Hot Posts

6/recent/ticker-posts

Birthday za wanawake zawadi kupima saratani

 -Waziri Ummy Mwalimu ashauri

-Asema asilimia 50 saratani inatesa wanawake

-Kila miaka 10 ongezeko asilimia 50

Exuperius Kachenje, daimatznews@gmail.com

Waziri wa Afya, Ummy Mwalimu amewataka wanawake wote wanaofikia umri wa miaka 30 kusherehekea siku zao za kuzaliwa kwa kujipa zawadi ya kupima saratani ya matiti na mlango wa kizazi.

Akizungumza leo Oktoba 21,2023, alipokuwa mgeni rasmi kwenye matembezi ya  kuadhimisha Mwezi wa Kampeni ya Elimu Kuhusu Saratani ya Matiti, pamoja na miaka 60 ya uwepo wa Ubalozi wa Sweden nchini katika Viwanja vya Ocean Road, jijini Dar es Salaam, Waziri Ummy amesema takwimu zinaonyesha saratani inaongezeka kwa asilimia 50 kila baada ya miaka 10.

“Kila mwanamke anayetimiza miaka 30 katika kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwake, zawadi ya kwanza ujipe mwenyewe, uwe umepima saratani ya matiti na saratani ya mlango wa kizazi. Ukifikia miaka 40 walau upime saratani kila baada ya miaka miwili,” amesema Ummy na kuongeza:

“Takwimu za Wizara ya Afya zinaonyesha katika kila vifo vitatu vinavyotokea, kimoja kimetokana na saratani, si hivyo tu bali pia asilimia 50 ya wagonjwa wa saratani ni wanawake.”

Waziri wa Afya, Ummy Mwalim (katikati) akiwa na Balozi wa Sweden nchini, Charlota Ozaki (kulia), kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa Asasi ya Shujaa Cancer Foundation, Glory Kida baada ya matembezi kuadhimisha Mwezi wa Elimu ya Saratani ya Matiti na miaka 60 ya ubalozi wa Sweden nchini.

Katika hotuba yake hiyo, Waziri Ummy amewaagiza watendaji ndani ya  wizara yake kutayarisha mwongozo kwa lengo la kusaidia kuwezesha kila mwanamke aliye na umri wa kuanzia miaka 30 atakapoenda hospitali kwa ugonjwa wowote, kufanyiwa pia vipimo vya saratani ya matiti na mlango wa kizazi.

“Watendaji waandae mwongozo, mwanamke yeyote aliye na umri wa miaka 30, anayekwenda hospitali, iwe ni wajibu wa daktari kumwelekeza au kumuelimisha mwanamke huyo kufanya uchunguzi, kupima saratani ya matiti na mlango wa kizazi. Iwe amekwenda hospitali na mafua, au mguu, mradi mwanamke apimwe saratani ya matiti, hata mlango wa kizazi,” amesema Waziri Ummy

Ummy pia amepiga marufuku wagonjwa wa saratani kurudishwa nyumbani kwa sababu ya kukosa fedha za kugharamia matibabu.

Waziri ametoa agizo hilo baada ya hali hiyo kuibuliwa na Jenister Mselu, mmoja wa mashujaa wa saratani wakati akitoa ushuhuda.

 Waziri wa Afya, Ummy Mwalim (mwenye kilemba) akiserebuka na Msanii Fina baada ya matembezi kuadhimisha Mwezi wa Elimu ya Saratani ya Matiti na miaka 60 ya ubalozi wa Sweden nchini.

“Ni marufuku kurudisha mgonjwa wa saratani nyumbani asipoweza kujilipia gharama. Serikali inatoa Sh. bilioni 6 kila mwaka ili kusaidia wagonjwa wa aina hiyo, kila mwaka tunapata visa vipya 42,000 lakini wanaofika hospitali ni 16,000 tu, nadhani hapo tunaweza kusaidia asilimia 50.”

Naye Asia Sima, shujaa mwingine wa saratani aliyeishi na ugonjwa huo kwa miaka 3, alielezea jinsi wahudumu wa afya (vijana) walivyompa majibu ya vipimo kuwa amegundulika na saratani, bila kumpa ushauri nasaha, hali iliyomfanya kuingiwa na hofu hata kutaka kujiua.

