Jumamosi, 30 Agosti 2025

Wagombea udiwani 16 Kigoma wakosa wapinzani

- Samia kunguruma Septemba 13

-Ndalichako kuwasha moto Sept 4

-Prof Yanga hapoi

Mwandishi Wetu, Kigoma

Wagombea udiwani 16 kupitia tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Kigoma wamebahatika kuwania nafasi hizo bila kupingwa, baada ya vyama vingine vya siasa mkoani humo kushindwa kusimamisha wagombea, huku kwenye baadhi ya kata wagombea wa upinzani wakielezwa kukosa sifa.

Rais Dk.Samia Samia Suluhu Hassan na Mwenyekiti wa Taifa wa CCM, akizungumza katika moja ya mikutano yake.

Katibu wa Siasa, Uenezi na Mafunzo CCM Mkoa wa Kigoma, Deogratius Nsokolo amebainisha hali hiyo akieleza kuwa kwa CCM hiyo ni dalili njema ya ushindi katika uchaguzi mkuu ujao Oktoba 29, 2025, ambapo sasa wagombea hao wanasubiri kupigiwa kura za ndiyo na hapana.

Nsokolo amezitaja kata hizo ambazo wagombea wa CCM wamekosa upinzani ni pamoja na zilizopo Wilaya ya Kasulu ambapo wagombea sita waliokosa wapinzani, Wilaya ya Buhigwe kata tano, Wilaya ya Kibondo  kata nne na Uvinza ikiwa kata moja ya Basanza.

"Mchakato wa kampeni za wagombea ubunge,udiwani na  za Urais za mgombea wa CCM, Samia Suluhu Hassan zitaendelea baada ya uzinduzi wa uliofanywa Viwanja vya Kawe jijini Dar es Salaam na kwamba Mgombea wa urais wa chama hicho atafanya mikutano ya  kampeni  mkoani humo Septema 13 mwaka huu," amesema.

Naye Mgombea Ubunge wa Jimbo la Kasulu Mjini, Profesa Joyce Ndalichako amesema atazindua kampeni za majukwaani Septemba nne na kwamba michakato mingine ya kampeni itaendelea kabla ya kuanza kwa mikutano hiyo ya hadhara.

Amesema miaka mitano ambayo amehudumu nafasi hiyo ya ubunge jimboni humo kulikuwa na changamoto kubwa ya barabara za jimbo hilo na kwamba sasa tayari  barabarani nyingine zimeanza kuchongwa, sambamba na utekelezaji wa mradi mkubwa wa maji, unaoendelea kutekelezwa, ambao utaondoa changanoto kubwa ya maji inayowakabili wananchi wa jimbo hilo.

Kwa upande wake, Mgombea Ubunge wa Jimbo la Buhigwe, Profesa Pius Yanda amesema baada ya uzinduzi wa kampeni uliofanywa na Mgombea uraisi wa chama hicho Agosti 28 mwaka huu,  watafanya kampeni bila kulala kuhakikisha ushindi wa wagombea wa chama hicho mwezi Oktoba mwaka huu.

Profesa Yanda amesema wakati anapambana kupata ridhaa ya wananchi kuongoza jimbo hilo, jambo la kwanza atakalolishughulikia akipewa ridhaa na wananchi kuwa mbunge ni barabara ndani ya jimbo, ambazo zitaunganisha jimbo hilo na barabara kuu ili ziweze kutafsiri kwa matendo uboreshaji wa miundo mbinu kuwezesha wakulima kuwa na barabara bora kwa usafirishaji wa mazao yao.Mwisho

BRELA ilivyojizatiti utoaji elimu, kusimamia Sheria ya Miliki Bunifu

- Usajili wapaa

- Miliki Bunifu 7 zasajiliwa kila siku ndani ya siku 365 

- Hataza 30

Exuperius Kachenje, daimatznews@gmail.com

Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), umejidhatiti kutoa elimu kwa wananchi, wasanii, wabunifu, watafiti na taasisi mbalimbali nchini kuhusu umuhimu wa kulinda na kusajili bunifu, sambamba na kusimamia utekelezaji wa Sheria ya Miliki Bunifu.

Waziri wa Viwanda na Biashara, Selemani Jafo(aliyeketi kulia) akisikiliza maelezo kutoka kwa Ofisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Godfrey Nyaisa kuhusu utendaji BRELA.

Hatua hiyo inalenga kuhakikisha wabunifu wananufaika na kazi zao, kukuza uchumi wa mtu mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla.

Miliki Bunifu nguzo ya maendeleo

Akizungumza katika maadhimisho ya Siku ya Kimataifa ya Miliki Bunifu Duniani yaliyofanyika Mei 21, 2025 jijini Dar es Salaam, Waziri wa Viwanda na Biashara Mhe. Dk. Selemani Jafo amesisitiza umuhimu wa wabunifu, wajasiriamali na wasanii kusajili bunifu zao ili kulinda haki zao kisheria.

Waziri Jafo amesema kauli mbiu ya mwaka huu, “Miliki Bunifu na Muziki: Sikiliza Mdundo wa Miliki Bunifu,” imelenga kuhamasisha wasanii na wabunifu wa sekta mbalimbali kutambua kwamba bunifu ni mali kama mali nyingine.

“Usajili wa bunifu ni hatua muhimu ya kuhakikisha wabunifu wananufaika na kazi zao wakiwa hai, na hata baada ya kufariki warithi wao watanufaika. Serikali imeweka mifumo thabiti ya ulinzi ili kuhakikisha ubunifu unaleta tija kwa Taifa,” amesema Jafo.

Aidha, ameuelezea mpango mkubwa wa Serikali wa kujenga viwanda 9,048 nchini kwa kipindi cha miaka sita kuanzia mwishoni mwa 2025 hadi mwaka 2031, akisema unatarajiwa kutoa ajira zaidi ya vijana milioni 6.5, ambapo bunifu na miliki bunifu vitakuwa nyenzo muhimu katika ustawi wa viwanda hivyo.

Elimu ya Miliki Bunifu vyuo vikuu, taasisi za utafiti

BRELA imekuwa mstari wa mbele katika kutoa elimu kwa vyuo vikuu, vyuo vya ufundi na taasisi za uzalishaji kuhusu umuhimu wa kulinda bunifu kupitia usajili wa hataza na alama za biashara.

Akizungumza Aprili 16, 2024 katika Chuo cha Waislamu Morogoro (MUM), Mkurugenzi wa Miliki Bunifu wa BRELA, Loy Mhando, alieleza:

“Bunifu nyingi katika vyuo zinatokana na tafiti za wanafunzi na wahadhiri. Tunahimiza bunifu hizi zisajiliwe ili walinziwe kisheria na ziweze kuwanufaisha wabunifu na jamii kwa ujumla.”

BRELA imetoa elimu katika vyuo mbalimbali vikiwemo;Chuo Kikuu cha Mzumbe, Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA), TaSUBa – Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo,Chuo cha Mafunzo ya Ufundi VETA, SIDO na Innovation Hub ya Taasisi ya Afya Ifakara (TAOTIC).

Lengo la BRELA kutoa elimu hiyo ni kuwajengea wabunifu uwezo wa kulinda bunifu zao, kupanua masoko na kupata manufaa ya kifedha kupitia tafiti na uvumbuzi.

