Mafanikio ya NHC mageuzi ya makazi Tanzania

-Yaja kivingine na Nyumba Bond

- Fursa mpya kwa wananchi kupata nyumba bora

Mwandishi Wetu, daimatznews@gmail.com

Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) limepata mafanikio makubwa katika kipindi cha miaka mitano iliyopita, huku likijidhihirisha kuwa  chombo muhimu katika ajenda ya mageuzi ya miji na maendeleo ya sekta ya makazi Tanzania.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la
Nyumba la Taifa (NHC), Hamad Abdallah

Chini ya Serikali ya Awamu ya Sita, inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan, NHC limeongeza wigo utendaji wake kupitia uwekezaji wa kimkakati kwenye sekta ya ardhi na majengo, usimamizi bora wa miradi na uanzishaji wa ushirikiano mpya kati ya sekta ya umma na binafsi.

Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah anabainisha hayo, huku akimshukuru Rais Samia Suluhu kwa uamuzi wake wa kuingilia kati na kuikwamua miradi mikubwa kadhaa ya NHC iliyokwama, ambayo sasa imeanza tena baada ya kusimama kwa karibu miaka minane.

Hamad aliyekuwa akizungumza na  wahariri wa vyombo mbalimbali vya Habari Abdallah amesema hatua hiyo ya Rais Samia imefungua njia ya maendeleo.

 Anasema shirika lake limefanikiwa kupata faida ya jumla ya Shilingi bilioni 235.4 kabla ya kodi, huku Shilingi bilioni 36.8 ikipatikana katika mwaka wa fedha uliopita pekee, kwa mujibu wa ripoti zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG).

Hamad anabainisha kuwa kufikia Juni 2024,thamani ya mali za NHC ilifikia Shilingi trilioni 5.5.

Mkurugenzi huyo wa NHC, anaweka wazi kuwa katika kipindi hicho, mchango wa shirika kwa Serikali pia umeongezeka kwa kiasi kikubwa.

“Shilingi bilioni 134.4 zimetolewa kama kodi katika kipindi cha miaka mitano, huku Shilingi bilioni 9.85 zikitolewa kama gawio,” anasema Hamad.

Kwa mujibu wa Hamad, mwaka wa fedha 2024/25, NHC imelipa gawio Shilingi bilioni 5.5 ambalo liliweka rekodi na kutambuliwa rasmi na Rais kama mojawapo ya mashirika ya umma yanayofanya vizuri zaidi.

Rais Samia Suluhu Hassan akikabidhi Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya NHC,Tuzo ya Kampuni Inayoongeza kwa Kasi Mchango wake Serikalini kwa uwiano wa miaka mitatu kati ya Sh bilioni moja hadi Sh bilioni 5.5 wakati wa hafla ya kukabihi Gawio kwa Serikali,Ikulu Dar es Salaam hivi karibuni. Kushoto ni Waziri wa Uwekezaji,Profesa Kitila Mkumbo na kulia ni Mkurugenzi Mkuu wa NHC, Hamad Abdallah.

“Kwenye ujenzi, NHC imejenga nyumba 5,399 zenye thamani ya Shilingi bilioni 659.5 kwa ajili ya kuuza na kupangisha. Kati ya hizo, nyumba 3,217 zimekamilika, huku 2,182 zikiwa katika hatua mbalimbali za ujenzi,” anasema.

Akitaja miradi mikubwa iliyotekelezwa na NHC ndani ya miaka mitano kuwa ni pamoja na Morocco Square, ambao umekamilika hivi karibuni, baada ya kuchelewa kwa miaka mingi, ikiwamo pia  miradi ya Kawe 711 na Golden Premier Residence ambayo imefufuliwa kutokana na ufadhili kutoka serikalini.

Mkurugenzi huyo wa NHC anasena shirika anloliongoza limekamilisha mikataba 67 ya kazi za umma, yenye thamani ya Shilingi bilioni 458.2, ikiwemo miradi ya kimkakati ya kitaifa kama vile Soko la Madini la Kimataifa la Tanzanite Mirerani, Kitengo cha Moyo cha JKCI Dar es Salaam na majengo ya ofisi za wizara mjini Dodoma.

“Kwa kushirikiana na sekta binafsi, NHC pia imeanzisha miradi ya ubia 21 yenye thamani ya Shilingi bilioni 351, inayoongeza upatikanaji wa nafasi za biashara na makazi nchini kote,” anasema Hamad.

Anabainisha kuwa mafanikio hayo ya NHC yametambuliwa ndani na nje ya nchi, ikiwamo kupata tuzo ya Mjenzi Bora wa Nyumba za Umma Afrika Mashariki, huku  pia shirika likipongezwa kwa viwango vyake bora vya uandaaji wa taarifa za fedha.

Hamad anaeleza kwamba kwa kupitia mpango wa ‘Nyumba za Samia’ unaolenga kujenga nyumba nafuu 5,000, na mpango wa ‘Nyumba Bond’ wa kuvutia uwekezaji wa umma, NHC inaelekea kuwa mhimili mkubwa wa kushughulikia changamoto ya uhaba wa makazi nchini.


Nyumba Bond

Katika mkutano huo na Wahariri wa Vyombo mbalimbali vya Habari, Hamad anatambulisha mpango wa ‘Nyumba Bond’, akieleza NHC inajiandaa kuzindua mpango huo mkubwa wa ukusanyaji mitaji kupitia uzinduzi wa ‘Nyumba Bond’.

