Hot Posts

6/recent/ticker-posts

BRELA, TAKUKURU 'zafunga ndoa' kukabili rushwa

 

-BRELA yapokea barua 120 za  TAKUKURU kwa mwezi

-Ni zinazohitaji taarifa za kampuni

-Zimo za kuwaita maofisa BRELA mahakamani

 Exuperius Kachenje, daimatz@gmail.com

Wakati mwaka 2023 ukielekea ukingoni Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), imeongeza kasi katika utendaji wake, ikilenga kuboresha utendaji na utoaji huduma zake kwa wananchi, lakini zaidi safari hii ikilenga kukuza ushirikiano kiutendaji kunakoondoa maswali kuhusu taarifa za usajili wa kampuni mbalimbali.

 Hii ni kutokana na ukweli kwamba kila mwezi BRELA hupokea takriban barua 120 kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) zinazohitaji taarifa za usajili wa kampuni, lakini pia maofisa wa BRELA wamekuwa wakiitwa mara kwa mara TAKUKURU kwa ajili ya mahojiano kuhusu masuala yanayohusu usajili wa kampuni.  

 Ukweli huo wa BRELA kupokea barua kwa wingi kutoka TAKUKURU zikihtaji taarifa za usajili wa kampuni mbalimbali kuiwezesha mamlaka hiyo ya Serikali kutekeleza majukumu yake katika kuzuia na kupambana na rushwa, unawekwa wazi na Ofisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Godfrey Nyaisa anayesema:

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Godfrey Nyaisa(kulia) na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Kamishna wa Polisi,  Salum Rashid Hamduni(kushoto), wakitia saini makubaliano ya ushirikiano (MOU), baina ya taasisi hizo katika hafla iliyofanyika Ofisi za  BRELA jijini, Dar es Salaam..

 “Katika utekelezaji wa majukumu ya kila siku, BRELA imekuwa ikipokea barua si chini ya sita (6) kwa siku kutoka TAKUKURU, zinazohitaji taarifa za usajili wa kampuni mbalimbali.”

Idadi hiyo ya barua sita kwa siku ikizidishwa mara tano ambazo ni siku za kazi za kiserikali, Jumatatu hadi Ijumaa, zinafikia barua 30 kwa wiki na zikizidishwa kwa wiki nne za mwezi ni sawa na barua 120. 

Kwa mujibu wa Nyaisa, BRELA pia ikipokea wito mara nyingi kutoka TAKUKURU, ikiwahitaji maofisa wa BRELA kwa ajili ya mahojiano kuhusu kampuni mbalimbali zilizosajiliwa na BRELA. 

Hatua hiyo ya TAKUKURU ni sehemu ya utekelezaji wa majukumu yake kwa mamlaka iliyonayo kuzuia na kupambana na rushwa nchini, inayotajwa kuhususisha maeneo mbalimbali zikiwamo kampuni ambazo kisheria husajiliwa na BRELA.

TAKUKURU hufanya hivyo kutokana na taarifa mbalimbali inazozipata au kupokea kutoka kwa wananchi na wadau mbalimbali zikiwamo taasisi za umma na binafsi kuhusu uwepo wa rushwa kwenye kampuni au baadhi ya watendaji wa BRELA kuhusishwa kwenye vitendo vya rushwa vinavyohitaji uchunguzi. 

Hata hivyo, kwa kutambua umuhimu wa kuboresha utendaji kazi wa wakala hiyo ya usajili wa kampuni pamoja na kukuza ushirikiano na tija na mamlaka nyingine za kiserikali ikiwemo TAKUKURU, Ofisa Mtendaji Mkuu wa BRELA anaweka wazi kuwa sasa wamepata dawa ya changamoto hiyo. 

Kwa mujibu Nyaisa dawa hiyo ni ‘kufunga ndoa’ kwa kuingia makubaliano ya utendaji kazi kwa pamoja na TAKUKURU, hali inayoashiria kwamba sasa TAKUKURU imepiga hodi na kupewa makazi ya kudumu ndani ya BRELA ili kuzuia na kupambana na rushwa katika utendaji wa wakala hiyo, lakini zaidi kusaidia kuharakisha kazi za uchunguzi wa TAKUKURU zinazohusu usajili wa kampuni na taarifa za umiliki wa kampuni. 

Nyaisa anasema kuwa tayari BRELA na TAKUKURU, zimesaini hati ya makubaliano ya utendaji kazi kwa pamoja lengo likiwa kurahisisha na kuharakisha taratibu mbalimbali za kiuchunguzi, bila kuathiri mamlaka na mipaka ya kiutendaji kati ya BRELA na TAKUKURU. 

Desemba 7, 2023 ndiyo siku ambayo itakumbukwa zaidi na BRELA kwa upande mmoja na wa pili TAKUKURU, kwani ulishuhudiwa utiaji saini ya hati ya makubaliano ya utendaji kazi kwa pamoja kati ya BRELA na TAKUKURU jijini Dar es Salaam mbele ya waandishi wa habari.