Loy Mhando

Sauti za Wanufaika

Mmoja wa walionufaika na usajili wa Miliki Bunifu kutoka Kampuni ya TALANTA, Ronald Nakaka anasema kwa kusajili wa ubunifu unamwezesha kufanya kazi zake hadi nje ya Tanzania bila kikwazo kwani sheria ya kimataifa inampa ulinzi wa kazi zake hasa za sanaa ya muziki.

Anawahimiza watanzania hasa wajasiriamali vijana kusajili bunifu zao hatua inayoweza kuwafikisha kwenye ndoto zao kimaisha.

Siku ya Kimataifa ya Miliki Bunifu

Kila mwaka, BRELA hushiriki kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Miliki Bunifu lengo likiwaa kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kulinda na kusajili bunifu.

Katika maadhimisho ya mwaka huu, wadau kutoka COSOTA, BPRA, COSOZA, vyuo vikuu, wajasiriamali na wasanii walishirikishwa, huku BRELA ikiendesha warsha na mikutano ya wadau kujadili mikakati ya kukuza uelewa wa usajili wa bunifu na kuongeza ubunifu wenye tija kwa Taifa la Tanzania.

Ushirikiano na wadau

BRELA ilivyotoa elimu kwa wadau wake, taasisi za elimu na wajasiriamali kuhusu Miliki Bunifu.

Katika eneo hilo BRELA imeendelea kushirikiana na taasisi mbalimbali ikiwemo; COSOTA (Ofisi ya Hakimiliki Tanzania, BPRA (Wakala wa Usajili wa Biashara na Mali Zanzibar) COSOZA, Taasisi ya Utafiti wa Mbegu, taasisi za teknolojia na Shirika la Miliki Bunifu Duniani (WIPO).

Kupitia ushirikiano huo, Tanzania inaendelea kuimarisha mifumo ya kitaifa na kimataifa ya ulinzi wa bunifu, ikiwemo rasimu ya Mkataba wa Sheria ya Maumbo na Michoro Bunifu iliyojadiliwa Novemba 2024 jijini Riyadh, Saudi Arabia.

Mchango wa vyombo vya habari

Vyombo vya habari nchini vimekuwa mshirika muhimu wa BRELA katika kutoa elimu kwa umma.

Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile

Katika warsha iliyoandaliwa na BRELA kwa wahariri, Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile, aliwataka wahariri kuwa mabalozi wa elimu ya miliki bunifu:

“Baada ya kupata elimu hii, tunapaswa kuwafikishia Watanzania taarifa sahihi kuhusu miliki bunifu, umuhimu wa usajili na namna ya kunufaika na kazi zao,” ameeleza Balile.

BRELA inahimiza vyombo vya habari kushirikiana kwa karibu na taasisi hiyo kuhakikisha jamii inapata taarifa sahihi na kwa wakati.

Faida za kusajili bunifu

Kwa mujibu wa BRELA, usajili wa bunifu unatoa manufaa kadhaa, ikiwa ni pamoja na:

  • Ulinzi wa kisheria dhidi ya wizi au uvunjaji wa haki.
  • Fursa ya kupata mikopo kupitia taasisi za kifedha.
  • Kuongeza thamani ya bidhaa na huduma kwa kutumia alama za biashara.
  • Kupanua masoko ya kitaifa na kimataifa.
  • Kuwezesha wabunifu kufaidika kifedha na kazi zao.

Kupitia mikakati yake ya utoaji elimu, ushirikiano na wadau, na kuimarisha mifumo ya ulinzi wa bunifu, BRELA imejidhatiti kuhakikisha wabunifu, wasanii, watafiti na wajasiriamali nchini wanatambua thamani ya bunifu na kunufaika nazo.

Serikali imesisitiza kuwa, ifikapo mwaka 2030, miliki bunifu itakuwa nguzo muhimu ya ukuaji wa uchumi, kuongeza ajira na kuimarisha ushindani wa bidhaa na huduma za Tanzania katika masoko ya ndani na nje.

Changamoto

Hata hivyo, zipo changamoto zinazowakabili watanzania katika kulinda  Miliki Bunifu na Hataza. Kwa mujibu wa Ripoti ya Shirika la Kimataifa la Miliki Bunifu na Hataza(WIPO) , baadhi zikiwa ni ukosefu wa uelewa kuhusu Miliki Bunifu, Kushindwa kutekeleza Sheria ya Miliki Bunifu na Udhibiti mdogo wa matumizi yasiyo rasmi ya Miliki Bunifu na Hataza.

Msaada kwa wajasiriamali, wabunifu, wasanii

Ofisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Godfrey Nyaisa,(Pichani chini), amewataka wasanii, wabunifu na wajasiriamali kusajili majina ya bidhaa na huduma wanazotoa kupitia brand zao ili kuyalinda kisheria.

Godfrey Nyaisa
Kwa mujibu wa Nyaisa, usajili unawawezesha wabunifu kupata haki ya kipekee ya kutumia bunifu zao na kuzuia mtu mwingine kuziiga au kuzitumia kibiashara bila ridhaa yao. Aidha, unatoa fursa ya kukopesheka katika taasisi za kifedha kwa kuwa BRELA inatoa vyeti vinavyotambulika kisheria. 

BRELA inavyoboresha mifumo

Nyaisa anabainisha kwamba BRELA imechukua hatua mbalimbali kuhakikisha inaboresha mifumo ya usajili Miliki Bunifu na Hataza kwa kuanzisha mfumo wa usajili mtandaoni, Kuwezesha maombi wa njia rahisi na  kutoa mwongozo wa watumiaji.

Naye Dk. Ashatu Kijaji, Waziri wa zamani wa Viwanda na Biashara, amewataka wanawake wajasiriamali kusajili bunifu na biashara zao ili kuongeza thamani ya bidhaa na kulinda haki zao kisheria.

“BRELA inazilinda bunifu na biashara kisheria. Iwapo mtu ataiga kazi yako, una haki ya kumshtaki na BRELA itasimama kukutetea,” amesema Nyaisa kwa niaba ya Dk. Kijaji.

Wadau kulinda bunifu kimataifa

BRELA, kwa kushirikiana na Shirika la Miliki Ubunifu Duniani (WIPO), imeandaa rasimu ya Mkataba wa Sheria ya Maumbo na Michoro Bunifu inayolenga kuweka mfumo wa kimataifa wa kulinda bunifu.

Nyaisa, anasema kuwa sheria hiyo itakapopitishwa, wabunifu wa maumbo, vifungashio, mavazi na michoro mbalimbali watapata fursa ya kulinda bunifu zao katika nchi nyingi kwa kutumia ombi moja tu kupitia WIPO.

“Hii itapunguza gharama za ulinzi wa bunifu na kuongeza ushindani wa bidhaa na huduma za wabunifu wa Kitanzania katika soko la kimataifa,” anasema.

Hali ilivyo, muda na hatua za usajili

Akizungumzia hali ya usajili miliki bunifu ilivyo kwa sasa, Ofisa Usajili kutoka BRELA, Stanlaus Kigosi anaeleza kuwa kadiri siku zinavyokwenda, ndivyo mwamko wa watu kusajili kazi zao unavyoongezeka.

