Makamu wa Rais alivyotoa maagizo, NHC yafunguka

- Mkurugenzi Hamad aeleza NHC ilivyogusa kila mkoa Tanzania

- NHC ilivyong’ara mkutano wa Wenyeviti wa Bodi, Wakurugenzi Arusha

Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. Phillip Mpango, ameliagiza Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), kuongeza juhudi zake katika ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, lengo likiwa ni kuhakikisha wananchi wote wanaostahili kupata makazi wanapata fursa hiyo kupitia shirika hilo.

Makamu wa Rais Dk. Isdor Mpango(Wa kwanza Kulia) akitembelea mabanda ya maonyesho ya shughuli zinazofanywa na taasisi za umma Viwanja vya AICC, Arusha hivi karibuni.

Dk. Mpango ametoa agizo hilo wakati alipotembelea banda la NHC kwenye viwanja vya Kituo cha Kimataifa cha Mikutano cha Arusha (AICC), wakati wa Kongamano la Wenyeviti wa Bodi na Wakuu wa Taasisi za Umma.

Alizungumza kwa niaba ya Rais Samia Suluhu Hassan ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye kongamano hilo lililofanyika kuanzia tarehe 23 Agosti, 2025.

"Nawaagiza muongeze juhudi za ujenzi wa nyumba za gharama nafuu ili muwawezeshe wananchi wote wanaotamani au kuhitaji kumiliki nyumba za NHC wapate nafasi hiyo," alisema Dk. Mpango.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hammad Abdallah, amelitolea majibu agizo hilo akieleza kuwa shirika hilo kwa sasa lina mpango mkubwa unaolenga kuhakikisha agizo hilo linafanyiwa kazi kwa ufanisi.

Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah (Wa kwanza kushoto), akitoa maelezo kwa Makamu wa Rais, Dk. Philip Mpango(Wa pili kulia), kuhusu miradi inayotekelezwa na shirika hilo, wakati Makamu wa Rais alipotembelea banda la NHC nje ya Ukumbi wa AICC jijini Arusha, lilipofanyika Kongamano la Wenyeviti wa Bodi na Wakurugenzi Watendaji wa taasisi za umma nchini, chini ya Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH), hivi karibuni.

"Tuna miradi karibu kote nchini Tanzania kwa sasa hivi," amesema  Hamad, na kuongeza kuwa hatua zote zinazohitajika zinaendelea ili wananchi waweze kumiliki nyumba zilizojengwa na NHC kwa urahisi.

Kuhusu miradi ya NHC mkoani Arusha, Hamad ameeleza kuwa kuna mradi wa nyumba 711 ambao tayari asilimia 20 ya nyumba hizo zimeuzwa na ujenzi unaendelea. "Ni moja ya miradi ya muda mrefu iliyokwama, lakini tunashukuru Serikali kwa kutuwezesha kuukwamua. Tulirudi kukopa na sasa ni mradi ambao una tija kubwa kwa taifa," amesema.

Ameongeza kuwa mkoani Arusha NHC pia ina miradi mingine ikiwemo Mradi wa Safari City ambao NHC imenunua ekari 500 za ardhi, imetengeneza mpango wa jumla (master plan), inaweka miundombinu na kuuza viwanja kwa wananchi.

"Awamu ya kwanza tulimaliza kuuza viwanja na sasa tunaandaa awamu ya pili. Baada ya kuuza viwanja tulipata tija kubwa, sasa tumekuja na mradi wa awamu ya tatu tayari tumeuanza ujenzi na tumeshauza asilimia 25 ya nyumba hizo," amefafanua Hamad.

Hamad alimueleza Makamu wa Rais kuwa NHC inafanya miradi mikubwa katika mikoa mbalimbali nchini, akikitaja mkoa wa Morogoro ambapo una miradi miwili, Tanga kwenye mradi wa jengo kubwa la Mkwawani Plaza, na Iringa kwenye Mradi wa Iringa Plaza.

 "Kwa hiyo karibu maeneo yote ya nchi tumeweza kuyagusa, Mheshimiwa Makamu wa Rais," amesema.

Mbali na Makamu wa Rais, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, George Simbachawene naye ametembelea banda la NHC kwenye kongamano hilo. Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah, aliongoza maonesho ya huduma na fursa mbalimbali zinazotolewa na shirika hilo, zilizovutia viongozi na wadau wa sekta ya fedha na umma.

Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah (Kulia),  akisalimiana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora George Simbachawene, wakati waziri huyo alipotembelea banda la shirika hilo na kupata maelezo kuhusu miradi inayotekelezwa na shirika hilo, wakati wa maonyesho nje ya Ukumbi wa AICC jijini Arusha lilipofanyika Kongamano la Wenyeviti wa Bodi na Wakurugenzi Watendaji wa taasisisi za umma chini ya Ofisi ya Msajili wa Hazina (OMH), hivi karibuni

Kongamano hilo liliwakutanisha viongozi wa mashirika ya umma, wenyeviti wa bodi na watunga sera, kwa lengo la kujadili mbinu za kuimarisha taasisi za umma na mchango wao katika maendeleo ya taifa. Banda la NHC lilivutia wengi ikiwemo mawaziri, wenyeviti wa bodi, wakurugenzi wa taasisi za umma na wananchi, wakionyesha dhamira ya shirika la kushirikisha wadau wengi katika utekelezaji wa majukumu yake.

Katika kongamano hilo, NHC pia ilipata tuzo maalum kutoka Ofisi ya Msajili wa Hazina kwa kuwa moja ya mashirika ya umma yaliyofanya vizuri katika mwaka wa fedha 2023/24.

Tuzo hiyo ilipokelewa na Mwenyekiti wa Bodi wa NHC, Dk. Sophia Kongelo na Mkurugenzi Mkuu,Hamad Abdallah.

Vigezo vilivyotumika katika utoaji tuzo ni pamoja na ukuaji wa mapato ya ndani, kuboresha uwazi, rejesho la uwekezaji, udhibiti wa matumizi, kuimarisha faida, kupunguza utegemezi wa ruzuku ya Serikali, ufanisi katika matumizi, utekelezaji wa hoja za kikaguzi, uchapishaji wa taarifa za fedha, na maboresho ya utoaji huduma kwa jamii.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Sanamu ya Bikira Maria yaonekana ndani ya Hifadhi ya Taifa Saadani

Kapteni Traole afuata huduma za afya nchini

Wawekezaji wa Oman watua nchini, wateta na NHC kuchochea mapinduzi sekta ya makazi