Katika hafla hiyo Ofisa Mtendaji Mkuu wa BRELA, Godfrey Nyaisa aliiongoza timu ya wakala hiyo, huku  Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Kamishna wa Polisi, Salum Hamduni naye akiiongoza timu ya watendaji wake katika ofisi ya Makao Makuu ya BRELA na kusaini makubaliano hayo ambayo kimsingi ni chachu ya kuongeza ufanisi kawenye utendaji wa taasisi hizo za serikali. 

Katika hafla hiyo, Nyaisa amesema: “Makubaliano haya yanalenga kuona uchunguzi unaenda kwa wakati na kuhakikisha TAKUKURU wanapata taarifa sahihi, mahiri kwa wakati huku tukibainisha changamoto zilizopo katika utendaji kazi, baina ya BRELA na TAKUKURU na kupendekeza kwa pamoja ufumbuzi wake.”

 Nyaisa anaongeza akisisitiza: “ Kwa siku BRELA imekuwa ikipokea barua si chini ya sita kutoka TAKUKURU zinazohitaji taarifa za usajili wa kampuni mbalimbali, pia tumekuwa tukipokea wito mbalimbali zinazowahitaji moafisa wa BRELA kwa ajili ya mahojiano TAKUKURU pamoja na kwenda mahakamani kushuhudia taarifa za kumbukumbu hizo.”

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Godfrey Nyaisa(Kulia) na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Kamishna Salum Rashid Hamduni wakikabidhiana hati ya makubalino ya ushirikiano (MOU), kwa taasisi hizo, baada ya kuzisaini jijini, Dar es Salaam. 

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU, Kamishna Salum Hamduni anaeleza: “Mkataba huu unalenga kutia nguvu na kurasimisha ushirikiano wa taasisi mbili kwa maeneo yaliyokubaliwa na pande zote ambazo ni kubadilishana taarifa za kiuchunguzi.”

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo wa TAKUKURU lengo lao kuu ni kupata ushahidi utakowezesha kuwafikisha watuhumiwa mahakamani, kuimarisha mfumo na utaratibu wa mafunzo kwa watumishi wa BRELA kuhusu dhana ya rushwa, madhara yake na namna watumishi hao wanavyoweza kupambana na rushwa ndani ya BRELA.

Anataja lengo jingine kuwa ni kushirikiana katika kufanya utafiti na tathmini ya mifumo ya kiutendaji ndani ya BRELA kwa lengo la kubaini na kuziba mianya ya rushwa ndani ya wakala hiyo.

“Kwa kutambua kuwa rushwa ni adui wa haki, utawala wa sheria, demokrasia na maendeleo, Serikali imedhamiria kupambana na tatizo la rushwa kwa nguvu zote,” anasema Hamduni. 

Anabainisha kuwa kwa kutambua kuwa mapambano dhidi ya rushwa hayawezi kufanikiwa bila ushiriki wa wadau, TAKUKURU kwa kuzingatia matakwa ya Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Sura ya 329, imekuwa ikishirikisha wadau kwa namna mbalimbali ikiwemo kuingia nao mikataba ya ushirikiano

“ TAKUKURU itauzingatia mkataba huu kuwa moja ya nyenzo muhimu katika kuifikia ndoto ya taasisi kuwa na Tanzania isiyokuwa na rushwa, kama ambavyo inavyobainishwa katika Mpango Mkakati wa TAKUKURU wa Mwaka 2022/23 – 2025/26,” anasema Kamishna Hamduni. 

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Godfrey Nyaisa (mbele kulia) na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Kamishna wa Polisi, Salum Rashid Hamduni (mbele kushoto), wakiwa na watendaji mbalimbali wa taasisi hizo  wakati wa hafla ya utiaji saini makubaliano ya ushirikiano  (MOU) baina ya taasisi hizo yaliyofanyika katika  Ofisi za  BRELA  jijini Dar es Salaam, Desemba 7,2023

Ikumbukwe kuwa Julai 8 hadi 9, 2022 BRELA na TAKUKURU zilifanya kikao kazi cha pamoja mkoani Morogoro kilicholenga kupeana elimu ya kiutendaji ili kuleta uhusiano wenye tija katika kutimiza majukumu ya pande hizo na kupeana taarifa mbalimbali kwa kuzingatia taratibu, kanuni na sheria.

 Kikao hicho kilibaini umuhimu kwa taasisi hizo kuanzisha utaratibu wa kuwa na vikao vya pamoja,  lengo likiwa kuelimishana kuhusu utendaji kazi na majukumu ya pande hizo.

Pia ulilenga kuleta mafanikio na maboresho katika utendaji kaz, kipekee katika usajili wa kampuni na biashara, utunzaji wa rekodi na taratibu za kufuata baada ya usajili, kubadilishana uzoefu pamoja na kubainisha changamoto ili kuzitafutia ufumbuzi wa pamoja kwa manufaa ya BRELA na TAKUKURU.

Chapisha Maoni

0 Maoni