“Usajili sasa unachukua nafasi, mwamko unaongezeka kila siku. Hii inatokana na BRELA inavyoendelea kujitahidi kuwafikia wajasiriamali, vikundi vya wanawake, hata kutoa elimu kwenye vyuo vikuu na taasisi mbalimbali,” anasema Kigosi, huku akibainisha kwamba takwimu kamili za Miliki Bunifu zilizosajiliwa zipo nje ya uwezo wake.

Anafafanua kuwa katika usajili wa Miliki Bunifu, usajili wa Alama za Biashara unafanyika zaidi kuliko usajili wa Hataza, jambo linalotokana asili ya maeneo hayo mawili.

Wakati Alama za Biashara huweza kuchukua muda mfupi kubuniwa na kuwasilishwa BRELA kwa usajili, HATAZA uhitaji muda zaidi kutokana na kuhusisha zaidi Teknololojia ya Habari(IT), hivyo pia kuhitaji kuidhinishwa na taasisi au bodi husika kabla kuziombea usajili w Miliki Bunifu.

Kuhusu muda wa usajili Miliki Bunifu, Kigosi anabainisha kuwa usajili hufanyika na kukamilika ndani ya siku 90, ukijumuisha masuala mbalimbali ya kisheria na kanuni ndani nan je ya nchi, ikiwemo kufanyia uchunguzi Miliki Bunifu inayoomba kusajiliwa, kuitangaza kwa siku 60 ndipo husajiliwa ikiwa haikuwekewa kipingamizi.

Gharama usajili Miliki Bunifu

Akihitimisha maelezo yake, Kigosi anasema usajili wa Miliki Bunifu unaenda sanjari na kulipia gharama kwa mujibu wa sheria.

 “Miliki Bunifu husajiliwa kwa kulipiwa gharama ambayo ni Shilingi 130,000. Gharama hiyo ni nafuu ikilinganishwa na zinazotozwa na nchi nyingi za Ukanda wa Afrika Mashariki,” anasema Kigosi.

Takwimu  Miliki Bunifu

Akizungumza na mwandishi wa Makala haya, Mkuu wa Kitengo cha Habari na Mawasiliano ya Jamii wa BRELA, Joyce Mgaya ameeleza kuwa mamlaka hiyo ina Idara maalum inayokusanya na kuhifadhi takwimu za masuala mbalimbali yanayosimamiwa na  kutekelezwa na BRELA ikiwemo Miliki Bunifu na Hataza.

“Katika mwaka mmoja uliopita, BRELA imesajili Miliki Bunifu  takriban 2,615. Lakini pia Hataza zilizosajiliwa katika muda huo ni 30,” anasema Joyce.

Ametoa wito kwa wafanyabiashara, wajasiriamali kuzingatia sheria za nchi kwa kusajili Miliki Bunifu zao na Hataza, ili kuendana na matakwa ya kisheria, lakini pia kunufaika ya usajili huo ambao ni ulinzi kwa ubunifu na ugunduzi wao.

Serikali na Sera mpya ya Miliki Bunifu

Naibu Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo, Hamisi Mwinjuma (Mwana FA), anasema Serikali ipo mbioni kukamilisha Sera ya Miliki Bunifu itakayotoa mwongozo mpya wa ulinzi na usimamizi wa haki za wabunifu nchini.

“Maendeleo ya taifa yanategemea bunifu. Miliki bunifu zitaongeza kipato kwa wabunifu na kuchangia ukuaji wa uchumi kwa mtu mmoja mmoja na taifa kwa ujumla,” anasema Mwinjuma.

Sera hiyo itatoa mwanga kwa wabunifu kupata mikopo, kufikia masoko makubwa zaidi na kunufaika na ubunifu wao kikamilifu.

Kwa jitihada zake na kujitambua, BRELA inaendelea kujidhatiti na kuwa nguzo ya ulinzi na uendelezaji wa bunifu nchini. Inafanya hivyo kupitia elimu, ushauri, sera na ushirikiano na wadau wa ndani na nje ya nchi.

Ushindi wa BRELA katika kuwezesha utekelezaji wa Sheria ya Miliki Bunifu ni Ushindi wa Watanzania

Taasisi hiyo inalenga kuweka mfumo imara wa kuhakikisha wabunifu, wajasiriamali, wasanii na vyuo vikuu wananufaika na ubunifu wao.

Kwa usajili wa bunifu, Tanzania inalenga kuongeza kipato cha wabunifu, kukuza sekta ya viwanda, kupanua soko la kimataifa na kuchochea maendeleo ya taifa kwa ujumla.

 

Jumapili, 24 Agosti 2025

NHC yapata tuzo maalum vigezo vitano vikiibeba

Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) limetunukiwa tuzo maalum, baada ya kuibuka kuwa moja ya mashirika  ya umma yaliyofanya vizuri katika mwaka wa fedha 2023/24.

Tuzo hiyo imetolewa na Ofisi ya Msajili wa Hazina katika hafla rasmi iliyofanyika kwenye Kikao Kazi cha Wenyeviti wa Bodi na Watendaji Wakuu wa Taasisi za Umma, kilichofunguliwa rasmi Agosti 2,2025 na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Philip Mpango, jijini Arusha.

Tuzo hizo zilizingatia vigezo vya kiuendeshaji ikiwamo ukuaji wa mapato ya ndani, kuboresha ukwasi, rejesho la uwekezaji, udhibiti wa matumizi na kuimarisha faida.

Vigezo vingine ni kupunguza utegemezi wa ruzuku ya Serikali, ufanisi katika matumizi, utekelezaji wa hoja za kikaguzi za Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), uchapishaji wa taarifa za fedha, na maboresho ya utoaji huduma kwa jamii.

Taasisi nyingine zilizotunukiwa tuzo maalum zilitangazwa chini ya makundi manne mahsusi kulingana na aina na majukumu husika huku NHC likiwa katika  kundi la mashirika yanayofanya biashara,  ambapo tuzo zilitolewa kwa mashirika yaliyoboresha mapato, faida, ukwasi na rejesho kwa mtaji wa Serikali.

Pamoja na NHC katika kundi hilo wengine walioshinda ni  Bohari ya Dawa (MSD) na Shirika la Madini la Taifa (STAMICO).

 

Rais Samia ahimiza kudumisha amani, haki kuelekea Uchaguzi Mkuu

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema upo umuhimu wa kuhakikisha Taifa linaendelea kudumu katika misingi imara ya haki, amani, umoja na mshikamano wa kitaifa iliyowekwa na waasisi wa Tanzania , akieleza kwamba ili kudumisha misingi hiyo ushirikiano na mshikamano wa viongozi wa dini ni nguzo muhimu.

Rais Dk. Samia akizungumza katika Kongamano la Amani kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

Ameeleza hayo katika hotuba yake leo Agosti 24, 2025 kwenye Kongamano la Amani kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, ambalo liliandalia na Umoja wa Maimamu Tanzania (UMATA) na Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania.

Taarifa Ikulu iliyotolewa na Naibu Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Shaaban Kissu imeeleza kuwa Rais Dk. Samia amesema uchaguzi ni fursa ya kidemokrasia inayopaswa kwenda sambamba na kulinda amani na utulivu wa taifa.

 “Kudumisha amani ni utamaduni wetu tuliojijengea katika demokrasia ya uchaguzi. Tuendeleze utamaduni huu kabla, wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu,” amesema Rais Dk. Samia.

