TRC YAONGEZA ULINZI SGR KWA TEKNOLOJIA MPYA

 -Yanunua magari ya kisasa yanayobaini hatari kabla ya ajali kwa teknolojia ya Laser

-Ni Ford Ranger maalum

-Uwekezaji utakaoongeza usalama, ufanisi huduma SGR.

Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Katika kuimarisha usalama wa reli ya kiwango cha kimataifa (SGR), Shirika la Reli nchini (TRC), limenunua magari maalum yanayotimia teknolojia ya laser kwa ajili ya kukagua na kufuatilia reli hiyo.

Moja ya magari maalum aina ya Ford Ranger yaliyonunuliwa na TRC kwa ajili ya ukaguzi wa reli ya SGR

Taarifa ya Kitengo cha habari na Mawasiliano imemnukuu Mkurugenzi Mkuu wa TRC, Mhandisi Machibya Masanja akieleza shirika hilo limenunua magari hayo aina ya Ford Ranger, yenye mfumo wa Hi-Rail.

"Magari hayo pia yana uwezo wa kubaini hitilafu za reli na vihatarishi mbalimbali kwa haraka na usahihi zaidi kuliko njia za kawaida za ukaguzi zilizokuwa zikitumika awali," amesema Mhandisi Masanja.

TRC yataja sababu uwekezaji huo

Kwa mujibu wa TRC, magari hayo maalum yana uwezo mkubwa wa kufanya kazi kwa haraka na uimara wa hali ya juu, yakiwa pia na uwezo wa kubadilika kwa urahisi kutoka barabarani kwenda kwenye mfumo wa reli.

Mkurugenzi Mkuu wa TRC, Mhandisi Masanja Machibya.

“Magari hayo yamefungwa vifaa maalum vya magurudumu ya reli, hivyo kuyawezesha kufanya kazi barabarani na kwenye reli kwa urahisi,” ameeleza Machibya.

Hali hiyo inatajwa kuwa sifa kubwa ya kipekee inayoyafanya kuwa bora kwa doria za kawaida na kutoa majibu ya haraka pale changamoto zinapotokea, zikiwa na nguvu kubwa inayoyawezesha kufanya kazi katika maeneo magumu, kubeba vifaa na kusaidia shughuli ngumu za ukaguzi wa reli.

Yatakavyoondoa ombwe la ukaguzi

TRC imeeleza kuwa magari hayo ni majibu ya haraka yanayoweza kuwassiadia wakaguzi kufika maeneo yenye changamoto kwa haraka zaidi, jambo linalotajwa kuwa litapunguza muda wa kusimama kwa huduma na kuongeza usalama wa wasafiri.

Sifa nyingine ya magari hayo imetajwa ni kuwa na uwezo wa kufanya doria umbali mrefu wa reli ya SGR, yakiwemo yenye mazingira magumu kufikika.

“Teknolojia ya laser uliopo kwenye magari hayo, unachunguza hali ya reli kwa kupima usahihi wa njia, kubaini shida yoyote katika reli ambavyo haviwezi kuonekana kwa macho ya kawaida,” amesema Mkurugenzi mkuu wa TRC na kuongeza:

“Inaweza pia kuimarisha usalama, kubaini mapema hitilafu kunasaidia kuzuia ajali, hata kulinda abiria na kuhakikisha huduma za reli zinaendelea kwa ufanisi.”

Teknolojia ya Laser ni nini?

Katika teknolojia ya Reli ya SGR, mifumo ya ukaguzi wa laser hutumia miale maalum yenye usahihi mkubwa kupima hali ya reli na ubora wa uso wa njia, ikiweza pia kubaini hata hitilafu ndogo sana katika mpangilio wa reli.

Kuhusu kasi, teknolojia hiyo inaelezwa kuwezesha ufuatiliaji wa moja kwa moja, wakati gari linaendelea kutembea kwenye reli, huku pia likitumika kubaini nyufa, maeneo yenye udongo dhaifu na hata kufuatilia mifumo ya umeme wa juu wa reli.

Kauli ya TRC na wasafiri

Akizungumzia zaidi magari hayo, Mkaguzi wa Njia wa TRC, Manyama Mazula amesema; “Haya siyo magari ya usafiri pekee, bali ni macho yetu kwenye reli.”

Mtumiaji usafiri wa SGR mara kwa mara, Akwilina Msangi anasema hatua hiyo ya TRC kununua magari hayo kunaongeza Imani kuhusu usalama wa safari za abiria kwa SGR.

“Kujua kuwa TRC inaweza kubaini matatizo kabla hayajatokea kunatufanya tujisikie salama zaidi,” amesema Msangi.

Msafiri mwingine aliyetambulika kwa jina la Zuberi Mkwama, amelipongeza Shirika la Reli Tanzania (TRC) kwa kununua magari hayo, akisema yataendelea kuhakikisha usalama wa abiria pamoja na mizigo.


Taswira kubwa zaidi

Uwekezaji huo unaonyesha dhamira ya TRC katika kuendelea kuboresha na kuifanya reli kuwa ya kisasa  kwa kuunganisha magari ya kisasa pamoja na teknolojia ya laser katika ukaguzi wa reli, hali ambayo inaifanya Tanzania kuendelea kuendana na viwango vya kimataifa vya usalama wa reli, hivyo kuhakikisha Reli ya SGR kutoka Dar es Salaam hadi Dodoma inaendelea kuwa mhimili salama na wa kuaminika wa usafiri wa Taifa.

 

Post a Comment

Mpya zaidi Nzee zaidi