Hot Posts

6/recent/ticker-posts

Bilionea Rostam Aziz aigeukia Zambia

 -Amwaga mabilioni ya fedha


Mwandishi Wetu, daimatz@gmail.com


Bilionea Mtanzania, Rostam Aziz ametangaza kutanua uwekezaji wake kwa kufanya uwekezaji mpya, safari hii akiwekeza nchini Zambia kiasi cha Dola za Marekani milioni 100 katika sekta ya nishati na madini.

Rostam ambaye pia ni Mwenyekiti wa kampuni za Taifa Group inayofanya kazi ukanda wa Afrika Mashariki amefanya uamuzi wa kuwekeza fedha hizo, sawa na takriban shilingi bilioni 250, unaoashiria kuwa na mkakati wa kupanua zaidi wigo wa uwekezaji wake kwenye ukanda wa kusini mwa Afrika.

Rais Dk. Samia Suluhu Hassan(kushoto) akishuhudia Mfanyabiashara Rostam Aziz, akitia saini moja ya mikataba ya kibiashara katika moja ya ziara za Rais nje ya nchi.


Kwa mujibu wa taarifa zilizochapishwa na Mtandao wa billionaires.africa za hivi karibuni, Rostam  anayetajwa kumiliki utajiri mkubwa barani Afrika, tayari amekutana na Rais wa Zambia, Hakainde Hichilema, Oktoba 20 mwaka huu 2023, ambapo walijadili kuhusu maeneo yenye fursa na vivutio vya uwekezaji kwenye sekta ya nishati na madini nchini humo.

Mkutano huo unatajwa kuchagiza hatua zaidi katika kukuza ushirikiano wa kiuchumi kati ya Tanzania na Zambia.

Taarifa hizo mpya za uwekezaji nchini Zambia zinafuatia taarifa za takriban miezi mitano iliyopita, zilizoitaja Kampuni ya Taifa Gas, kueleza mkakati wake wa kutaka kuwekeza katika uzalishaji umeme nchini Zambia, mradi uliotajwa pia kugharimu Dola za Marekani milioni 100 (sh bilioni 250).

 

Mradi huo wa umeme unaelezwa utaimarisha uwepo wa kampuni ya Taifa Gas kusini mwa Afrika ukiimarisha pia mtandao wa biashara na kuongeza fursa kibiashara baina na Tanzania na Zambia.


Akizungumzia uwekezaji huo, Rostam alikaririwa akieleza kuwa Zambia ni eneo linalovutia kwa uwekezaji zaidi na kwamba Taifa Gas itahakikisha uhusiano kati ya Zambia na Tanzania unazidi kukua na kuendeleza fursa za uwekezaji katika nishati na madini.

“Tutahakikisha Tanzania na  Zambia zinakuza uhusiano na moyo wa ushirikiano kwa maendeleo endelevu ya nchi hizo jirani, ninafurahi kwamba tayari tuna mshirika ndani ya Zambia, nasi kama Taifa Gas tutatumia vizuri fursa hii ya uwekezaji kwa maslahi ya nchi zetu mbili za Afrika,” amesema Rostam.

Bilionea huyo mwenye umri wa miaka 58, amesema anaheshimu mwaliko wa Rais wa Zambia, akitoa wito kwa wawekezaji wengine barani Afrika kuwekeza mitaji Zambia, huku akiahidi kuongeza wigo wa uwekezaji nchini humo na kwamba uwekezaji wake ni wa ushirikiano na mwekezaji raia wa nchi hiiyo.

Rostam alitambuliwa kuwa Mtanzania wa kwanza kumiliki utajiri unaofikia Dola bilioni na mtandao wa Forbes, mwaka 2013, kutokana na biashara na uwekezaji mbalimbali ikiwamo katika kampuni za simu, usafiri wa anga, nishati, madini, gesi na sekta ya nyumba.

 

 

Chapisha Maoni

0 Maoni