Trump atimua kazi maelfu ya watumishi wa umma

Washington, Marekani. Serikali ya Rais Donald Trump nchini Marekani, imetangaza kuwaachisha kazi maelfu ya wafanyakazi ikiwa ni sehemu ya mpango wake mkubwa wa kupunguza wafanyakazi, unaohusiana na kufungwa kwa taasisi za Serikali.

Rais Donald Trump wa Marekani

Ofisi ya Usimamizi na Bajeti ya nchi hiyo (OMB) imeeleza katika hati za mahakama kuwa notisi ya kuachishwa kazi zimetumwa kwa takribani wafanyakazi 4,200 katika wizara na taasisi za serikali nane.

Kwa mujibu wa Mtandao wa Forbs leo, hatua hiyo iliyoanza jana Oktoba 9-2025, inafuatia kesi iliyofunguliwa na Shirikisho la Wafanyakazi wa Serikali ya Marekani (AFGE), chama kikubwa zaidi cha wafanyakazi wa Serikali kinachowakilisha wafanyakazi 800,000 kufungua kesi ikipinga wafanyakazi hao kuachishwa kazi.

Kwa mujibu wa OMB, karibu wafanyakazi 1,500 wa Wizara ya Fedha ya Marekani wameachishwa kazi, wakiwemo takribani wafanyakazi 1,300 kutoka Mamlaka ya Mapato ya Marekani (IRS), kama ilivyoripotiwa na Bloomberg.

Wizara ya Afya na Huduma za Kibinadamu (Health and Human Services Department) pia imeathirika kwa kiwango kikubwa na hatua hiyo, ambapo OMB imeripoti kuwa takriban wafanyakazi 1,200 wameachishwa kazi.

Awali, Gazeti la The New York Times, liliripoti kuwa makumi ya wafanyakazi waliokuwa wakifanya kazi katika Vituo vya Kudhibiti na Kuzuia Magonjwa (CDC) wamepokea barua za kuachishwa kazi siku ya jana Oktoba 9-2025, wakiwemo takribani maofisa 70 wa Huduma za Uchunguzi wa Magonjwa ya Mlipuko (Epidemic Intelligence Service) na baadhi ya wafanyakazi wa jarida la Morbidity and Mortality Weekly Report.

Kwa mujibu wa nyaraka za mahakama, Wizara ya Usalama wa Ndani (Department of Homeland Security) imewajulisha wafanyakazi 176 kwamba wataachishwa kazi, wote wakiwa ni watumishi wa Wakala wa Usalama wa Mtandao na Miundombinu (Cybersecurity and Infrastructure Security Agency), kama ilivyoripotiwa na PBS.

Maelezo kuhusu hatua hizo za kuwaachisha kazi yametolewa hadharani Ijumaa jioni jana, muda mfupi baada ya Mkuu wa Bajeti wa White House, Russ Vought, kutangaza kupitia mtandao wa X kwamba “mchakato wa kupunguza wafanyakazi umeanza.”
Baada ya tangazo hilo, Chama cha Wafanyakazi wa AFGE kilifungua haraka ombi mahakamani kikipinga hatua hiyo na kutaka izuiliwe mara moja.

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Sanamu ya Bikira Maria yaonekana ndani ya Hifadhi ya Taifa Saadani

Kapteni Traole afuata huduma za afya nchini

Wawekezaji wa Oman watua nchini, wateta na NHC kuchochea mapinduzi sekta ya makazi