Wafanyakazi wa majumbani wamwangukia Rais Samia -

-Wamwomba aridhie Mkataba wa ILO kuwaokoa taabuni

Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassa, imeombwa kukamilisha mchakato wa kuridhia Mkataba wa Kimataifa wa Kazi wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) namba 189 na kupitisha ili kuwezesha haki za msingi za wafanyakazi wa majumbani.

Rais Samia Suluhu Hassan

Ombi hilo limetolewa na wafanyakazi wa majumbani, wakieleza kuwa mkataba huo wa kazi zenye staha utawasaidia kupata haki na kuheshimiwa kama wafanyakazi wa sekta nyingine.

Wametoa ombi hilo walipokuwa wakizungumza katika Kikao Kazi kilichowakutanisha kwa siku mbili mjini Morogoro, ambapo wamepata Mafunzo ya Utatuzi wa Migogoro ya Wafanyakazi wa Majumbani.

Mwenyekiti wa Wafanyakazi wa Majumbani Tanzania, Zanini Athuman anasema mkataba huo wa ILO unaweka wazi stahiki halali kwa wafanyakazi wa majumbani, ikiwemo kupewa mapumziko ya kutosha, kuishi katika mazingira ya heshima (hasa kwa wanaoishi kwa waajiri).

“Pamoja na uwepo wa sheria mbalimbali hapa nchini zinazolitambua kundi hilo, bado kuna ugumu katika utekelezaji wake, kutokana na sheria kutoruhusu nyumba ya mtu binafsi kuwa ofisi ya kazi. Mwarobaini pekee unaotazamiwa ni kuridhiwa kwa mkataba huo,” amesema Zanini.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu Chama cha Wafanyakazi wa Majumbani, Hifadhini, Mahotelini, Huduma za Kijamii na Ushauri (CHODAWU) Said Wamba, amewahimiza wafanyakazi wa majumbani kujiunga katika vyama mbalimbali vya wafanyakazi, ili kuwa na sauti ya pamoja ya kupambania haki na stahiki zao.

“Tunajaribu kuwainua hawa wafanyakazi wa majumbani, wapo chini mno, hili si jambo la CHODAWU pekee, bali jamii nzima ya Watanzania ina jukumu la kufanya kuwaokoa kwa sababu wanafanya kazi kubwa na muhimu kwa waajiri wao na taifa kwa ujumla, lakini hawapati matunda ya jasho lao,”amesema Wamba.

Shirika la Kazi Duniani (ILO) limewakutanisha kwa pamoja mkoani Morogoro Tume ya Usuruhishi na Uamuzi (CMA) Taasisi ya Serikali inayohusika na utatuzi wa migogoro ya kazi Tanzania Bara pamoja na wawakilishi wa wafanyakazi wa majumbani katika kikao kazi cha siku mbili, lengo likiwa kutafuta mwarobaini wa pamoja wa kukabiliana na changamoto zinazolikumba kundi hilo muhimu katika jamii na Taifa kwa ujumla.

 

Mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo, Desdelia Saimon, amesema kuchelewa kwa mchakato wa kuridhia mkataba huo kunawafanya waendelee kufanya kazi katika mazingira hatarishi, ikiwemo ukosefu wa haki ya faragha na maisha binafsi pamoja na kinga ya kisheria ya kutosha.

Naye Nasra Seleman kutoka Dar es Salaam amesema; “Endapo Serikali itaridhia mkataba huo, utatufungulia mambo mengi kwa sababu, mkataba huo unatuhusu moja kwa moja sisi wafanyakazi wa majumbani. Tunamuomba Rais Samia Suluhu Hassan aridhie mkataba huo ili na sisi tutendewe haki kama wafanyakazi wengine.”

Awali, akizungumza katika ufunguzi wa kikao hicho, Mratibu wa Mradi wa Kuboresha Utambuzi na Mazingira ya Kazi kwa Wafanyakazi wa Majumbani kutoka ILO, Chiku Semfuko amesema kwamba mafunzo hayo yatawawezesha wafanyakazi wa majumbani kutambua mahali sahihi panapofaa kupeleka migogoro yao na kupata utatuzi.

Naye Mkurugenzi na Mtendaji Mkuu CMA Tanzania Bara, Usekelege Mpulla, amesema tayari mwongozo maalumu wa utatuzi wa migogoro ya wafanyakazi kwa ajili ya wafanyakazi wa majumbani pekee umeshaandaliwa, lengo likiwa kutafsiri utatuzi wa migogro pamoja na kutekeleza matakwa ya kisheria pamoja na mkataba wa ILO namba 189.

“Tumejipanga kuhakikisha haki za wafanyakazi wa majumbani zinatolewa kwa wakati na mafunzo haya yatakapokamilika, tunaamini wasuluhishi wanaohusika na migogoro watapata uwezo wa kumaliza migogoro kwa haraka,” amesema Mpulla.

 

Awali, Kamishna Msaidizi Idara ya Kazi, Ofisi ya Waziri Mkuu, kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Rehema Moyo aliyekuwa mgeni rasmi kwenye mafunzo hayo amesisitiza CMA kuhakikisha wanatoa kipaumbele kushughulikia migogoro ya wafanyakazi wa majumbani kutokana na ugumu wa mazingira ya kazi wanayopitia kupata stahiki zao.

“Ni muhimu pia hata wafanyakazi wenywe wa majumbani wajue haki zao. Pamoja na kuwa vyombo vya kisheria  vipo, lakini lazima wapewe elimu wa kutambua wapi waende kupata utatuzi wa migogoro yao,” amesema.

 

Baadhi ya wafanyakazi majumbani waliohudhuria mafunzo hayo walieleza umuhimu wa Serikali kuridhia na kuupitisha Mkataba Namba 189 wa ILO.

 

Summary: Kuridhiwa kwa mkataba namba189 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO) ni hatua muhimu ya kuwapa wafanyakazi wa majumbani hadhi, heshima na ulinzi wanaostahili katika mazingira yao ya kazi. ucheleweshaji wa mchakato huo huendelea kuwafanya wafanyakaizi wa majumbani kufanya kazi katika mazingira hatarishi huku wakikosa mikataba rasmi, mapumziko, haki ya faragha na kinga ya kisheria

 

Mwisho.

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Sanamu ya Bikira Maria yaonekana ndani ya Hifadhi ya Taifa Saadani

Kapteni Traole afuata huduma za afya nchini

Wawekezaji wa Oman watua nchini, wateta na NHC kuchochea mapinduzi sekta ya makazi