Amebainisha kuwa kipindi cha uchaguzi huongeza joto la kisiasa, lakini amani itaendelea kudumu ikiwa viongozi wa dini, kijamii na kisiasa watashirikiana kuhubiri amani na mshikamano kwa kuepusha migongano isiyo ya lazima.

Kuhusu nafasi ya wadau mbalimbali katika kudumisha amani wakati wa uchaguzi, Rais Dk. Samia amewataka wanasiasa kuepuka lugha za uchochezi katika kampeni,  badala yake kujikita katika sera na hoja.

Rais Dk. Samia pia ameeleza umuhimu wa kuzingatia maelekezo ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), pamoja na kutoa ushirikiano kwa vyombo vya ulinzi na usalama, huku  akikumbusha nafasi muhimu ya vyombo vya habari katika kuimarisha mshikamano wa kitaifa hasa katika kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu.

“Waandishi wa habari ni kundi muhimu kwa mustakabali wa amani ya nchi yetu. Kalamu zao zinaweza ama kudumisha au kuhatarisha amani ya nchi yetu,” amesema Rais Dk. Samia.

Amewahimiza Watanzania kujitokeza kwa wingi siku ya Uchaguzi Mkuu Oktoba 29, 2025, akibainisha kuwa kushiriki kupiga kura ni wajibu wa kikatiba na kizalendo unaojenga mustakabali wa taifa.

.

 

Jumatano, 20 Agosti 2025

Miezi 24 ya BRELA kuipigania Sheria ya Umiliki Manufaa

  --Yawafunda wamiliki wa kampuni, mawakili

-  Yaziwezesha taasisi za uchunguzi wa uhalifu kukabiliana na tatizo hilo

Na Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Katika harakati za kuimarisha uwazi na uwajibikaji kwenye sekta ya biashara na makampuni nchini, Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) umechukua hatua thabiti ili kukabiliana na vitendo vya uhalifu wa kifedha na utambuzi, kuhusu utambuzi wa wamiliki manufaa wa kampuni na majina ya biashara.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA),  Godfrey Nyaisa akikabidhi Tuzo kwa wafanyakazi wa  taasisi hiyo iliyotunukiwa baada ya kutoa gawio kwa Serikali la Shilingi Bilioni 20.4  kwa mwaka 2024. BRELA imepata Tuzo hiyo katika kipengele cha Taasisi zilizofanya vizuri kwa utoaji gawio kwa wakati kwa mwaka 2025

.

BRELA imeeleza kuwa hatua hizo ni utekelezaji wa Pendekezo Na. 24 la Kundi Kazi la Kimataifa la Kupambana na Uhalifu wa Kifedha (FATF), linalosisitiza uwazi katika umiliki wa kampuni kama njia ya kuzuia matumizi ya kampuni katika uhalifu wa kifedha, kama vile utakatishaji fedha na ufadhili wa ugaidi.

Ikiwa ni wajibu wake kisheria kwa taifa, lakini pia utekelezaji wa sheria ya kimataifa, BRELA imefanya juhudi hizo kwa takriban miaka miwili, tangu mwaka 2023 yalipofanyika mabadiliko ya kisheria, ikitumia njia mbalimbali kupiga vita wanaokiuka sheria ya umiliki manufaa ambayoni ya kimataifa.

Njia ambazo BRELA imezitumia ni pamoja na kutoa elimu kwa taasisi za kiuchunguzi wa uhalifu, zinazosimamia sheria, wafanyabiashara hata taasisi za elimu ya juu, maeneo mbalimbali nchini.

Katika muda huo wa miaka miwili iliyopita BRELA imetekeleza jukumu hilo kwa kutoa mafunzo hayo, ambayo yalifanyika mikoa mbalimbali nchini yakihusisha taasisi saba muhimu za kitaifa.

Taasisi hizo ni pamoja na TAKUKURU, Jeshi la Polisi, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka.

Nyingine ni Uhamiaji, Mahakama ya Tanzania pamoja na Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, huku BRELA ikiweka wazi lengo kuu la mafunzo hayo kuwa ni kuwawezesha wadau hao muhimu kutekeleza kwa ufanisi jukumu lao la kuzuia na kupambana na uhalifu wa kifedha kwa kushirikiana na wakala hiyo katika kutambua wamiliki halisi wa makampuni na majina ya biashara.

Kitaifa BRELA pia ina dhamana ya kuendesha na kuhifadhi kanzidata za usajili wa makampuni na majina ya biashara, hivyo kuimarisha ushirikiano na taasisi za uchunguzi ni hatua muhimu ya kuhakikisha kuwa taarifa hizi nyeti zinatumika kwa ufanisi katika mapambano dhidi ya uhalifu wa kifedha.

Elimu hiyo pia inatolewa na BRELA kwa mawakili, taasisi binafsi, wamiliki wa kampuni na wafanyabiashara wakubwa, wa kati hata wa chini, ili kuepuka kuingia mikononi mwa sheria kwa kukiuka Sheria ya Umiliki Manufaa.

Mkurugenzi wa Makampuni na Majina ya Biashara wa BRELA, Isdori Nkindi, anaeleza kuwa; ”Kutokana na jukumu hilo, kila nchi mshirika wa FATF inapaswa kuhakikisha taasisi zake zote zinazohusika na kupambana na uhalifu wa kifedha, zinaelewa vyema namna ya kufikia taarifa sahihi za umiliki manufaa, ili kusaidia kuzuia uhalifu kabla haujatokea.”

Isdor Nkindi

Anasisitiza kwamba kutokana na ukweli kuwa BRELA ndiyo msimamizi wa sajili za makampuni na majina ya biashara nchini,  taasisi za uchunguzi zina wajibu wa kutumia taarifa hizo ipasavyo pindi tu vinapojitokeza viashiria vya uhalifu.

BRELA inaeleza kuwa hiyo ni mojawapo ya njia za kuzuia uhalifu kabla haujatokea, kwa kuhakikisha taasisi zote zinazungumza lugha moja na kufanya kazi kwa ushirikiano wa karibu.

Nkindi anawakumbusha maofisa wa taasisi hizo kufuata utaratibu wa kisheria wa kuomba taarifa kutoka BRELA kupitia taasisi zao, badala ya maofisa mmoja mmoja kuomba taarifa binafsi, jambo analosema linaweza kuathiri mchakato mzima wa ukusanyaji wa taarifa na ushahidi.

Mafunzo hayo yamepokelewa kwa mtazamo chanya na wadau walioshiriki, wakiwemo mawakili na wafanyabiashara, ambao walipata fursa ya kuelewa kwa kina dhana ya umiliki manufaa na umuhimu wake katika kusaidia utekelezaji wa haki na sheria nchini.

Kupitia mikakati hii, BRELA inaonesha kwa vitendo dhamira yake ya kuhakikisha kuwa kampuni na biashara zilizopo nchini zinawajibika kwa mujibu wa sheria na hazitumiki kama kichaka cha kuficha uhalifu wa kifedha. Hii ni hatua muhimu kuelekea kujenga mazingira ya biashara yenye uwazi, uwajibikaji na uadilifu, yanayochochea maendeleo endelevu ya kiuchumi nchini.

Washiriki wa kikao kazi kuhusu Dhana ya Wamiliki Manufaa  iliyotolewa na BRELA kwa wadau, wakiwemo mawakili na wafanya biashara jijini Arusha, wakifuatilia mafunzo hayo mapema Februari 27, 2024.


