Hot Posts

6/recent/ticker-posts

Namba zinaipaisha MSD

-Mapato yaongezeka, ufanisi wapaa 

Exuperius Kachenje, daimatznews@gmail.com

Namba zinaipaisha Bohari ya Dawa nchini (MSD), ndivyo unavyoweza kueleza, baada taasisi hiyo kupata mafanikio makubwa katika utendaji wake kwa mwaka 2023.

MSD imetangaza ongezeko la shilingi bilioni 52 katika mapato yake, sanjari na upatikanaji dawa kuongezeka kutoka asilimia 57 kwa mwaka 2022 hadi asilimia 81 kufikia Juni mwaka 2023

 Taasisi hiyo ya Serikali iliyo chini ya Wizara ya Afya, iliyoanzishwa mwaka 1993, pia imetangaza kuongezeka kwa upatikanaji wa bidhaa za afya kutoka asilimia 51, Juni 2022 hadi kufikia asilimia 64 Juni 2023.

Akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari leo jijiniDar es Salaam, chini ya uratibu wa Ofisi ya Msajili wa Hazina, Mkurugenzi Mkuu wa MSD, Mavere Tukai amebainisha hayo akitaja majukumu na muundo wa bohari hiyo, pia kubainisha ongezeko la mapato yake kwa usambazaji kufikia shilingi bilioni 372.4 mwaka huu kutoka shilingi bilioni 320.9 mwaka 2022.

Mkurugenzi Mkuu wa Bohari ya Dawa nchini (MSD), Mavere Tukai, akitoa taarifa ya utendaji, mafanikio na uelekeo wa MSD mbele ya Wahariri wa Vyombo vya Habari jijini Dar es Salaam,  Septemba 27,2023.

“MSD ina majukumu manne nayo ni uzalishaji, ununuzi, utunzaji na usambazaji, dhamira kubwa ikiwa kuhakikisha upatikanaji wa bidhaa za afya katika vituo vya kutolea huduma za afya,” amesema Tukai wakati akitoa taarifa ya utendaji, mafanikio na uelekeo wa MSD na kuongeza:

“MSD ina watumishi 688,magari 185 ya usambazaji, vituo vinavyohudumiwa  zaidi ya 7,600, viwanda vya kuzalisha bidhaa za afya viwili, mizunguko ya usambazaji 6 na kanda 10.”

Kwa mujibu wa mkurugenzi huyo, katika mwezi Agosti mwaka huu MSD ililenga kukusanya mapato ya shilingi bilioni 35.68, hata hivyo makusanyo halisi ni shilingi bilioni 34.08.

Akitaja mafanikio mengine mbele ya Wahariri, Tukai amesema MSD imefanikiwa kuanzisha kitengo malum cha usimamizi na ufuatiliaji wa mikataba, kuongezeka wa ununuzi wa bidhaa za afya kutoka kwa wazalishaji wa ndani kutoka shilingi bilioni 14.1 mwaka 2021/2022 hadi kufikia shilingi bilioni 39.77.

Baadhi ya Wahariri wa Vyombo vya habari mbalimbali, wakifuatilia mkutano wao na Mkurugenzi wa MSD, Mavere Tukai (Hayupo pichani)chini ya Ofisi ya Msajili wa Hazina, uliofanyika Septemba 27, 2023, jijini Dar es Salaam.

“Tumeongeza zaidi mikataba ya muda mrefu kutoka mikataba 100 yenye bidhaa za afya kwa mwaka wa fedha 2021/22 hadi kufikia mikataba 233 yenye bidhaa 2,209 kwa mwaka 2022/23,” amefafanua Tukai.

Katika hatua nyingine, Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), limeipongeza MSD kwa kuvitumia viwanda vya ndani kufanikisha kazi zake, badala ya kuegemea viwanda vya nje, huku ikimpongeza Msajili wa Hazina kwa kuweka utaratibu wa taasisi zilizo chini yake kukutana na vyombo vya habari. 

Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa TEF, Deodatus Balile wakati wa mkutano huo akieleza kuwa kufanya kazi na viwanda vya ndani vinavyozalisha bidhaa za afya ni jambo zuri linalofaa kupigiwa mfano.

"Kutumia viwanda vya ndani inasaidia kupunguza gharama hivyo kuinua uchumi wa taifa. MSD imeonesha mwelekeo mzuri katika kujali afya za watanzania kwa kuhakikisha dawa hata vitendea kazi vinapatikana," amesema Balile.

Mkuu wa Kitengo cha habari na Mawasiliano Ofisi ya Msajili wa Hazina, Erick Anthon Mkuti, (Kushoto), na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), katika mkutano wa MSD na Wahariri, Septemba 23, 2023 jijini Dar es Salaam. 


Kuhusu Msajili wa Hazina, Balile amesema: " Nampongeza ndugu yetu Nehemia Mchechu na timu yake, kwa kuanzisha utaratibu wa taasisi zilizo chini yake kukutana na wahariri na kueleza kazi zao. Hii itasaidia  wananchi kuzifahamu vizuri taasisi hizo na majukumu yake."


 

 

Chapisha Maoni

0 Maoni