Rais Samia ahimiza kudumisha amani, haki kuelekea Uchaguzi Mkuu

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan, amesema upo umuhimu wa kuhakikisha Taifa linaendelea kudumu katika misingi imara ya haki, amani, umoja na mshikamano wa kitaifa iliyowekwa na waasisi wa Tanzania , akieleza kwamba ili kudumisha misingi hiyo ushirikiano na mshikamano wa viongozi wa dini ni nguzo muhimu.

Rais Dk. Samia akizungumza katika Kongamano la Amani kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025.

Ameeleza hayo katika hotuba yake leo Agosti 24, 2025 kwenye Kongamano la Amani kuelekea Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2025, ambalo liliandalia na Umoja wa Maimamu Tanzania (UMATA) na Jumuiya ya Maridhiano na Amani Tanzania.

Taarifa Ikulu iliyotolewa na Naibu Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu, Shaaban Kissu imeeleza kuwa Rais Dk. Samia amesema uchaguzi ni fursa ya kidemokrasia inayopaswa kwenda sambamba na kulinda amani na utulivu wa taifa.

 “Kudumisha amani ni utamaduni wetu tuliojijengea katika demokrasia ya uchaguzi. Tuendeleze utamaduni huu kabla, wakati na baada ya Uchaguzi Mkuu,” amesema Rais Dk. Samia.

Amebainisha kuwa kipindi cha uchaguzi huongeza joto la kisiasa, lakini amani itaendelea kudumu ikiwa viongozi wa dini, kijamii na kisiasa watashirikiana kuhubiri amani na mshikamano kwa kuepusha migongano isiyo ya lazima.

Kuhusu nafasi ya wadau mbalimbali katika kudumisha amani wakati wa uchaguzi, Rais Dk. Samia amewataka wanasiasa kuepuka lugha za uchochezi katika kampeni,  badala yake kujikita katika sera na hoja.

Rais Dk. Samia pia ameeleza umuhimu wa kuzingatia maelekezo ya Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), pamoja na kutoa ushirikiano kwa vyombo vya ulinzi na usalama, huku  akikumbusha nafasi muhimu ya vyombo vya habari katika kuimarisha mshikamano wa kitaifa hasa katika kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu.

“Waandishi wa habari ni kundi muhimu kwa mustakabali wa amani ya nchi yetu. Kalamu zao zinaweza ama kudumisha au kuhatarisha amani ya nchi yetu,” amesema Rais Dk. Samia.

Amewahimiza Watanzania kujitokeza kwa wingi siku ya Uchaguzi Mkuu Oktoba 29, 2025, akibainisha kuwa kushiriki kupiga kura ni wajibu wa kikatiba na kizalendo unaojenga mustakabali wa taifa.

.

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Sanamu ya Bikira Maria yaonekana ndani ya Hifadhi ya Taifa Saadani

Kapteni Traole afuata huduma za afya nchini

Wawekezaji wa Oman watua nchini, wateta na NHC kuchochea mapinduzi sekta ya makazi