Mabadiliko ya Sheria ya Fedha ya Mwaka 2020, ndiyo yaliyopitisha marekebisho kwenye Sheria ya Kampuni Sura 212 pamoja na Kanuni za Wamiliki Manufaa wa Kampuni na Kanuni za Majina ya Biashara (Umiliki Manufaa) za Mwaka 2023 pia kanuni zake kupitishwa na Waziri mwenye dhamana na biashara nchini."

Waandishi wa habari pia wana fursa ya kipekee kutumia vyombo vyao kusaidia kufikisha elimu kuhusu dhana ya Wamiliki Manufaa ili wadau na wananchi wote waielewe na kuitii. 

Mkurugenzi wa Makampuni na Majina ya Biashara wa BRELA, Isdori Nkindi, anasisitiza kwamba katika  kuisimamia Sheria ya Umiliki Manufaa, wanaendelea kuelimisha wadau, lakini pia kushirikiana na vyombo vya usalama kudhibiti na kuwasaka wanaovunja sheria hiyo.                                                  

 

Miezi 24 ya BRELA kuipigania Sheria ya Umiliki Manufaa

 --Yawafunda wamiliki wa kampuni, mawakili

-  Yaziwezesha taasisi za uchunguzi wa uhalifu kukabiliana na tatizo hilo

Na Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Katika harakati za kuimarisha uwazi na uwajibikaji kwenye sekta ya biashara na makampuni nchini, Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA) umechukua hatua thabiti ili kukabiliana na vitendo vya uhalifu wa kifedha na utambuzi, kuhusu utambuzi wa wamiliki manufaa wa kampuni na majina ya biashara.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA),  Godfrey Nyaisa akikabidhi Tuzo kwa wafanyakazi wa  taasisi hiyo iliyotunukiwa baada ya kutoa gawio kwa Serikali la Shilingi Bilioni 20.4  kwa mwaka 2024. BRELA imepata Tuzo hiyo katika kipengele cha Taasisi zilizofanya vizuri kwa utoaji gawio kwa wakati kwa mwaka 2025

.

BRELA imeeleza kuwa hatua hizo ni utekelezaji wa Pendekezo Na. 24 la Kundi Kazi la Kimataifa la Kupambana na Uhalifu wa Kifedha (FATF), linalosisitiza uwazi katika umiliki wa kampuni kama njia ya kuzuia matumizi ya kampuni katika uhalifu wa kifedha, kama vile utakatishaji fedha na ufadhili wa ugaidi.

Ikiwa ni wajibu wake kisheria kwa taifa, lakini pia utekelezaji wa sheria ya kimataifa, BRELA imefanya juhudi hizo kwa takriban miaka miwili, tangu mwaka 2023 yalipofanyika mabadiliko ya kisheria, ikitumia njia mbalimbali kupiga vita wanaokiuka sheria ya umiliki manufaa ambayoni ya kimataifa.

Njia ambazo BRELA imezitumia ni pamoja na kutoa elimu kwa taasisi za kiuchunguzi wa uhalifu, zinazosimamia sheria, wafanyabiashara hata taasisi za elimu ya juu, maeneo mbalimbali nchini.

Katika muda huo wa miaka miwili iliyopita BRELA imetekeleza jukumu hilo kwa kutoa mafunzo hayo, ambayo yalifanyika mikoa mbalimbali nchini yakihusisha taasisi saba muhimu za kitaifa.

Taasisi hizo ni pamoja na TAKUKURU, Jeshi la Polisi, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka.

Nyingine ni Uhamiaji, Mahakama ya Tanzania pamoja na Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali, huku BRELA ikiweka wazi lengo kuu la mafunzo hayo kuwa ni kuwawezesha wadau hao muhimu kutekeleza kwa ufanisi jukumu lao la kuzuia na kupambana na uhalifu wa kifedha kwa kushirikiana na wakala hiyo katika kutambua wamiliki halisi wa makampuni na majina ya biashara.

Kitaifa BRELA pia ina dhamana ya kuendesha na kuhifadhi kanzidata za usajili wa makampuni na majina ya biashara, hivyo kuimarisha ushirikiano na taasisi za uchunguzi ni hatua muhimu ya kuhakikisha kuwa taarifa hizi nyeti zinatumika kwa ufanisi katika mapambano dhidi ya uhalifu wa kifedha.

Elimu hiyo pia inatolewa na BRELA kwa mawakili, taasisi binafsi, wamiliki wa kampuni na wafanyabiashara wakubwa, wa kati hata wa chini, ili kuepuka kuingia mikononi mwa sheria kwa kukiuka Sheria ya Umiliki Manufaa.

Mkurugenzi wa Makampuni na Majina ya Biashara wa BRELA, Isdori Nkindi, anaeleza kuwa; ”Kutokana na jukumu hilo, kila nchi mshirika wa FATF inapaswa kuhakikisha taasisi zake zote zinazohusika na kupambana na uhalifu wa kifedha, zinaelewa vyema namna ya kufikia taarifa sahihi za umiliki manufaa, ili kusaidia kuzuia uhalifu kabla haujatokea.”

Isdor Nkindi

Anasisitiza kwamba kutokana na ukweli kuwa BRELA ndiyo msimamizi wa sajili za makampuni na majina ya biashara nchini,  taasisi za uchunguzi zina wajibu wa kutumia taarifa hizo ipasavyo pindi tu vinapojitokeza viashiria vya uhalifu.

BRELA inaeleza kuwa hiyo ni mojawapo ya njia za kuzuia uhalifu kabla haujatokea, kwa kuhakikisha taasisi zote zinazungumza lugha moja na kufanya kazi kwa ushirikiano wa karibu.

Nkindi anawakumbusha maofisa wa taasisi hizo kufuata utaratibu wa kisheria wa kuomba taarifa kutoka BRELA kupitia taasisi zao, badala ya maofisa mmoja mmoja kuomba taarifa binafsi, jambo analosema linaweza kuathiri mchakato mzima wa ukusanyaji wa taarifa na ushahidi.

Mafunzo hayo yamepokelewa kwa mtazamo chanya na wadau walioshiriki, wakiwemo mawakili na wafanyabiashara, ambao walipata fursa ya kuelewa kwa kina dhana ya umiliki manufaa na umuhimu wake katika kusaidia utekelezaji wa haki na sheria nchini.

Kupitia mikakati hii, BRELA inaonesha kwa vitendo dhamira yake ya kuhakikisha kuwa kampuni na biashara zilizopo nchini zinawajibika kwa mujibu wa sheria na hazitumiki kama kichaka cha kuficha uhalifu wa kifedha. Hii ni hatua muhimu kuelekea kujenga mazingira ya biashara yenye uwazi, uwajibikaji na uadilifu, yanayochochea maendeleo endelevu ya kiuchumi nchini.

Washiriki wa kikao kazi kuhusu Dhana ya Wamiliki Manufaa  iliyotolewa na BRELA kwa wadau, wakiwemo mawakili na wafanya biashara jijini Arusha, wakifuatilia mafunzo hayo mapema Februari 27, 2024.


Mabadiliko ya Sheria ya Fedha ya Mwaka 2020, ndiyo yaliyopitisha marekebisho kwenye Sheria ya Kampuni Sura 212 pamoja na Kanuni za Wamiliki Manufaa wa Kampuni na Kanuni za Majina ya Biashara (Umiliki Manufaa) za Mwaka 2023 pia kanuni zake kupitishwa na Waziri mwenye dhamana na biashara nchini."