“Niliona wakata sanda, niliona wachangisha michango, niliwaza ntaziwa dar es Salaam au mkoani hata nikapanda ghorofa ya pili hapa Ocean Road kutaka kujiua, nilichanganyikiwa, nikaanza kukimbia wakanikamatia kule getini,” amesimulia Asia.

 Masimulizi hayo ya Asia yakamsukuma Waziri wa Afya kusema; “Naagiza, majibu ya saratani yatolewe na daktari bingwa.”

 Waziri Ummy alishiriki matembezi hayo kuchangia mashujaa wa saratani kupata vifaa vya mazoezi akiwa na Balozi wa Sweden nchini Charlota Ozaki,  yaliyobeba ujumbe “ Tuungane kuzipa pengo la huduma ya saratani,”

Baadhi ya Mashujaa wa Saratani wakishiriki maandamano yao leo Oktoba 21,2023.

Matembezi hayo yaliandaliwa na Ubalozi wa Sweden ukishirikiana na Asasi ya Shujaa Cancer Foundation (SCF) na Taasisi ya Saratani Ocean Road (ORCI).

 “Takwimu zinaonyesha katika kila vifo vitatu, kimoja ni kutokana na saratani. Ugonjwa huu unaongezeka asilimia 50 kila miaka kumi. Mwaka 2010 kulikuwa na wagonjwa wa saratani 24,000by, mwaka 2023 wapo wagonjwa 43,000. Lakini, asilimia 50 kati ya hao ni wanawake,” amesema Ummy na kufafanua:

“Kila mwaka katika wagonjwa wapya 42,000 wa saratani, 4,000 ni wa saratani ya matiti. Ili kudhibiti halo ni muhimu watu wajitokeza kupima saratani. Kwa akina mama ya matiti na mlango wa kizazi, kinababa tezi dume.”

Waziri huyo wa Afya amesema Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassani, inaendelea kuboresha huduma za saratani akiwataka wananchi hasa wanawake, kutambua umuhimu wa kupima  afya.

“Ni muhimu kila mwananchi awe balozi wa saratani, ugonjwa huo kwa kuwa hauchagui, masikini wanaugua hata matajiri. Hapa muhimu kupima ili kubaini matatizo mapema na kuchukua hatua,” amesema.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shujaa Cancer Foundation, Gloria Kida amesema wakati dunia inaadhimisha mwezi wa elimu kuhusu saratani ya matiti, bado wana changamoto, ikiwamo kunyanyapaliwa, kutengwa na kutelekezwa. 

Kuhusu utendaji wa SCF, Kida ambaye pia ni shujaa wa saratani amesema shirika lake limeshindwa kuwafikia wagonjwa wengi zaidi kwa ukosefu wa fedha.

Katika hotuba yake wakati wa hafla hiyo, Balozi wa Sweden nchini Charlota Ozaki ameitaja saratani kuwa ni sababu kubwa ya vifo vya wananwake akieleza ni elimu iendelee kutolewa, lakini Wizara ya Afya iendelee pia kutoa huduma kwa jamii ili wasiugue saratani.

Balozi huyo aliyejitambuliwa pia kwamba ni shujaa wa saratani ya matiti, kwani aliwahi kuugua alisema kuna umuhimu kwa wanawake kujenga tabia ya kujichunguza afya zao, lakini pia kwenda hospitali kupima, itakayowasaidia kubaini kama wana matatizo ili wapate tiba mapema.

Balozi wa Sweden nchini, Charlota Ozaki (wa nane kulia), Waziri wa Afya, Ummy Mwalim (wa tisa)  na  Mkurugenzi Mtendaji wa Asasi ya Shujaa Cancer Foundation, Glory Kida (wa saba kulia) wakiwa katika picha ya pamoja na Mashujaa wa Saratani baada ya matembezi kuadhimisha Mwezi wa Elimu ya Saratani ya Matiti na miaka 60 ya ubalozi wa Sweden nchini Oktoba 21, 2023.


 

Chapisha Maoni

0 Maoni