Hot Posts

6/recent/ticker-posts

Rais Dk. Samia kufungua kongamano STICE2024

 Kuzindua Mfuko Mikopo Nafuu 

Exuperius Kachenje, daimatznews@gmail.com

Rais Dk, Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuwa mgeni rasmi na kufungua Kongamano na Maonesho ya Tisa ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (STICE2024), ambapo pia atazindua Mfuko wa Mikopo Nafuu na kutoa fedha kwa watafiti.

Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH Dk, Amos Nungu

Akizungumza katika kikao kazi na Wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari nchini jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi Mkuu wa COSTECH, Dk. Amos Muhunda Nungu amesema Rais atafungua kongamano hilo Desemba 2, 2024 ukumbi wa Mwalimu Julius Nyerere (JNICC) jijini humo.

“Tutaanza na Shilingi Bilioni 2.3 za kuwakopesha watafiti waliokidhi vigezo kutokana na maandikowaliyoleta COSTECH, Rais atazindua mfuko huo. Fedha hizo ni kwa kuanzia, tutaendelea kupata fedha kwa wadau na Serikali,” amesema Dk Amos na kufafanua;

“Kauli mbiu ya Kongamano kwa mwaka huu ni; Matumizi ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu katika Kuhimili Mabadiliko ya Tabianchi na Maendeleo ya Uchumi.”

Dk. Nungu amesema kongamano hilo litafanyika hadi Desemba4,2024 likijumuisha wabunifu, watafiti, wajasiriamali na watunga sera.

Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, licha ya kuwepo changamoto mbalimbali zikiwemo za afya na mazingira, COSTECH ina mengi ya kujivunia kuwashika mkono vijana  wenye maono katika ubunifu na utafiti kwa kuwasaidia kifedha, kuwaunganisha na taasisi mbalimbali za usaidizi pia zile za kimataifa.

Viongozi wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) waliosimama mbele pamoja na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF),Deodatus Balile ( wapili kulia) wakifuatilia matangazo ya washindi wa tuzo za waandishi bora wa sayansi na teknolojia baada  ya mkutano  na wahariri wa vyombo vya habari kwenye ukumbi wa ofisi wa tume hiyo Dar es Salaam Novemba 22,2024.

“Tunao mwongozo wa kitaifa ubunifu, tunaufuata, tunawasaidia vijana wetu wabunifu na watafiti. Fedha za utafiti tunazotumia zinatolewa na Serikali, pia wafadhili. Tunaamini Mfuko wa Mikopo Nafuu ukishazinduliwa pesa zitaongezeka, lakini pia utakuwa wa uwazi, waombaji watahojiwa,” amesema Dk Amos.

 Akizungumza katika mkutano huo,Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Deodatus Balile, ameipongeza COSTECH na kuishauri ijifikirie zaidi katika kuboresha eneo lao liwe lakisasa zaidi.

Mwenyekiti wa Bodi ya Makamishna wa COSTECH, Profesa Makenya Maboko, amesema wamepokea wazo hilo na kwamba watajenga majengo ya kisasa Dar es Salaam na Dodoma. 

Amewaomba wahariri wa vyombo vya Habari kusaidia kusukuma mbele ajenda ya sayansi, teknolojia na ubunifu. 

" Imarisheni ushirikiano naCOSTECH ili kuhakikisha taarifa za sayansi, teknolojia na ubunifu zinaifikia jamii kwa ufanisi,"amesema.

Chapisha Maoni

0 Maoni