Waandishi wa habari pia wana fursa ya kipekee kutumia vyombo vyao kusaidia kufikisha elimu kuhusu dhana ya Wamiliki Manufaa ili wadau na wananchi wote waielewe na kuitii. 

Mkurugenzi wa Makampuni na Majina ya Biashara wa BRELA, Isdori Nkindi, anasisitiza kwamba katika  kuisimamia Sheria ya Umiliki Manufaa, wanaendelea kuelimisha wadau, lakini pia kushirikiana na vyombo vya usalama kudhibiti na kuwasaka wanaovunja sheria hiyo.                                                  

 

Jumatatu, 18 Agosti 2025

Saa 144 za CCM kutaja kikosi chake bungeni

-Wagombea presha inapanda, presha inashuka

Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Saa 148 zimesalia kuanzia leo Agosti 18, kabla ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), kutangaza majina ya wateule wake kwa nafasi za ubunge watakaochuana na wagombea vyama vya upinzani katika Uchaguzi Mkuu ujao Oktoba 29, 2025 ili kuingia bungeni. 

Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan

Muda huo ambao ni sawa na siku sita, unawaacha wagombea waliopita kwenye kura za maoni ngazi ya jimbo, presha zao zikipanda na kushuka, wakisubiri kwa hamu uamuzi wa vikao vya kitaifa vya CCM vya uteuzi, ambavyo uamuzi wake ni wa mwisho.

Vikao hivyo vinafanyika huku kukiwa na kumbukumbu ya baadhi ya wagombea majina yao kutorudi kwenye mchujo wa awali mwaka huu, lakini pia kuwepo waliokatwa kwenye uteuzi wa mwisho katika vikao kama hivyo, mwaka 2020 ambapo CCM ilikuwa chini ya uenyekiti wa hayati John Magufuli, aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.  

Agosti 17, 2025, CCM kimetangaza ratiba ya vikao vyake vya kitaifa, kikieleza vitafanyika chini ya Mwenyekiti wa CCM na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan.

Kwa mujibu wa taarifa ya CCM, iliyotolewa na kusainiwa na  Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa, Itikadi, Uenezi na Mafunzo, CPA Amos Makalla Agosti 17, 2025, Kamati Kuu ya Halmashauri Kuu ya CCM Taifa itafanya kikao chake Agosti 21 Agosti 2025, kikifuatiwa na Kikao cha Halmashauri Kuu ya CCM (NEC).Taifa kitakachofanyika Agosti 23, 2025.

"Ajenda ya vikao hivyo itakuwa ni uteuzi wa; Wagombea Ubunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Wabunge wa Viti Maalum, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, na Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Viti Maalum," imeeleza taarifa hiyo ya CCM..

Taarifa hiyo imehitimisha kwamba, viikao vyote vitafanyika jijini Dodoma, yalipo makao makuu ya chama hicho

Jumapili, 17 Agosti 2025

Samia Housing Scheme Kawe: Ndoto makazi bora ya kisasa imetimia

-Kutoka wazo, ramani hadi uhalisia
-Wamiliki wapigwa msasa, waanza kukabidhiwa nyumba zao

Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com
Barabara zimekamilika, mifereji ya maji safi na maji taka iko tayari, taa za barabarani na kamera za usalama zimeshawekwa, huku bustani na miti michache ikipamba mitaa na kuleta utulivu. 

Ukiwa maeneo hayo asubuhi utashuhudia jua linapochomoza, lakini jioni jua linapozama juu ya majengo hayo mapya, likiongeza mvuto wa rangi za nyumba hizo mpya zilivyopangiliwa kwa umaridadi, zisizochosha kutazama.

Eneo hilo pia lina vizuia moto, mifumo ya kisasa ya utiririshaji maji na barabara za ndani  zilizokamilika, mitandao ya umeme imetengenezwa, na maeneo ya kijamii yameundwa kwa ustadi, pamoja na bustani.

Mradi huo  wenye nyumba 560 unaunganisha maisha ya kisasa, faraja, na mshikamano wa kijamii, lakini pia kutoa mwonekano unaochochea hisia za kifahari. 

NHC sio tu limekamilisha mradi huo, bali pia siku limeanza kukabidhi kwa wamiliki wake nyumba hizo, ambao walisubiri miaka mitatu kwa hamu  kutimia  ndoto hiyo, iliyofanikishwa kwa jitihada za Shirila la Nyumba la Taifa , chini ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah, nyumba hizo zina thamani ya Sh, bilioni 48, ukiwa ni mpango mkubwa zaidi unaolenga kujenga nyumba 5,000 kote nchini, ambao ukikamilika utakuwa na thamani ya Sh bilioni 466.

Mkurugenzi Mkuu wa NHC Hamad Abdallah

Kila nyumba imejengwa kwa ubora wa hali ya juu, kwa kuzingatia mazingira ya kijamii, usalama wa familia, na uhakika wa kuwa na thamani ya muda mrefu. 

Bila shaka huu ni mfano wazi wa dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita, ya Rais Samia ikilenga kuhakikisha Watanzania wanapata makazi bora ya heshima, yenye thamani na ustawi, yakiwa yamejengwa maghorofa 10 yenye ghorofa kumi kila moja, yaliyosanifiwa na timu ya NHC ya wasanifu majengo yaliozingatia mtiririko wa hewa kutoka Bahari ya Hindi. 

Hii ndiyo taswira ya ustaarabu, faraja na mshikamano wa kijamii walionao wamiliki wa nyumba eneo la Kawe kwenye Mradi wa nyumba bora za makazi wa Samia Housing Scheme, mkoani Dar es Salaam, uliofanikishwa na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC).

Mkutano wa kwanza wa wamiliki wa nyumba

Kutokana na kukamilika mradi huo wa Kawe, hivi karibuni wamiliki watapatiwa taarifa kuhusu miundombinu, sheria, ada za matengenezo, bima na usajili wa huduma.
Si hivyo tu bali sasa kimeanzishwa Chama cha Wamiliki wa Nyumba (Homeowners Association – HOA) kitakachoratibu usimamizi na maendeleo ya eneo hilo.
Wateja wa nyumba za NHC Samia Scheme, Kawe wakiwa kwenye mkutano na watendaji wa Shirika la Nyumba la Taifa, kuhusu ukaazi katika nyumba hizo.

Kabla ya makabidhiano rasmi, NHC imeandaa Mkutano wa Kwanza wa Wamiliki wa Nyumba utakaofanyika Jumamosi, 16 Agosti 2025, eneo la mradi. Mkutano huu unaashiria mwanzo wa maisha mapya ya pamoja.

Sherehe ya kukabidhi funguo za mfano, kukata utepe na picha za pamoja zitahitimisha hafla, huku alama rejeleo #SamiaHousingScheme ikitamba kwenye mitandao ya kijamii kusambaza furaha hii kwa taifa zima.

