Dk. Biteko afungua Karibu Kilifair 2025, aagiza matumizi ya TEHAMA kukuza utalii

 - Ataka Sekta Binafsi iendelee kuwekeza Sekta ya Utalii hasa huduma za malazi, kukidhi ongezeko la mahitaji ya soko

Exuperius Kachenje, daimatznews@gmail.com

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko ameiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii kutumia fursa za ukuaji wa sekta ya TEHAMA katika utangazaji utalii na upatikanaji wa masoko ya utalii sanjari na matumizi ya nishati safi na endelevu.

Wananchi wakiingia Viwanja vya Magereza, Kisongo kushuhudia Maonyesho ya Nane ya Utalii ya Karibu Kilifair kwa mwaka 2025 yanayofanyika kwa siku tatu,Juni 6 hadi 8,2025.
Aidha, amesema sekta ya utalii imeendelea kuwa na mchango mkubwa katika uhifadhi wa maliasili na malikale, ustawi wa jamii na ukuaji wa kiuchumi akibainisha kuwa takwimu zinaonesha, sekta hiyo inachangia asilimia 17.2 ya Pato Ghafi la Taifa (GDP) na asilimia 25 ya mauzo ya nje.

Dk. Biteko (Pichani chini),amesema hayo Juni 6, 2025 viwanja vya Magereza,Kisongo jijini Arusha wakati akimwakilisha Rais Dk. Samia Suluhu Hassan katika ufunguzi wa Maonesho ya Kimataifa ya Utalii ya Karibu -Kilifair 2025, yanayofanyika kuanzia Juni 5 hadi 7, 2025, yakiwa na kaulimbiu isemayo “Utalii Endelevu, Kujenga Ustahimilivu na Ubunifu”.

“Ninaiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii mambo matatu;… kutumia fursa za ukuaji wa sekta ya TEHAMA katika utangazaji utalii na upatikanaji wa masoko ya utalii sanjari namatumizi ya nishati safi na endelevu.” 

Dk. Biteko amesema kwa mwaka huu pekee, maonesho ya Karibu Kilifair yamekutanisha waoneshaji zaidi ya 500 kutoka Tanzania Bara, Zanzibar na zaidi ya nchi 10 duniani, wanunuzi wa kimataifa 1,000 kutoka mataifa zaidi ya 40 pamoja na maelfu ya wadau na wataalamu wa sekta ya utalii.

“Hii ni dhahiri kuwa, dunia inaiangalia Tanzania na Afrika Mashariki kuwa kitovu cha utalii. Tutumie fursa hii kutangaza vitu tulivyonavyo,” amesema Dk. Biteko.

Ameshauri pia badala ya kutangaza kwa kutumia majarida pekee, ishirikiane na mamlaka mbalimbali za Serikali na Sekta binafsi katika kuboresha mazingira ya biashara za utalii nchini ili kuchochea na kuvutia uwekezaji zaidi.

Katika  maagizo yake, Dk. Biteko pia ameiagiza wizara kuendelea kubuni njia mbalimbali za uendelezaji wa mazao ya utalii nchini kwa kuzingatia mgawanyiko wa aina ya mazao na mtawanyiko wa kijiografia wa nchi.

Kwa upande wa sekta binafsi,  Dk, Boteko ametoa rai iendelee kuwekeza katika sekta ya utalii hasa katika eneo la huduma za malazi, ili kukidhi ongezeko la mahitaji ya soko kwa kuzingatia uwepo wa matukio mbalimbali ya kimataifa yanayoendelea kufanyika nchini.

Amesema Serikali itaendelea kushirikiana nao katika nyanja mbalimbali ili kuhakikisha ustawi wa biashara za utalii nchini na maendeleo ya sekta kwa ujumla wake unanufaisha taifa, huku akiwataka Watanzania kuendelea kuwa wakarimu na kuelezea taswira nzuri ya nchi ili kuvutia wageni zaidi.

Kwa mujibu wa Dk. Biteko, maonesho ya utalii ya Karibu– Kilifair yanaendelea kukuwa kimataifa na kuwakutanisha wadau wa utalii kutoka maeneo mbalimbali duniani kwa lengo la kujadili fursa za biashara, kubadilishana uzoefu katika biashara za utalii na masoko pamoja na kuhamasisha uwekezaji kwenye sekta hiyo muhimu ya uchumi.

Amebainisha kuwa Serikali inatekeleza programu mbalimbali za kimkakati za utangazaji utalii, zikiwemo filamu za Tanzania - the Royal Tour na Amazing Tanzania, ambazo zimeleta mafanikio makubwa kwa nchi.

Dk. Biteko amesema Tanzania imeendelea kutambulika na kushinda tuzo mbalimbali ikiwemo tuzo maarufu duniani za World Travel Awards – WTA zinazotolewa na Taasisi ya World Luxury Media Group Limited ya nchini Uingereza ambazo pia ni chachu katika kuvutia watalii katika soko la kimataifa.

