Hot Posts

6/recent/ticker-posts

TEF 'walia' na Waziri Silaa

Exuperius Kachenje

Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), limeeleza kutoridhishwa kwake na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Jerry Silaa kushindwa kufika kwenye matukio ya wadau wa habari ikiwemo kufungua Mkutano Mkuu wa Nane wa jukwaa hilo unaofanyika Dar es Salaam.

Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile (Aliyesimama) akizungumza wakati wa Mkutano Mkuu wa Nane wa Jukwaa hilo unaofanyika Novemba 6 hadi 9, 2024 jijini Dar es Salaam.

Katika mkutano huo wa Novemba 6 hadi 9, 2024, Waziri Silaa amewakilishwa na Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Nicholaus Mkapa.

Kauli hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa TEF, Deodatus Balile alipokuwa akizungumza kwenye ufunguzi wa mkutano huo leo Novemba 7, 2024 katika ukumbi wa NSSF Mafao House, Ilala Dar es Salaam,uliobeba kauli mbiu; "Weledi kwa Uhimilivu wa Vyombo vya Habari."

"Sisi Wahariri hatufurahishwi na hatuwezi kuficha jambo hili, hatufurahishwi na Waziri wa Habari, Mawasiliano, na Teknolojia ya Habari Jerry Silaa," amesema Balile na kufafanua:

 "Alialikwa kwenye Mkutano wa PST Arusha hakwenda, aliakiwa kwenye Tuzo za Waandishi wa Habari hakwenda, alialikwa Mbeya kwenye tukio la Wadau wa Habari hakwenda na sasa Mkutano Mkuu wa Jukwaa la Wahariri hakuja.  Hali hii inaonesha kuwa Waziri wetu hayupo tayari kushirikiana na Wadau wa Tasnia ya Habari."

Balile amesema kwenye matukio ya aina hiyo ndiyo jukwaa sahihi kwa wadau kukutana na Waziri na kuzungumza kwa pamoja masuala muhimu yanayohusu mustakabali wa Tasnia ya Habari, lakini inasikitisha kuwa Waziri hayupo tayari kwa ushirikiano.

Huku akikumbuka tukio la aliyekuwa Waziri wa Habari enzi hizo Ramadhan Mapuri habari zake kususiwa kuandikwa na vyombo vya habari, Balile ameongeza kuwa wakati wa Waziri Nape Nnauye kwenye Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, wakati wowote alikuwa mstari wa mbele kwa muda wowote kuhudhuria matukio mahimu ya wadau wa Tasnia ya Habari na ushirikiano huo ulikuwa na tija kubwa kwenye tasnia.

"...Mfikishie salam, Waziri wa Habari kondoo wake ni vyombo vya habari, sisi tupo tayari kushirikiana na Serikali," amesema Balile akiomuomba Mkapa.

Hata hivyo, Mwenyekiti huyo waTEF amemwomba waziri huyo kuwaambia mawaziri wengine wawe  na utaratibu wa  kukutana na wahariri wa vyombo  vya habari ili kuzungumza masuala mbalimabali ya kitaifa kwa maslahi ya Tanzania.

"Rais ameshakutana na wahariri mara mbili, Waziri Mkuu amefanya hivyo mara tatu,Naibu Waziri Mkuu ameshafanya hivyo, pia Rais wa Zanzibar (Dk. Hussein  Mwinyi), ameshakutana na wahariri," amesema Balile.

 Akifungua  mkutano huo kwa niaba ya  Waziri Silaa, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Nicholas Mkapa, amesema Waziri wake ametingwa na majukumu mengine ya Wizara na hivyo amemtuma yeye kumwakilisha.

Amesema wizara inaendelea kufanyia kazi madai mbalimbali ya wanahabari  ikiwamo kuboresha sera na sheria zinazogusa  utendaji wa vyombo vya habari nchini.

Wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari wanachama wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), wakifuatilia Mkutano wao Mkuu wa Nane wa Mwaka ukumbi wa NSSF, Mafao House Dar es Salaam.

Akizungumzia Uchaguzi wa Serikali za Mitaa unaotarajiwa kufanyika  baadae mwezi huu na Uchaguzi Mkuu mwaka ujao,Mkapa amesema matukio hayo yatakuwa ni kipimo muhimu cha weledi kwa vyombo vya habari na wahariri.

"Hakikisheni mnasimamia na kutimiza sheria na misingi ya utoaji habari," amesema.    

Awali, akizungumza kabla ya mgeni rasmi, Mkuu wa Wilaya ya Ilala, Edward Mpogolo ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Albert Chalamila, ameishukuruTEF kwa kuiunga mkono Serikali katika masuala mbali mbali ya maendeleo ya taifa.

 

 

 

Chapisha Maoni

0 Maoni