Kwa nini mradi umepewa jina la Rais Samia
Mradi huu umepewa jina la Rais Samia kuenzi mchango wake mkubwa katika mageuzi ya NHC, yaliyowezesha taasisi kupata mikopo, kukamilisha miradi iliyokwama kwa miaka nane, na kuongeza uwezo wake wa kifedha.
Wateja wa nyumba za Samia Housing Scheme-Kawe wakifuatilia mkutano wao na NHC

Mbali na Kawe, NHC linaendeleza miradi mingine mikubwa ikiwemo Soko la Madini Mirerani, 2H Plaza Morogoro, Tabora Commercial Complex, na Meru Shops Arusha

Miradi hii inaimarisha ajira, mapato na huduma kwa wananchi, ikiashiria kwamba uwekezaji wa makazi ni kichocheo cha maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Samia Housing Scheme inabaki kuwa zaidi ya mradi wa nyumba – ni hadithi ya matumaini, mabadiliko na ustawi wa taifa. Kila nyumba ni sehemu ya historia binafsi ya mmiliki, kila bustani ni alama ya familia, na kila awamu mpya ni ahadi ya mustakabali bora kwa vizazi vijavyo.mradi huu unawakilisha mafanikio ya mageuzi ya kiutendaji na kiushirikiano yaliyofanikisha makazi bora kwa Watanzania.

Mradi huu ni sehemu ya mpango wa uboreshaji wa miji, unaotekelezwa kwa njia kadhaa: kuvunja majengo ya zamani na kuyajenga upya, kuendeleza vitovu vya miji (satellite city), kuimarisha maendeleo ya miliki, na kuendeleza miradi ya ubia pamoja na nyumba za gharama kubwa. Ni mradi unaochangia si tu kwa makazi, bali pia kwa maendeleo ya miundombinu na mpangilio wa miji unaolenga kuongeza thamani ya maisha ya wakazi.

Mpango wa NHC unafanya faida inayopatikana kutokana na nyumba za gharama kubwa inarejeshwa kwa jamii, kwa kujenga nyumba za bei nafuu ambazo Watanzania wa kipato cha chini wanaweza kumudu. Hii ni ishara dhahiri ya dhamira ya Shirika ya kuunganisha ufanisi wa kifedha na ustawi wa jamii.

Mradi wa Samia Housing Scheme- Kawe unawakilisha mafanikio ya mageuzi ya kiutendaji na kiushirikiano yaliyofanikisha makazi bora kwa Watanzania.

Mbali na mradi huo, NHC pia inaeleza kuwa miradi mbalimbali inabuniwa na kujengwa katika miji na majiji, huku asilimia 75 ya biashara ya nyumba ikihusisha Dar es Salaam ikihusiana na mikoa mitano ya Shirika. Faida ya Shirika imeongezeka kutoka Sh. bilioni 198 miaka mitano iliyopita hadi Sh. bilioni 235 mwaka huu, jambo linalothibitisha ukuaji endelevu wa mpango wa makazi na ufanisi wa miradi.

Hadi sasa, nyumba 5,399 ziko kwenye mpango wa kuuza na kupangisha kwa gharama ya jumla ya Sh. bilioni 659.48, kati ya hizo nyumba 3,217 zimekamilika, na nyumba 2,182 ziko katika hatua mbalimbali za ujenzi ambazo zinatarajiwa kukamilika ifikapo Juni 2026. Hii inaonesha wazi kuwa mradi huu sio wa kawaida; bali ni matokeo ya sera bora, mageuzi makuu, na dhamira thabiti ya Shirika ya kuleta makazi bora kwa Watanzania wote.

Kwa msingi huu, mradi umepewa jina la heshima ili kuwakilisha dhahiri mageuzi, usimamizi bora, na mchango wa Shirika katika kuhakikisha kila Mtanzania ana makazi salama, ya kisasa, na yenye thamani ya muda mrefu.

Miradi minginne ya NHC

NHC siyo tu limejenga majengo ya kisasa, bali limeibua matumaini mapya kwa maelfu ya Watanzania, huku likichochea uchumi, kuzalisha ajira, na kuboresha taswira ya miji na mikoa mbalimbali, jambo ambalo ni ishara wazi ya jinsi taasisi za umma zinavyoweza kuleta mabadiliko chanya katika maisha ya watanzania.

Miradi ya NHC imeenea katika miji mikubwa na mikoa ya pembezoni, ikilenga kutoa makazi salama, ya kisasa, na yenye thamani. 

NHC pia linaendeleza miradi ya kibiashara na ukarabati wa majengo ya zamani, ikionyesha ushirikiano wa miradi ya makazi na biashara. Mradi wa Soko la Madini Mirerani, 2H Plaza Morogoro, Tabora Commercial Complex, na Meru Shops Arusha unaimarisha ajira, mapato na huduma kwa wananchi. 

Hali hii inathibitisha kuwa uwekezaji katika makazi hauishii kwenye nyumba pekee, bali unachochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi kwa ujumla

Serikali sasa kusaini muongozo mshahara KCC kwa Sekta Binafsi

Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

SERIKALI imesema hivi karibuni inatarajia kusaini muongozo wa Kima Cha Chini Cha Mshahara (KCC) kwa TaasisiI Minafsi zinazofanywa kazi nchini, ili kuwa sheria.

Waziri wa Nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi,Ajira  Vijana na Wenye Ulemavu, Ridhiwan Kikwete.

Imesema katika miongozo huo inatarajia kuainisha viwango vipya vya mshahara ambapo wafanyakazi Wa sekta binafsi watakuwa wanalipwa.

Waziri wa Nchi,Ofisi ya Waziri Mkuu Kazi,Ajira  Vijana na Wenye Ulemavu, Ridhiwan Kikwete amesema hayo jijini Arusha katika uzinduzi wa Jengo la Biashara Shirikisho la Vyama Vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA), lililoko mkabala na soko kuu, jijini humo.

Kuhusu miongozo huo Ridhiwan amesema tayari mazungumzo yameshafanyika baina ya wadau ambao ni taasisi binafsi na wasimamizi wa sera, pamoja na uongozi wa timu Ya Wizara uliopewa jukumu la kusimamia marekebisho hayo.

Amesema kikao kilichobakia ni cha mashauri ,ambapo watashauriana na wenzao juu ya viwango vilivyowekwa na baada ya hapo mapema mwezi ujao huenda wakasaini marekebisho hayo.

“Nawaambia wafanyakazi kuwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan anathamini sana maslahi yenu,” amesema Ridhiwan na kuongeza: "Serikali Itaendelea kuboresha Sheria za Wafanyakazi Ili ziendane na mahitaji yao."

Kwa mujibu wa Ridhiwan, Serikali  itaendelea kushirikiana na wafanyakazi bega kwa bega katika kutekeleza mikakati ya kuongeza ajira, kulinda haki za wafanyakazi, na kuimarisha mifumo ya utatuzi wa migogoro kwa njia ya mazungumzo.


Waomba kuondolewa vikwazo biashara ya mazao ya kilimo Ikolojia mipakani

Mussa Juma,Arusha

Serikali katika nchi za Afrika ya Mashariki, zimeombwa kuondoa vikwazo vinayoathiri biashara za mazao ya kilimo Ikololojia mipakani, hasa kwa wajasiriamali wadogo, ili kuwezesha kukuza biashara hiyo.

Utafiti uliofanywa kuhusu biashara za kilimo Ikolojia (Kilimo Hai) mipakani zimebaini kuwepo kwa changamoto kadhaa ikiwemo viwango vya ubora wa bidhaa,mifumo ya ulipaji kodi,vikwazo vya barabarani,udhibiti wa bidhaa zisizo na ubora na uelewa mdogo wa wajasiriamali katika masuala ya biashara ya mipakani.

