saad Mohamed, anasema maandalizi yanaendelea vizuri
huku Zanzibar ikiendelea kujijengea mazingira ya kuvutia uwekezaji kupitia
fursa zinazotekelezeka katika sekta mbalimbali muhimu.
Anaitaja kaulimbiu ya mkutano huo kuwa ni “Kukuza
mseto wa uwekezaji kwa maendeleo endelevu Zanzibar: Kujenga simulizi jipya la
ukuaji wa Zanzibar,” akieleza inaakisi dhamira ya Serikali ya Mapinduzi
Zanzibar kuimarisha uchumi jumuishi, kuongeza ushindani wa uwekezaji na
kupunguza utegemezi wa sekta chache za kiuchumi.
Saleh amesema mkutano huo unaofanyika wakati
Zanzibar imeshaidhinisha miradi ya uwekezaji 1,351 yenye thamani ya Dola za
Marekani14,291,020,523 takriban Shilingi 38.58 bilioni, hautakuwa tukio la
kawaida bali jukwaa la kimkakati litakalowezesha visiwa hivyo kuonesha safari
yake ya mageuzi ya kiuchumi na kuwaunganisha wawekezaji na miradi yenye tija
inayoweza kuharakisha ukuaji wa uchumi jumuishi na endelevu.
Kwa mujibu wa Saleh, ajenda ya mkutano huo
imejengwa sambamba na Dira ya Zanzibar 2050 ambayo inaweka msisitizo katika
uchumi wenye mseto, maendeleo ya miundombinu, ukuaji wa sekta binafsi pamoja na
kuongeza ushindani wa mazingira ya uwekezaji.
“Mkutano huu unatuma ujumbe wazi kuwa
Zanzibar iko tayari kwa biashara na inakaribisha ushirikiano wa muda mrefu
utakaosaidia kubadili sekta mbalimbali za uchumi na kuleta manufaa kwa
wananchi,” amesema.
Sekta kadhaa zimeainishwa kama nguzo za
mjadala na fursa kuu za uwekezaji katika mkutano huo, zikiwemo uchumi wa buluu,
kilimo na biashara ya mazao, viwanda na biashara, mafuta na gesi, uchumi wa
kidijitali, ubunifu, maendeleo ya miundombinu pamoja na utalii endelevu.
Katika eneo la uchumi wa buluu, Zanzibar
inalenga kuvutia uwekezaji katika uvuvi wa kisasa, ufugaji wa viumbe baharini,
usafirishaji wa majini, uchakataji wa mazao ya bahari kama mwani pamoja na
teknolojia za uhifadhi wa mazingira ya bahari.
Sekta ya kilimo na biashara ya mazao nayo
inatajwa kuwa na nafasi kubwa ya uwekezaji, hasa katika kuongeza thamani ya
mazao, usindikaji wa bidhaa za kilimo, usalama wa chakula, uzalishaji wa mazao
ya kuuza nje na teknolojia za kilimo himilivu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.
Katika sekta ya viwanda na biashara, fursa
zinatarajiwa kujikita katika uzalishaji wa bidhaa, minyororo ya ugavi,
usafirishaji wa mizigo, maeneo maalumu ya viwanda pamoja na ujumuishaji wa
masoko ya kikanda ili kuongeza ushindani wa uchumi wa Zanzibar.
Aidha, sekta ya mafuta na gesi pamoja na
nishati inatarajiwa kuvutia wawekezaji wanaotafuta fursa katika usalama wa
nishati na matumizi endelevu ya rasilimali.
Uchumi wa kidijitali nao umepewa uzito mkubwa
kupitia majadiliano yatakayohusu miundombinu ya TEHAMA, teknolojia za kifedha
(fintech), huduma za kidijitali, vituo vya ubunifu na mifumo ya kusaidia
ujasiriamali wa kisasa.
Miundombinu inatajwa kuwa moja ya maeneo
muhimu ya uwekezaji, ikijumuisha usafiri, bandari, barabara, maendeleo ya miji,
huduma za msingi na ushirikiano kati ya sekta ya umma na binafsi kwa lengo la
kuimarisha msingi wa ukuaji wa muda mrefu wa uchumi.
Utalii endelevu, ambao ni nguzo kuu ya uchumi
wa Zanzibar, pia utaendelea kuwa eneo muhimu la uwekezaji huku mamlaka
zikielekeza nguvu katika kuboresha huduma za ukarimu, kupanua utalii wa
mazingira na kuvutia uwekezaji wenye thamani kubwa unaozingatia uhifadhi wa
mazingira.
Mbali na kuonesha miradi ya uwekezaji,
mkutano huo unatarajiwa kuonesha maboresho ya sera na mifumo ya udhibiti
yatakayorahisisha mazingira ya biashara na kuongeza imani kwa wawekezaji wa
ndani na nje.
Kwa wawekezaji wanaotafuta masoko mapya yenye
ukuaji, Zanzibar inaonekana kujijenga upya kutoka uchumi unaotegemea zaidi
utalii kwenda uchumi wenye mseto unaotegemea ubunifu, ushindani, ustahimilivu
na maendeleo endelevu ya muda mrefu.
Mkutano huo Zanzibar Investment Summit 2026
ni hatua muhimu ya kuandika sura mpya ya uwekezaji na ushirikiano wa kimataifa
kwa maendeleo ya visiwa vya Zanzibar.
Chapisha Maoni