“Tuzo hii ni matokeo ya Tanzania ya kutangaza ubora wa vivutio vilivyopo nchini kama vile Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na Mlima Kilimanjaro kuwa mahali bora pa kutembelea barani Afrika kwa shughuli za utalii wa safari na maeneo mbalimbali ikiwemo Zanzibar. Pia, Tanzania imepewa hadhi ya kuwa mwenyeji wa Tuzo za World Travel Awards kwa Kanda ya Afrika zitakazotolewa mwezi huu Juni, 2025,” amesema Dk. Biteko.

Naibu Waziri Mkuu na Waziri wa Nishati, Dk. Doto Biteko(aliyevaa jaketi), akisikiliza maelezo ya mtumishi wa Wizara ya Maliasili na Utalii kuhusu utalii wa tiba ya kung'atwa na nyuki unaofanywa kwenye maonyesho hayo, iliyoelezwa tiba na kinga ya maradhi sugu.

Awali, akimkaribisha Naibu Waziri Mkuu kufungua maonyesho hayo ya nane ya maarufu Karibu Kili Fair 2025, Naibu Waziri wa Wizara ya Maliasili na Utalii,Dustan Kitandula amemshukuru Rais Samia Suluhu Hassan kwa uongozi wake wenye maono na kukuza sekta ya utalii nchini.

Kitandula amesema sekta ya utalii inakuwa kwa kasi duniani katika nchi mbalimbali mfano Tanzania ambapo kwa mwaka 2024 imeingiza mapato ya utalii dola za Marekani bilioni 3.9 pamoja na kupata watalii 5,360,247 huku watalii wa ndani wakiwa 3,218,352 na watalii wa nje wakiwa 2,218,352.

Amesema katika kuendelea kuimarisha sekta hiyo nchini, Serikali imeridhia kujenga ukumbi mkubwa wa kimataifa jijini Arusha kwa gharama ya shilingi bilioni 230.

Naibu Waziri Kitandula  ameongeza kuwa Wizara yake imeendelea kushirikiana na wadau ili kukuza biashara ya utalii nchini kwa kuwa na vikao na wadau hao ambapo imefanya maboresho ya sheria ya ada na tozo kwa lengo la kukuza sekta hiyo.

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. Paul Makonda amewapongeza waandaji wa maonesho hayo ya Karibu - Kilifair na kusema kuwa ni kichocheo kikubwa cha uchumi mkoani humo, aidha amewaomba waandaji kuongeza idadi ya siku za maonesho kufikia siku tano hadi saba.

Akizungumza kwenye maonyesho hayo,  Balozi wa Shirikisho la Ujerumani nchini, Thomas Terstegen amesema sekta ya utalii imesaidia kutoa ajira na kuongeza mapato nchini Tanzania na kwamba nchi yake itaendelea kuunga mkono jitihada mbalimbali za utalii katika nchi za Afrika Mashariki akieleza kuwa  kwa kushirikiana na EAC wamezindua kampeni inayoitwa Visit East Africa Feel the Vibe, inayolenga kusaidia watalii kutembelea nchi za Afrika Mashariki.

Naibu Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Andrea Murietha amesema kuwa Jumuiya hiyo imeendelea kufanya jitihada za kutangaza utalii kwa kufanya kazi karibu na nchi wanachama ili kuhakikisha manufaa ya utalii yanapatikama kwa usawa katika nchi hizo.

Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Waongoza Watalii Tanzania (TATO), Henry Kimambo ameishukuru Serikali kwa kuendelea kushirikiana na wadau wa sekta hiyo.

 “ Tunapokuwa na jambo kuhusu utalii tunasikilizwa kuanzia ngazi ya wilaya, mkoa hadi Taifa tunaishukuru sana Serikali kwa hili. Niiombe Serikali na wadau utalii kwa pamoja tuongeze nguvu katika maonesho haya ili siku moja tushindane na yale ya Afrika Kusini, tunaweza kufanya haya maonesho ya Karibu- Kilifair kuwa makubwa zaidi Afrika,” amesema Kimambo.

Awali, Dk. Biteko ametembelea mabanda mbalimbali ikiwemo Banda la Wizara ya Maliasili na Utalii ambalo limetangaza fursa mbalimbali za uhifadhi na utalii kwa ajili ya kuvutia watalii na wawekezaji wa ndani na nje.

Ametembelea pia Banda la Nishati (Energy Solutions) ambapo amejionea vifaa mbalimbali vinavyotumia nishati ya jua pamoja na banda la Hal linanalotengeneza magari ya kusafirisha watalii nayotumia umeme.

 

 

 

 

 

Maoni

Machapisho maarufu kutoka blogu hii

Sanamu ya Bikira Maria yaonekana ndani ya Hifadhi ya Taifa Saadani

Kapteni Traole afuata huduma za afya nchini

Wawekezaji wa Oman watua nchini, wateta na NHC kuchochea mapinduzi sekta ya makazi