Akisoma mapendekezo ya kisera yaliyotokana na  warsha ya wadau kuhusu biashara  ya mipakani kwa mazao ya bidhaa za kilimo Ikolojia, Ofisa wa Utetezi na Ushawishi wa Shirikisho la  Wakulima Tanzania (SHIWAKUTA), Thomas Laizer amesema   wamekubaliana kuwa ni  muhimu, kuchukuliwa hatua madhubuti ili kuondoa au kupunguza vikwazo visivyo vya kikodi (NTBs), ikiwemo mazuio yasiyo rasmi ya barabarani, ambayo kwa kiasi kikubwa inaathiri biashara za mipakani (cross-border trade).  

Laizer amesema  vikwazo hivyo  sio tu  vinavuruga mfumo wa kibiashara, bali vinamuumiza mkulima kutokana na ukweli kwamba wafanyabiasha huishia kununua mazao kwa bei ya chini kufidia hasara wanayoitarajia kukumbana nayo wasafirishapo mazao. 

"Hali hii huchochea wafanyabiashara na wazalishaji kutumia njia zisizo rasmi (njia za panya) kusafirisha mazao na bidhaa na hivyo kukosesha serikali mapato ambayo huyatumia kuwaletea wananchi maendeleo,"amesema

Amesema pia wanapendekeza Serikali na wadau, kuchukua hatua ya kuwekeza katika kuwaelimisha wakulima kuhusu mahitaji ya kisera na kisheria yanayohusu uzalishaji wa mazao na bidhaa za kilimo ikolojia ili kuwawezesha kushiriki kikamilifu katika biashara za mipakani na kukuza uchumi wa kilimo endelevu.

Laizer amesema, pia wanaihimiza Serikali  kuchukua jukumu la msingi katika kuweka miundombinu wezeshi, sera rafiki na mikakati shirikishi ili kuwawezesha Watanzania kufikia masoko ya kimataifa kwa bidhaa ghafi na zilizosindikwa, hivyo kuongeza thamani ya mazao na kukuza pato la taifa.

"Tunatambua na kukubali kuwa uwepo wa wanunuzi na wafanyabiashara toka nje ni fursa kwa wazalishaji wadogo nchini na  Tunatoa wito kwa serikali yetu kuweka mazingira wezeshi na ya uwazi yatakayolinda maslahi ya wazalishaji wa ndani kwa kuhakikisha biashara inayoendeshwa inanufaisha wazalishaji hao, inazingatia haki na usawa, na serikali inapata mapato stahiki ili kuweza kuwaletea wananchi wake maendeleo"alisema

Laizer amesema  , wamekubaliana Serikali ya Tanzania inapaswa kuzijengea uwezo wa kirasilimali, ikiwa ni pamoja na rasilimali watu na vifaa, mamlaka zinazodhibiti ubora wa mazao ili ziweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi na kuhakikisha walaji wanalindwa dhidi ya mazao yaliyozalishwa kwa kutumia pembejeo zenye viambata hatarishi kwa afya na mazingira.

Ameongeza kuwa wanapendekeza  Bunge la Afrika Mashariki (EALA) kutumia nafasi yake kuzihimiza nchi wanachama kuweka sera na mikakati ya pamoja itakayoielekeza Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) kuwa ukanda wa uzalishaji na biashara ya mazao na bidhaa zilizozalishwa kiikolojia, kwa lengo la kulinda afya ya walaji, kuhifadhi mazingira na kuongeza ushindani wa bidhaa za ukanda huu katika masoko ya kikanda na kimataifa.

Awali, wakizungumzia utafiti huo uliofanywa na Washauri wa Biashara za Kilimo Ikolojia mpakani, kwa udhamini wa  Shirika la Muungano wa Uhuru wa Chakula Afrika(AFSA), Ofisa Miradi wa SHIWAKUTA na MVIWAARUSHA,Damian Sulumo  amesema iwapo vikwazo vya biashara ya mazao ya kilimo Ikolojia vikiondolewa uzalishaji utaongezeka.

Sulumo amesema hata hivyo, bado kunahitajika mafunzo kwa wafanyabiashara wa bidhaa za kilimo Ikolojia  ili kuboresha bidhaa zao na badala kuendelea kuuza nje bidhaa kama  malighafi wanatakiwa kuuza bidhaa zilizosindikwa katika masoko ya kimataifa.

Mshauri wa Biashara za Mazao ya Kilimo Ikolojia wa AFSA , Africa Kiiza  ambaye aliongoza utafiti huo, amesema anaamini mapendekezo waliyoyatoa baada ya utafiti huo, yatafanyiwa kazi.

Amesema AFSA ,kwa kushirikiana na wadau wengine, itaendelea kuwajengea uwezo wadau mbalimbali, ikiwepo wabunge wa EAC,Wanahabari  na wafanyabiashara wamazao ya kilimo Ikolojia.

Mratibu wa SHIWAKUTA,  Richard Masandika amesema utafiti huo uliofanyika katika mipaka ya  Tanzania na Kenya, Kenya na Rwanda na mipaka mingine katika nchi za Afrika ya Mashariki, umekuwa na manufaa makubwa.

Amesema wanaimani kuna taratibu za kikanda na kiserikali za EAC, zinazoweza kufanywa ili kuondoa vikwazo kwa wafanyabiashara wa bidhaa za kilimo Ikolojia.

Wadau wa kilimo Ikolojia katika nchi za Afrika ya Mashariki, wakiwepo wakulima, vyama vya wakulima, watafiti na wanahabari za kilimo Ikolojia walishiriki warsha ya siku mbili jijini Arusha, kuhusiana na utafiti uliofanywa wa AFSA  kuhusiana na biashara za kilimo Ikolojia (Kilimo Hai) mipakani.

Jumatano, 6 Agosti 2025

Job Ndugai afariki dunia

 Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com 

Spika wa Bunge la 12, Job Ndugai amefariki dunia, jijini Dodoma.

Marehemu Job Ndugai

Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Bunge imemnukuu Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson ikieleza kuwa Spika mstaafu, Ndugai ambaye alikuwa Mbunge wa Kongwa, amefariki dunia leo Agost 6 mwaka 2025. Taarifa zaidi zinaeleza kuwa Ndugai amefariki wakati akiendelea kupatiwa matibabu katika moja ya hospitali jijini Dodoma.

"Kwa masikitiko makubwa, naomba kutoa taarifa ya kifo cha kiongozi wetu, mwanasiasa mkongwe na Spika mstaafu wa Bunge, Mheshimiwa Job Yustino Ndugai, kilichotokea leo jijini Dodoma.

Natoa pole kwa familia ya marehemu, ndugu, jamaa na wananchi wa Jimbo la Kongwa. Mwenyezi Mungu awape moyo wa uvumilivu na subira kipindi hiki kigumu," amesema Spika wa Bunge, Dk. Tulia Ackson.

Spika mstaafu Ndugai amefariki dunia siku moja baada ya kutangazwa kushinda kura za maoni kuwania tena kiti cha Ubunge Jimbo la Kongwa kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), nafasi aliyokuwa akiishikilia, hadi Bunge lilipovujwa kwa mujibu wa sheria Agosti 3,2025.