Akifafanua Hamad anasema: “Dhamana hii ya nyumba, inalenga kukusanya fedha kutoka kwa wananchi na kuwawezesha Watanzania wa kipato cha aina zote kuwekeza moja kwa moja katika maendeleo ya makazi.”

Kwa mujibu wa Mkurugenzi Mkuu huyo wa NHC, dhamana hiyo itakuwa chombo muhimu katika kuongeza kasi ya upatikanaji wa makazi nafuu nchini, huku pia ikiwavutia wawekezaji kwa faida nzuri.

“Nyumba Bond itakuwa mfano wa kwanza wa aina yake Afrika Mashariki utakaotoa fursa kwa wananchi wa kawaida, mifuko ya hifadhi ya jamii, kampuni za bima na wawekezaji wa taasisi kuchangia moja kwa moja kwenye ajenda ya makazi ya kitaifa,” anasema Hamad.

Anasema kwa kutumia uwekezaji wa umma kwenye miradi mikubwa ya ujenzi, NHC inalenga kuziba pengo la makazi na kuchochea ukuaji jumuishi wa uchumi.

Hamad anaweka wazi kuwa tayari NHC imeanza mashauriano na mamlaka za udhibiti, washauri wa kifedha na wadau muhimu ili kukamilisha muundo wa dhamana hiyo.

Anasema kipaumbele kitatolewa kwa uwazi, ulinzi wa wawekezaji na kulingana na malengo ya muda mrefu ya maendeleo ya Taifa, akiainisha kwamba uzinduzi wa dhamana hiyo ya miaka saba, unatarajiwa kufanyika mwakani baada ya kupitishwa na Bodi ya NHC.

Wahariri wa Vyombo mbalimbali vya habari nchini, wakimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa NHC, katika mkutano wake na vyombo vya habari jijini Dar es Salaam, hivi karibuni.

Anabainisha kwamba fedha zitakazopatikana zitagharamia miradi kama vile ‘Nyumba za Samia’, miji ya pembeni (satellite cities), na kukamilisha majengo ya kimkakati mijini.

“Mara tu Nyumba Bond itakapoanza, itaongeza mtaji wa NHC na kuimarisha ushiriki wa wananchi katika maendeleo ya miundombinu. Huu ni mpango utakaoleta mageuzi makubwa katika namna tunavyofadhili nakubadili makazi Tanzania," anasema Mkurugenzi Mkuu.

Rais Samia na miradi ya NHC

Akizunguzia miradi mikubwa kadhaa ya NHC iliyoanza tena baada ya kusimama kwa karibu miaka minane, Hamad anarejea kumshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kuingilia kati na kufungua njia ya maendeleo akisema;

"Miradi hiyo ilisimama kwa sababu baadhi ya watendaji walishindwa kutekeleza majukumu yao. Lakini Rais Samia alipoingia madarakani, alifanya uamuzi jasiri wa kufufua miradi hii."

Miradi iliyochelewa na sasa inaendelea ni pamoja na ujenzi wa majengo ya kibiashara na makazi chini ya Morocco Square, Kawe 711 na Golden Premier Residence.

Mradi wa Morocco Square sasa umekamilika kikamilifu na shughuli zinaendelea. Kawe 711 uko kwenye ujenzi na unatarajiwa kukamilika ifikapo Aprili mwakani.

Hata hivyo, Golden Premier Residence bado uko hatua za awali baada ya kusimama kwa miaka minane.

Meneja Uhusiano na Habari wa NHC, Muungano Saguya (Mbele), akiwaongoza  wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari nchini kufanya ziara na kujionea miradi inayotekelezwa na NHC jijini Dar es Salaam, hivi karibuni. 

Kama Kawe 711, Golden Premier Residence pia upo Kawe, ambapo pia kuna mradi mwingine—Nyumba za Samia.

Hamad anasema kuchelewa kwa miradi hiyo kumesababisha kuongezeka kwa gharama kwa wateja wa NHC.

Hata hivyo, anakiri kuwa kuchelewa kulisababisha gharama kupanda, lakini shirika halikupata hasara.

“Kama biashara nyingine yoyote, tulipopata fursa ya kukamilisha miradi, tulirekebisha bajeti. Gharama za ziada zilihamishiwa kwa wateja waliokuwa wamenunua au kupangisha nyumba hizo,” anasema Abdallah.

Akitoa mfano wa Morocco Square, alisema kuwa kama mradi huo ungekamilika miaka minane iliyopita, gharama zingekuwa chini na wateja wangelipa kidogo.

Sehemu ya Jengo la Morocco Sqare linavyoonekana.

“Kwa mfano, badala ya mteja kulipa Shilingi milioni 300, sasa amelazimika kulipa Shilingi milioni 500,” alisema.

Hamad anahitimisha kuwa mafanikio hayo ya NHC yanatarajiwa kuchochea kukamilika kwa miradi mingine kama Kawe 711 na Golden Premier Residence, hivyo kuendeleza ajenda ya Serikali ya makazi na maendeleo ya miji.

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Sanamu ya Bikira Maria yaonekana ndani ya Hifadhi ya Taifa Saadani

Kapteni Traole afuata huduma za afya nchini

Wawekezaji wa Oman watua nchini, wateta na NHC kuchochea mapinduzi sekta ya makazi