Hot Posts

6/recent/ticker-posts

Serikali yatoa msimamo Sekta ya Posta Afrika

Mwandishi Wetu, WHMTH, Arusha

Serikali ya Tanzania imeuhakikishia Umoja wa Posta Afrika (PAPU), msimamo wake usioyumba kwamba, itaendelea kuunga mkono na kusaidia mikakati ya umoja huo kwa maendeleo ya Sekta ya Posta Afrika.

Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Maryprisca Mahundi (Mb), akihutubia Mkutano wa 42 wa Baraza la Utawala la PAPU, makao makuu ya umoja huo jijini Arusha, leo Juni 11,2024.

Msimamo huo wa Serikali umetolewa leo Juni 11, 2024 na Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Maryprisca Mahundi (Mb), wakati akihutubia Mkutano wa 42 wa Baraza la Utawala la PAPU, unaofanyika makao makuu ya umoja huo jijini Arusha.

"Kwa heshima kubwa, napenda kuthibitisha msimamo usioyumba wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika kusaidia mipango mbalimbali ya PAPU," amesema Mhandisi Mahundi aliyekuwa mgeni rasmi wa mkutano huo.

Mhandisi Mahundi ameutaka mkutano huo wa PAPU, kutafakari njia zitakazowezesha mageuzi ya posta Afrika, ili kuendana na maendeleo ya kasi ya biashara mtandao (e-commerce), pamoja na mabadiliko makubwa ya teknolojia ya mawasiliano na dijitali.

Wajumbe wa Mkutano wa 42 wa Baraza la Utawala la PAPU, wakifuatilia hotuba ya ufunguzi iliyotolewa leo Juni 11, 2024 na Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Maryprisca Mahundi. Mkutano huo, unaofanyika jijini Arusha.

Naibu Waziri huyo amesisitiza kwamba barani Afrika, posta inafanya kazi kubwa ya kutoa huduma za kuaminika, uhakika na zenye tija kwa biashara kubwa, ndogo na za kati (MSMEs).

“Ni vizuri kwamba wakati dirisha la biashara mtandao likiwa limefunguka na kuja na fursa zaidi, tayari baadhi ya Posta Afrika zimeanza kujishughulisha na kutoa huduma mbalimbali katika mnyororo wa biashara mtandao,” amesema Maryprisca Mahundi.

Amesema, bado kila mtu anakumbuka matukio ya Septemba 3 mwaka uliopita, liliposhuhudiwa tukio la kihistoria la uzinduzi wa Jengo la Makao Makuu ya Ofisi za PAPU jijini Arusha, uliofanywa na Rais, Dk. Samia Suluhu Hassan.

Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Maryprisca Mahundi (Katikati), akishuhudia tukio la Katibu Mkuu wa Umoja wa Posta Afrika (PAPU) Dk. Sifundo Chief Moyo (kushoto) kupokea kompyuta 60 na Kamera ya Video kwa ajili ya Kituo cha Umahiri cha Huduma za Posta Kidijitali kutoka kwa wawakilishi wa Umoja wa Posta Duniani (UPU) na Shirika la Posta Ufaransa.

Amebainisha kuwa tukio hilo la kihistoria la nembo hiyo ni kielelezo na uthibitisho wa uhakika wa uongozi wa dhati na wenye maono wa viongozi wa Tanzania kuhusu mikakati na malengo ya PAPU.

Kwa mujibu wa Naibu Waziri huyo, uzinduzi wa PAPU Tower ni alama ya juhudi za pamoja za nchi wanachama wa umoja huo katika kuendeleza ugunduzi, kuimarisha mawasiliano na kukuza maendeleo katika eneo lote la Afrika.         

Mkutano huo wa Baraza la Utawala la PAPU, unatarajiwa kujadili maazimio na taarifa za vikao vya Kamati za Wataalam wa masuala ya posta vilivyoanza Juni 03 hadi 7, 2024, kujadili masuala mbalimbali yanayohusu Fedha na Utawala, Sera na Kanuni, Uendeshaji na Teknolojia pamoja na Mikakati.

Wajumbe wa Tanzania katika Mkutano wa 42 wa Baraza la Utawala la PAPU, wakifuatilia hotuba ya ufunguzi ya Naibu Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhandisi Maryprisca Mahundi, iliyotolewa leo jijini Arusha, unapofanyika mkutano huo.

Awali, akimkaribisha mgeni rasmi, Naibu Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Nicholaus Merinyo Mkapa, amesema udhibiti madhubuti wa maafa na hatari ni muhimu katika ulimwengu wa leo, hivyo Sekta ya Posta lazima iwe thabiti na tayari kukabiliana na majanga ya asili, vitisho vya mtandao na hatari zingine.

Mkapa amesema  hatua hiyo inahusisha kuandaa mipango ya kina ya udhibiti wa maafa na hatari, kuwekeza katika miundombinu salama na kutoa mafunzo kwa wafanyakazi ili kushughulikia dharura kwa ufanisi.

Amesema mfumo thabiti wa Sera ya Posta ni muhimu kwa ajili ya kuongoza sera za mahitaji ya sekta zinazokuza uvumbuzi, ushindani na maendeleo.

Chapisha Maoni

0 Maoni